Mtabiri Wa Nyota Na Kufru Yake

 

Mtabiri Wa Nyota Na Kufru Yake

 

Alhidaaya.com

 

SWALI:

 

Mtabiri wa nyota na kusoma viganja vya watu vya mikono na kuwaeleza hivyo wanavyosema ameona, huyu mtu ana tofauti gani na Mpiga Ramli?

 

Kuna uhalali wa mtu kutabiriwa nyota

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Aina zote za hawa watu ni sawa ikiwa ni mtabiri wa nyota, kusoma viganja au kupiga ramli na zote hizi hizi zimekatazwa. Allaah Anasema:

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِنَّمَا الْخَمْرُ وَالْمَيْسِرُ وَالْأَنصَابُ وَالْأَزْلَامُ رِجْسٌ مِّنْ عَمَلِ الشَّيْطَانِ فَاجْتَنِبُوهُ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ ﴿٩٠﴾

Enyi walioamini! Hakika pombe na kamari na masanamu na kutazamia kwa mishale ya kupigia ramli; ni najisi na chukizo kutokana na kitendo cha shaytwaan; basi jiepusheni navyo, mpate kufaulu. [Al-Maaidah: 90]

 

Na Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amekataza jambo hilo, hivyo inatakiwa tujiweke kando kabisa.

Mambo yote haya ni haramu na yeyote mwenye kuamini kuwa jambo fulani limetokea kwa sababu ya nyota kadhaa na kadhaa amemkanusha Allaah kama Alivyosema katika Hadiyth ifuatayo:

 

"Yeyote atakayejimai (kufanya kitendo cha ndoa) na mwanamke mwenye hedhi, au kwa kutumia njia ya nyuma, au kumkaribia mtabiri na kuamini aliyoambiwa, basi amekufuru yale aliyoteremshiwa Muhammad." [Hadiyth Sahiyh imesimuliwa na AsWhabus-Sunnan na wengineo]

 

Na kufanya hivyo ni kuingia katika elimu ya ghayb (mambo yaliyofichika ya Allaah) ambayo hakuna aijuwae ila Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na humpeleka mtu kuingia katika shirk.  Na Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) humghufuria mtu dhambi zote ila shirk kama Alivyosema:

إِنَّ اللَّـهَ لَا يَغْفِرُ أَن يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَٰلِكَ لِمَن يَشَاءُ ۚ وَمَن يُشْرِكْ بِاللَّـهِ فَقَدِ افْتَرَىٰ إِثْمًا عَظِيمًا ﴿٤٨﴾

Hakika Allaah Haghufurii kushirikishwa; lakini Anaghufuria yasiyokuwa hayo kwa Amtakae. Na yeyote atakayemshirikisha Allaah basi kwa yakini amezua dhambi kuu. [An-Nisaa: 48]

 

Tafadhali pia soma Jibu la Swali kuhusu 'Kutuma Ujumbe Wa Makumbushano Ya Dini Kwa Kutishana Au Kubashiria' ambalo liko katika kiungo kifuatacho ili kujua hatari ya kutaka kujua elimu ya ghayb:

 

Bonyeza hapa:

 

Kutuma Ujumbe Wa Makumbushano Ya Dini Kwa Kutishana Au Kubashiria

 

Nasaha zetu ni kuwa tumuamini Allaah na nguzo zilizobakia za Imani kama Qadar na tutaondoka na matatizo ya kumkufuru Allaah kwa kwenda kuangaliliwa na hawa wapiga bao, ramli na wengineo.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share