Ibaadah Tatu Usiache Maishani Mwako: 3-Wasiya Wa Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم): Swalaah Ya Witr

 

'Ibaadah Tatu Usiache Kutenda Maishani Mwako

 

Wasiya Wa Tatu Wa Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم)

Usilale Mpaka Uswali Witr

 

Alhidaaya.com

 

 

 

Juu ya kuwa fadhila ya Swalaah ya Witr ni miongoni mwa wasiya wa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), imethibiti pia fadhila zake katika Hadiyth ifuatayo:

 

 

عَنْ عَلِيٍّ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُ قَال: أَوْتَرَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ ثُمَّ قَالَ: ((يَا أَهْلَ الْقُرْآنِ أَوْتِرُوا فَإِنَّ اللَّهَ عَزَّ وَجَلَّ وِتْرٌ يُحِبُّ الْوِتْرَ))  أخرجه أبو داود في كتاب الوتر- باب استحباب الوتر برقم (1416)  والنسائي في كتاب قيام الليل وتطوع النهار- باب الأمر بالوتر برقم (1675) وصححه الألباني.

Imepokelewa kutoka kwa ‘Aliy bin Abiy Twaalib (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliswali Witr kisha akasema: ((Enyi watu wa Qur-aan! Swalini Witr kwani hakika Allaah ‘Azza wa Jalla Anapenda Witr)) [Abu Daawuwd katika Kitaab Al-Witr - Baab Istihbaab Al-Witr (1416), An-Nasaaiy katika Kitaab Qiyaam Al-Layl wa tatwawwa’ An-Nahaar Baab: Al-Amr bil-Witr (1675) na ameisahihisha Al-Albaaniy.

 

Swalaah ya Witr ni kuswali Rakaa moja, au tatu, au tano, au saba, au tisa au kumi na moja. Swalaah hii huswaliwa usiku baada ya Swalaah ya 'Ishaa. Rakaa zozote utakazojaaliwa kuswali, basi umalizie na rakaa moja au tatu za Witr ambazo huswaliwa kama ifuatavyo:

 

 

1-Kuswali rakaa mbili mbili kisha utoe salaam, kisha unamalizia na rakaa moja na kutoa salaam.

 

 

2-Au kuswali rakaa zote tatu kwa kikao cha tashahhud moja ya mwisho tu na kutoa salaam.

 

Haifai kuswali rakaa tatu zote pamoja kwa kuleta Tashahhud mbili kama vile Swalaah ya Magharibi, bali linalopasa ni kuitofautisha na Swalaah ya Magharibi kutokana na kauli ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

((… ولا تشبهوا بصلاة المغرب))

 ((… wala msiishabihishe (hiyo witr) na Swalaah ya Magharibi)) [Al-Haakim, Al-Bayhaqiy, Ibn Hibbaan, Ad-Daraaqutwniy]  

 

 

3-Unaweza kuiswali baada ya kulala wakati wowote ule utakaomka lakini kabla ya Swalaah ya Alfajiri kwa dalili ifuatayo:  

 

عنْ أبي بصرة رضي الله عنه: أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: ((إِنَّ اللَّهَ زَادَكُمْ صَلَاةً وَهِيَ الْوِتْرُ فَصَلُّوهَا بَيْنَ صَلَاةِ الْعِشَاءِ إِلَى صَلَاةِ الْفَجْرِ)) رواه احمد و صححه الألباني في سلسلة الأحاديث الصحيحة  108

Imepokelewa kutoka kwa Abu Baswrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba Rasuli wa Allaah Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam amesema: ((Hakika Allaah Amekuzidishieni Swalaah, nayo ni Al-Witr, basi iswalini baina ya Swalaah ya ‘Ishaa na Swalaah ya Alfajiri) [Imaam Ahmad na ameisahihisha Al-Albaaniy katika Silsilah Al-Ahaadiyth Asw-Swahiyha 108]

 

