069-Swahiyh Fiqh As-Sunnah: Mlango Wa Twahara: Je Anaweza Kutayammamu Mtu Ambaye Wakati Umekuwa Mfinyu Kwake Na Wakati Wa Swalaah Utampita Kama Atatumia Maji?

 

Swahiyh Fiqh As-Sunnah

 

Mlango Wa Twahara

 

069-Je Anaweza Kutayammamu Mtu Ambaye Wakati Umekuwa Mfinyu Kwake Na Wakati Wa Swalaah Utampita Kama Atatumia Maji? 

 

Alhidaaya.com

 

 

Kuna kauli mbili za Maulamaa katika suala hili:

 

Ya kwanza:

 

Haijuzu kutayammamu hata kama wakati utampita. Limesemwa hili na Mashaafi’iy, Mahanbali na Abuu Yuusuf. [Al-Mughniy (1/166), Al-Majmu’u (2/280), Al-Istidhkaar (3/171) na Tamaam Al-Minnah (uk.132)]

 

Dalili zao ni:

 

1- Neno Lake Allaah Mtukufu:

((إذا قمتم إلى الصلاة فاغسلوا وجوهكم.... فلم تجدوا ماء فتيمموا))

((Mnaposimama kuswali, basi osheni nyuso zenu….na hamkupata maji, basi tayammamuni)). [Al-Maaidah (5:6)].

 

Wanasema: “Hapa kukosa maji kumefanywa kuwa ni sharti ya kuhalalika kutayammamu”.

 

2- Hadiyth ya Abuu Hurayrah ikiwa Marfu’u:

((لا يقبل الله صلاة أحدكم إذا أحدث حتى يتوضأ))

((Allaah Hakubali Swalaah ya mmoja wenu anapokuwa na hadathi mpaka atawadhe)). [Hadiyth Swahiyh: Imefanyiwa “ikhraaj” na Al-Bukhaariy (6954) na Muslim (526)].

 

3- Hadiyth ya Ibn ‘Umar ikiwa Marfu’u:

((لا تقبل الصلاة بغير طهور ولا صدقة من غلول))

((Swalaah haikubaliwi bila ya wudhuu, wala swadaqah ya mali haramu)). [Hadiyth Swahiyh: Imefanyiwa “ikhraaj” na Muslim (524), At-Tirmidhiy (1) na Ibn Maajah (272)].

 

Hapa mtu kaamuriwa kutumia maji. Ikiwa ataiwahi Swalaah, basi vizuri, na kama itampita kwa kuzembea kwake, basi hayo amejitakia mwenyewe.

 

Ya pili:

 

Anaweza kutayammamu na kuswali kabla wakati haujampita.

Wamelisema hili Ahlu Rra’ayi (Abuu Haniyfah na wenzake), Al-Awzaa’iy, Maalik, Ibn Hazm. Shaykh wa Uislamu amelikhitari hili.  [Al-Mughniy (1/166), Al-Muhalla (2/117), Majmu’u Al-Fataawaa (21/439,456) na Al-Awsatw (2/30)].

 

Mahanafi wameliwekea hili sharti ya kuwa ni lazima liwe kwa Swalaah ambayo haina badala yake kama Swalaah ya maiti.  [Al-Mughniy (1/166), Al-Muhalla (2/117), Majmu’u Al-Fataawaa (21/439,456) na Al-Awsatw (2/30)].

 

Hoja zao ni:

 

1- Hadiyth ya Abu Juhaym Al-Answaariy, amesema: “Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'Alayhi wa Aalihii wa Sallam) alikuja akitokea upande wa kisima cha Jamal. Mtu mmoja alikutana naye akamsalimia. Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'Alayhi wa Aalihii wa Sallam) hakuitikia mpaka alipokwenda ukutani, akapukusa uso na mikono yake. Kisha akamjibu salamu”. [Hadiyth Swahiyh: Imefanyiwa “ikhraaj” na Al-Bukhaariy (337) na Muslim (800)].

Wamesema: “Na hii ni asili katika kujuzu kutayammamu kwa ajili ya kuhofia kupitwa na faradhi”.

 

2- Ibn ‘Abdul Barri amesema katika Al-Istidhkaar (3/171):

“Kila ambaye hakuyapata maji na akachelea kupitwa na Swalaah, anaweza kutayammamu kama ni mgonjwa au msafiri kwa matni. Na kama ni mkazi na mzima, basi ni kwa maana. Na Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi".

 

3- Shaykh wa Uislamu amesema:

“Kauli sahihi zaidi ya Maulamaa ni kuwa atatayammamu kwa kila lile analolichelea kupitwa nalo kama Swalaah ya maiti, Swalaah za idi mbili na kadhalika. Swalaah kwa kutayammamu ni bora zaidi kuliko kuiacha ipite..”

 

Na amesema tena:

“Vile vile, kama hakuweza kuswali Swalaah ya Jamaa ya faradhi ila kwa kutayammamu, basi ataiswali kwa kutayammamu”.

 

Ninasema:

 

“Na huenda lililo wazi zaidi ni kuwa mtu atatayammamu ili aiwahi Swalaah, kwani tayammumi imewekwa kwa ajili ya kuuwahi wakati wa Swalaah na kuchelea kupitwa ili kuulinda wakati. Na Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi”.

 

 

Share