Skip navigation.
Home kabah

Siku Kila Mmoja Atakayomkimbia Mwenzake

13 Dhul-Hijjah  13-01-2006

Anasema Allaah سبحانه وتعالى    

 ((فَإِذَا جَاءتِ الصَّاخَّةُ))

((يَوْمَ يَفِرُّ الْمَرْءُ مِنْ أَخِيهِ))

(( وَأُمِّهِ وَأَبِيه ))  

(( وَصَاحِبَتِهِ وَبَنِيهِ))

(( لِكُلِّ امْرِئٍ مِّنْهُمْ يَوْمَئِذٍ شَأْنٌ يُغْنِيه))

((Basi utakapo kuja ukelele))   

((Siku ambayo mtu atamkimbia nduguye))   

((Na mamaye na babaye))

 ((Na mkewe na wanawe)) 

((Kila mtu miongoni mwao siku hiyo atakuwa na lake la kumtosha)) ['Abasa:33-37]

Ibn 'Abbaas رضي الله عنه amesema kuwa "As-Saakhkhah ni moja wapo wa jina la siku ya Qiyaamah, siku ambayo Allaah سبحانه وتعالى Amewaonya waja Wake". [At-Twabariy 23:229]

Ibn Jariyr amesema: "Labda ni jina la kupigwa tarumbeta." [At-Twabariy 23:231] 

Al-Baghaawiy amesema: "As-Saakhkhah ina maana ukelele wa mngurumo wa siku ya Qiyaamah. Umeitwa hivyo kwa sababu utawazibua watu masikio. Hii ina maana kwamba utapenya katika masikio hadi kwamba utayazibua. [At-Twabariy 24:449]

Na kama Anavyosema Allaah سبحانه وتعالى kuwa siku hiyo kila mtu atamkimbia jamaa yake. Watakapoonana watakimbiana kutokana na kihoro na khofu ya hali ya juu itakayokuweko siku hiyo. Hakuna mmoja atakayetaka kumsaidia mwenziwe, hata mitume hawatotaka siku hiyo kutusaidia, kila mmoja atasema "nafsiy nafsiy" (nafsi yangu, nafsi yangu). Hata 'Iysa bin Maryam atasema: "Sitomuomba (Allaah) kuhusu yeyote ila nafsi yangu. Situmuomba hata Maryam ambaye amenizaa. [Muslim]. 

Mtume pekee atakayetuombea ni kipenzi chetu Muhammad  صلى الله عليه وآله وسلم

Hadiyth hii ifuatayo inatupa picha jinsi hali itakavyokuwa siku ya Qiyaamah:

 عن عائشة رضي الله عنها ، أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: ((يبعث الناس يوم القيامة حفاة عراة غُرلا)). فقالت عائشة: يا رسول الله، فكيف بالعورات؟ فقال:   (لِكُلِّ امْرِئٍ مِنْهُمْ يَوْمَئِذٍ شَأْنٌ يُغْنِيهِ )).  النسائي 

Kutoka kwa Bibi 'Aishah رضي الله عنها kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema

((Watu watafufuliwa siku ya Qiyaamah bila ya viatu, uchi na bila ya kutahiriwa)) Akasema Bibi 'Aishah, ewe mjumbe wa Allaah: Vipi watakuwa uchi? Akasema: ((Kila mtu miongoni mwao siku hiyo atakuwa na lake la kumtosha)) [An-Nasaiy] 

 

************