Ila kuiswali kabla ya kulala ni bora zaidi kutokana na wasiya wa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ili isije kukupita pindi ukishindwa kuamka usiku khasa ikiwa si mwenye uzoefu wa kuamka usiku kuswali Tahajjud. Ikiwa ni uzoefu wako kuamka kwa ajili ya Swalaah ya Tahajjud basi wakati bora kabisa kuiswali Swalaah ya Witr ni wakati wa mwisho kabla ya Alfajiri kwa dalili zifuatazo:

 

عَنْ جَابِرٍ رَضِيَ اللهُ عَنهُ قالَ: قالَ رَسُولُ الله صلى الله عليه وسلم:  ((مَنْ خَافَ أنْ لا يَقُومَ مِنْ آخِرِ اللَّيْلِ فَلْيُوتِرْ أوَّلَهُ، وَمَنْ طَمِعَ أنْ يَقُومَ آخِرَهُ فَلْيُوتِرْ آخِرَ اللَّيْلِ، فَإِنَّ صَلاةَ آخِرِ اللَّيْلِ مَشْهُودَةٌ، وَذَلِكَ أفْضَلُ )) أخرجه مسلم

Imepokelewa kutoka kwa Jaabir (Radhwiya Allaahu ‘anhu) ambaye amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Atakayekhofia kutokuamka mwisho wa usiku, basi aswali Witr mwanzo wake. Na atakayetaraji kuamka mwisho wake basi aswali Witr mwisho wa usiku (kabla ya Alfajiri), kwani Swalaah mwisho wa usiku ni yenye kushuhudiwa, na hivyo ni bora zaidi)) [Muslim]

 

Na pia,

 

  عائشة رضي الله عنها حيث قالت:  "من كل الليل قد أوتر رسول الله صلى الله عليه وسلم من أول الليل وأوسطه وآخره فانتهى وتره إلى السحر"  - أخرجه مسلم  

Imepokelewa kutoka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) ambaye amesema: “Rasuli wa Allaah Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam ameswali Witr kila usiku; mwanzo wake, katikati yake, na mwisho wake na humalizia Witr nyakati za kabla ya Alfajiri” [Muslim]

 

 

4-Suwrah za kusoma katika Swalaah ya Witr:

 

Rakaa ya mwanzo unasoma Suwrah Al-A’laa (87), Rakaa ya pili Suwrah Al-Kaafiruwn (109), Rakaa ya tatu ambayo ni ya pekee Suwrah Al-Ikhlaasw (112) kwa dalili ifuatayo:

 

عَنِ ابْنِ عَبَّاسٍ رضي الله عنهما أَنَّ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ : "كَانَ يُوتِرُ بِثَلَاثٍ : بِسَبِّحِ اسْمَ رَبِّكَ الْأَعْلَى، وَقُلْ يَا أَيُّهَا الْكَافِرُونَ، وَقُلْ هُوَ اللَّهُ أَحَدٌ " - رواه أحمد (2715) والترمذي  (462)وصححه الألباني في صحيح الترمذي .

Imepokelewa kutoka kwa Ibn ‘Abbaas (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) kwamba Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiswali Witr kwa (Suwrah) tatu; Sabbihisma Rabbikal-A’-laa na Qul-Yaa-Ayyuhal-Kaafiruwn na Qul-Huwa-Allaahu Ahad [Amesimulia Ahmad (2715) na At-Tirmidhiy (462) na ameisahihisha Al-Albaaniy katika Swahiyh At-Tirmidhiy]

 

Na pia,

 

عَنْ أُبَيِّ بْنِ كَعْبٍ رضي الله عنهما قَالَ : "كَانَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ يُوتِرُ بِسَبِّحِ اسْمَ رَبِّكَ الْأَعْلَى، وَقُلْ يَا أَيُّهَا الْكَافِرُونَ، وَقُلْ هُوَ اللَّهُ أَحَدٌ"   روى النسائي (1730) وابن ماجه (1171)  وصححه الألباني في صحيح ابن ماجه .

