Kutokuongea Na Mtu Kuhofu Dhambi Inafaa?

 

 

SWALI:

 

ASSALAM ALEIKUM swali langu  dini ina ruhusu kama una ona kuongea na mtu huyu kutakupatisha dhambi ni bora kwako kuto ongea naye ili ujiepushe na mathanbi dini inaruhusu kufanya hivyo au nitajiapusha vipi na mtu huyu na pili mtu hataki kuongea na wewe zaidi ya kukusalimia,  mtu kama huyu anaweza kukuharibia ibada yako isikubaliwe kwa sababu hamongei kitu kingene zaidi ya salam. naomba mniondole uzito huu niliokuwa nao na sina jibu kitu nacho ogopa ni mimi nisipate thambi.


 

 

JIBU: 

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Shukrani kwa swali lako kuhusu kutoongea na mtu kwa ajili ya kuhofia dhambi.

Hakika ni kuwa Uislamu umemkataza Muislamu kutoongea na mtu mwengine na hasa akiwa Muislamu. Uislamu ni Dini ambayo inamuongoza mtu katika haki na ukweli pamoja na kutaka kuleta amani, upendo na rehema hasa baina ya Waislamu.

 

Ikiwa kuzungumza kunaweza kukuingiza katika dhambi basi ni bora kwako kunyamaza na kutozungumza zaidi ili usiingie katika dhambi. Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema katika yale yaliyopokewa na Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa:

Mwenye kumuamini Allaah na Siku ya Mwisho na aseme jambo zuri au anyamaze” (al-Bukhaariy na Muslim).

Kusema la kheri lenye faida ni bora kuliko kunyamaza, na kunyamaza ni bora kuliko kusema jambo baya au ya upuuzi. Na kusema mambo mabaya ni sababu kuu kwa mtu kuingizwa katika Moto (at-Tirmidhiy).

 

Hata hivyo, ni wajibu kwa Waislamu kusalimiana kwani Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

Peaneni zawadi mtapendana. Je, siwaonyeshi jambo ambalo mkilifanya mtapendana? Toleaneni salaam baina yenu”.

 

Na ikiwa yupo Muislamu ambaye hataki kuzungumza nawe au wewe hutaki kuzungumza naye basi toleaneni salamu kwani hilo ni jambo lililo muhimu na huenda likaondoa yale yaliyo baina yenu.

 

Ikiwa mtu hataki kuongea nawe huwezi kumlazimisha ikiwa atakuwa ni mwenye kukutolea salamu japokuwa hilo si jambo zuri baina ya Waislamu na inatakiwa ikiwa hakuna sababu yoyote ya hilo kufanyika utumie watu wa kuzungumza naye au wewe mwenyewe ujaribu.

 

Linapotokea hilo la kutozungumza na mwenzako, halitaharibu ‘Ibadaah zako wala kuiteremsha thawabu yake, maadam mnatoleana salamu.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share