Imepokelewa kutoka kwa Ubayy bin Ka’ab (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akiswali Witr kwa Sabbihisma Rabbikal-A’-laa na Qul-Yaa-Ayyuhal-Kaafiruwn na Qul-Huwa-Allaahu Ahad [Amesimulia An-Nasaaiy (1730), Ibn Maajah (171) na ameisahihisha Al-Albaaniy katika Swahiyh Ibn Maajah]

 

 

Unaweza kuongezea katika rakaa ya mwisho, Suwrah Al-Falaq (113) na Suwrah An-Naas baada ya kusoma Suwrat Al-Ikhaasw kwa dalili ifuatayo:

 

عن عائشة رضي الله عنها أنها سئلت : بِأَيِّ شَيْءٍ كَانَ يُوتِرُ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ ؟ فقَالَتْ : "كَانَ يَقْرَأُ فِي الْأُولَى بِسَبِّحِ اسْمَ رَبِّكَ الْأَعْلَى، وَفِي الثَّانِيَةِ بِقُلْ يَا أَيُّهَا الْكَافِرُونَ، وَفِي الثَّالِثَةِ بِقُلْ هُوَ اللَّهُ أَحَدٌ وَالْمُعَوِّذَتَيْنِ  " رواه الترمذي (463)  وصححه الألباني في صحيح الترمذي

 

Hadiyth ya 'Aaisha (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) ambaye amesema: Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akisoma katika Rakaa ya mwanzo ya   Witr: Sabbihisma Rabikal-A'-alaa na Rakaa ya pili: Qul-Yaa-Ayyuhal-Kaafiruwn,  na Rakaa ya tatu: Qul-Huwa-Allaahu Ahad pamoja na Qul-A'uwdhu mbili (Al-Falaq na An-Naas)  [At Tirmidhiy (463) na ameisahihisha Al-Albaaniy katika Swahiyh At-Tirmidhiy]

 

 

5-Du’aa ya Qunuwt katika Rakaa  ya mwisho:

 

اللّهُـمَّ اهْـدِنـي فـيمَنْ هَـدَيْـت، وَعـافِنـي فـيمَنْ عافَـيْت، وَتَوَلَّـني فـيمَنْ تَوَلَّـيْت، وَبارِكْ لـي فـيما أَعْطَـيْت، وَقِـني شَرَّ ما قَضَـيْت، فَإِنَّـكَ تَقْـضي وَلا يُقْـضى عَلَـيْك، إِنَّـهُ لا يَـذِلُّ مَنْ والَـيْت، (وَلا يَعِـزُّ مَن عـادَيْت) تَبـارَكْـتَ رَبَّـنا وَتَعـالَـيْت.

 

Allaahummah-diniy fiyman Hadayta, wa 'Aafiniy fiyman 'Aafayta, wa Tawallaniy fiyman Tawallayta, wa Baarik-liy fiymaa A'attawyta, wa Qiniy sharra maa Qadhwayta, fainnaka Taqdhwiy  walaa yuqdhwa 'Alayka. Innahu laa yadhillu man Waalayta, walaa ya'izzu man 'Aadayta, Tabaarakta Rabbanaa wa Ta'aalayta.

 

Ee Allaah! Niongoze pamoja na Uliowaongoza, na Unipe afya pamoja na Uliowapa afya njema, na Nifanye kuwa ni mpenzi Wako pamoja na Uliowafanya  wapenzi na Nibariki katika Ulichonipa na Nikinge na shari ya Ulilolihukumu kwani Wewe Unahukumu wala Huhukumiwi. Hakika hadhaliliki Uliyemfanya mpenzi (wala hana ’izzah (hadhi)  Uliyemfanya adui) Umebarikika Ee Rabb wetu na Umetukuka.

 

[Hadiyth ya Al-Hasan bin ‘Aliy  (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa)- Aswhaabus-Sunan wane; Abu Daawuwd [1425], At-Tirmdhiy [464], An-Nasaaiy (1/252), Ibn Maajah [1178], Ahmad (1/200), Ad-Daarimiy (1/373), Al-Haakim (3/173), Al-Bayhaqiy (2/209) [497, 4987]. Taz pia Swahiyh At-Tirmidhiy (1/144) na Swahiyh Ibn Maajah (1/194), na Irwaa Al-Ghaliyl ya Al-Albaaniy (Rahimahu Allaah) (2/172)]

 

 

Unaweza pia kuongezea:

 

اللّهُـمَّ إِنِّـي أَعـوذُ بِرِضـاكَ مِنْ سَخَطِـك، وَبِمُعـافاتِـكَ مِنْ عُقوبَـتِك، وَأَعـوذُ بِكَ مِنْـك، لا أُحْصـي ثَنـاءً عَلَـيْك، أَنْـتَ كَمـا أَثْنَـيْتَ عَلـى نَفْسـِك

 

Allaahumma inniy a'uwdhu bi Ridhwaaka min sakhatwika, wa bi mu'aafaatika min 'uquwbatika, wa a'uwudhu Bika Minka, laa ukhswiy Thanaa-an 'Alayka, Anta kamaa Athnayta 'Alaa Nafsika.

 

Ee Allaah! Hakika mimi najikinga kwa radhi Zako kutokana na hasira Zako na kwa msamaha Wako kutokana na adhabu Yako, na najikinga  Kwako kutokana na Wewe, mimi siwezi kuzidhibiti sifa Zako kwa kadiri ya idadi yake, Wewe ni kama Ulivyojisifu Mwenyewe

 

[Hadiyth ya ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhwiya Allaahu ‘anhu) - Aswaabus-Sunan wane; Abu Daawuwd [1427], At-Tirmidhiy [3561], An-Nasaaiy (1/252), Ibn Maajah [1179], Ahmad (1/96, 118, 150), na taz Swahiyh At-Tirmidhiy (3/180), Swahiyh Ibn Maajah (1/194) na Al-Irwaa (2/175)]

 

Na:

 

اللّهُـمَّ إِيّـاكَ نعْـبُدْ، وَلَـكَ نُصَلّـي وَنَسْـجُد، وَإِلَـيْكَ نَسْـعى وَنَحْـفِد، نَـرْجو رَحْمَـتَك، وَنَخْشـى عَـذابَك، إِنَّ عَـذابَكَ بالكـافرين ملْحَـق. اللّهُـمَّ إِنّا نَسْتَعـينُكَ وَنَسْتَـغْفِرُك، وَنُثْـنـي عَلَـيْك الخَـيْرَ، وَلا نَكْـفُرُك، وَنُـؤْمِنُ بِك، وَنَخْـضَعُ لَكَ وَنَخْـلَعُ مَنْ يَكْـفرُك

 

Allaahumma Iyyaaka na'-budu, walaka nuswwaliy wa nasjudu, wa Ilayka nas-'aa wa nahfidu, narjuw Rahmataka wa nakhshaa 'adhaabak, inna 'adhaabaka bilkaafiriyna mulhaqq. Allaahumma innaa nasta'iynuka wa nastaghfiruka, wa nuthniy 'Alaykal-khayra, wa laa nakfuruka, wa nu-uminu Bika, wa nakhdhwa'u Laka, wa nakhla'u man yakfuruka.

 

Ee Allaah! Wewe tu Ndiye tunayekuabudu, na Kwako tunaswali na tunasujudu, na Kwako tunakimbilia na tunakutumikia, tunataraji Rehma Yako na tunaogopa adhabu Yako, kwani adhabu Yako hakuna shaka kuwa makafiri itawafikia. Ee Allaah! Hakika sisi tunakutaka msaada na tunakuomba maghfirah na tunakusifu kwa kheri na wala hatukukufurishi na tunakuamini Wewe, na tunakunyenyekea na tunamuepuka anayekukufuru

[Hadyth ya ‘Umra bin Al-Khatwaab Radhwiya Allaahu ‘anhu - Al-Bayhaqiy katika As-Sunan Al-Kubraa na ameisahihisha isnadi yake (2/211) na amesema Shaykh Al-Albaaniy (Rahimahu Allaah) katika Irwaa Al-Ghaliyl na hii isnadi Swahiyh (2/170) nayo ni mawquwfun kwa ‘Umar (Radhwiya Allaahu ‘anhu]

 

 

Adkhaar baada ya kutoa salaam katika Swalaah ya Witr:

 

سُـبْحانَ المَلِكِ القُدّوسِ

Subhaanal-Malikil-Qudduwsi

 

(mara tatu). Ya tatu yake aivute kwa sauti yake na huku akisema:

(ربِّ الملائكةِ والرّوح)

Rabbil-Malaaikati war-Ruwh

[Hadiyth ya ‘Abdur-Rahmaan bin Abzay Radhwiya Allaahu ‘anhu - An-Nasaaiy (3/244), Ad-Daaraqutwniy na wengineo, na ilivyo katika mabano ni ziada ya Ad-Daaraqutwniy (2/31), na isnadi yake Swahiyh. Angalia: Zaad Al-Ma’aad kwa tahqiyq ya Shu’ayb Al-Arnaawutw, na ‘Abdul-Qaadir Al-Arnaawutw (1/337)]

 

Bonyeza viungo vifuatavyo upate Adhkhaar hizo kwa sauti na faida yenginezo:

 

 

032-Hiswnul-Muslim: Du’aa Ya Qunuwt Ya Witr

 

033-Hiswnul-Muslim: Du’aa Baada Ya Salaam Katika Swalaah Ya Witr

 

 

 

6-Ufanyeje ukiswali Witr baada ya ‘Ishaa kisha ukaweza kuamka usiku?

 

Ikitokezea umeswali Witr baada ya ‘Ishaa kisha ukajaaliwa kuamka usiku ukapenda kuswali, basi swali Rakaa mbili mbili tu, usirudie tena witr kutokana na kauli ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam): 

((لا وتران في ليلة)) رواه الترمذي

 ((Hakuna Witr mbili katika usiku)) [At-Tirmidhiy]

 

 

 

7-Qadhwaa (kuilipa) Swalaah Ya Witr:

 

Ikiwa ni kawaida yako kuiswali Swalaah ya Witr kisha ikatokezea umepitiwa kuiswali, unaweza kuilipa asubuhi wakati wa Adhw-Dhwuhaa kwa Hadiyth zifuatazo:

 

حديث أبي سعيد الخدريّ رضي الله عنه : ((مَنْ نَامَ عَنْ وِتْرِهِ أَوْ نَسِيَهُ فَلْيُصَلِّهِ إِذَا ذَكَرَهُ))

Hadiyth ya Abu Sa’iyd Al-Khudriyy Radhwiya Allaahu ‘anhu: ((Atakayepitiwa na Witr yake akalala au akasahau basi aiswali atakapokumbuka)) [Abu Daawuwd katika Asw-Swalaah milango ya Al-Witr (1431), At-Tirmidhiy (465) na wengineo na ameisahihisha Al-Albaaniy katika Al-Irwaa (2/189)

 

Ikiwa ada yako ni kuswali usiku Rakaa tatu, basi ulipe Rakaa nne, na ikiwa ada yako ni kuswali Rakaa tano, basi ulipe Rakaa sita na kuendelea kwa uthibitisho wa Hadiyth ifuatayo:

 

 حديثِ عائشةَ رضي اللهُ عنها قالتْ": كَانَ النَّبِيُّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمَ إِذَا نَامَ أَوْ مَرِضَ صَلَّى بِالنَّهَارِ ثِنْتَيْ عَشْرَةَ رَكْعَةً"

Hadiyth ya ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) ambaye amesema: Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa anapopitiwa akalala au akiwa mgonjwa, huswali mchana Rakaa kumi na mbili. [Abu Daawuwd, At-Tirmdhiy na wengineo na ameisahihisha Al-Albaaniy katika Swahiyh Abi Daawauwd (1342) na Swahiyh At-Tirmidhiy (445)]

 

Lakini kama si kawaida yako kuswali Witr au kuamka usiku kuswali basi si juu yako kuilipa.

 

 

 

 

Share