Skip navigation.
Home kabah

Kwa Nini Tumswalie Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ?

SWALI:

ASSALAMA  ALEYKUM !!!!

NAMSHUKURU ALLA  KWA  KUTUJAALIA  KUIPATA WEBSITE YENYE KUTUNYOOSHA JUU YA DINI YETU. BARAKA  ZA ALLA  ZIWAENDEE  WOTE  WENYE KUJIHUSISHA NA 'WEBSITE HII' ,  KILA MMOJA  KWA  KIWANGO APENDACHO  ALLAH.

SUALI  LANGU KWA  LEO  NI  HILI  : -

NINI   HEKIMA   YA  KUMSWALIA  MTUME.    NAHANGAISHWA  NA  MAWAZO YANGU KWAMBA  MTUME  NI MJUMBE WA MNWENYEENZI - MUNGU  NA AMESHAMTAKASA NA KILA OVU   NA AMESHAMWAHIDI PEPO YAKE KILA ZURI   YEYE  NI  KIONGOZI HUKO  AKHERA.  AMESHATAKASIKA - SASA  KWA NINI  TUNAHITAJI KUMUOMBEA-OMBEA KILA   WAKATI NA WENGINE HATA HATUNA KAULI NJEMA  NINI   KUMTAJA-TAJA  KIPENZI  CHA ALLAH. NADHANI  SISI  NDIO  TUKO  NJIA    PANDA,  HATUJIJUI,   TUNAHITAJI KUOMBEANA KILA WAKTI.


NAOMBA    MAFAHAMISHO.  JUU   YA  HEKIMA   ILIYOPO.
A H S A N T E.

  

 


JIBU:

  بسم الله الرحمن الرحيم الحمد لله والصلاة والسلام على أشرف الأنبياء والمرسلين وعلى آله وصحبه أجمعين و بعد

Kauli yako uliyosema kuwa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ameshatakaswa na maovu na ameshaahidiwa Pepo na kadhalika, na kwamba sisi ndio tunaohitaji kuombeana yote hayo ni kweli kabisa. Lakini bila shaka umetatizwa kufahamu hikma ya kumswalia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم hivyo Insha Allaah سبحانه وتعالى tutakufahamisha kwa kadiri tunavyoelewa na Allaah سبحانه وتعالى Anajua zaidi.

Kwanza tutambue kuwa Allaah سبحانه وتعالى Hatotuhitaji sisi tumuombee au tumswalie  Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ikiwa sisi hatutapenda kufanya hivyo. Bali sisi ndiye wenye kumhitaji Allaah سبحانه وتعالى kwa kutaraji Neema Zake na kutupa fadhila kama hizo za kumuombea na kumswalia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم. Kwa hiyo ikiwa tutampenda Mtume صلى الله عليه وآله وسلم au hatumpendi vile vile Mola wetu hatuhitaji sisi tumpende Mtume Wake kwani Yeye  Mwenyewe pamoja Malaika wake Wanampenda na wamekwishatangulia kumswalia kabla ya kutuamrisha sisi:       

Anasema Allaah سبحانه وتعالى  

((إِنَّ اللَّهَ وَمَلَائِكَتَهُ يُصَلُّونَ عَلَى النَّبِيِّ يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا صَلُّوا عَلَيْهِ وَسَلِّمُوا تَسْلِيمًا))

((Hakika Mwenyezi Mungu na Malaika wake Wanamswalia Nabii. Enyi mlioamini! Mswalieni na mumsalimu kwa salamu)) [Al-Ahzaab: 56]

Lakini kwa nini basi tumswalie Mtume صلى الله عليه وآله وسلم? Jibu la swali hakika ni refu sana itaweza kuwa ni makala ndefu au kitabu kizima cha mas-ala haya. Lakini tutafupisha ili tusiwachoshe wasomaji.

1) Kumtukuza Mtume wa mwisho

Kumswalia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ni katika kumtukuza kwani yeye ndiye Mtume wa mwisho, na hii ni neema kwetu Umma wa Kiislamu kujaaliwa sisi kuwa yeye ndiye Mtume wetu. Na Allaah سبحانه وتعالى Ametuambia kuwa sisi ni Umma bora kabisa. Bila ya yeye tusingeliweza kupata uongofu kamili (Qur'aan) na mafunzo ya Sunnah ambayo yametutoa kizani na kutuingiza katika nuru.

Na ikiwa Allaah سبحانه وتعالى Mwenyewe Amemtukuza kwa kumtofautisha na mitume mingine yote, kwani wote Amewaita kwa majina yao katika Qur'aan isipokuwa Mtume Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم pekee Amemwita aidha 'Ewe Nabii', Ewe Mtume. Basi sisi kumswalia ndio mojawapo ya   njia ya kumtukuza

        2)      Ni ibada kwetu

Kwa vile ni amri kutoka kwa Mola wetu kama tulivyoona katika aya hiyo ya juu, na ndio maana tunamswalia mpaka kwenye Swalah zetu za fardhi na za Sunnah, bila ya kumswalia Swalah haikamiliki.

        3)    Rahma kwetu kupata fadhila na thawabu zaidi

Binaadamu kila siku ana makosa hata awe anafanya ibada vipi, kwa hiyo ni neema kwetu kuzidishiwa fadhila kwa kutekeleza vitendo vya Sunnah fulani ili kujiongezea thawabu na  daraja ya Pepo kwani hakuna mtu asiyependa ziada ya neema.

Fadhila ya Kuswaliwa na Allaah سبحانه وتعالى mara kumi

 عنْ عبد اللَّه بن عمرو بن العاص ، رضي اللَّه عنْهُمَا أنَّهُ سمِع رسُول اللَّه صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم يقُولُ : (( من صلَّى عليَّ صلاَةً ، صلَّى اللَّه علَيّهِ بِهَا عشْراً))   رواهُ مسلم

Imetoka kwa 'Abdullah ibn 'Amru ibn Al'Aasw رضي اللَّه عنْهُمَا kwamba kamsikia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم anasema, ((Atakayeniswalia Swalah moja Allaah Atamswalia mara kumi)) [Muslim]

Maana ya Swalah ya Allaah سبحانه وتعالى  na Malaika Wake:

Swalah ya Allaah سبحانه وتعالى  kwa waja Wake ni: Rahma na kuwasifu kwa malaika.

Swalah ya Malaika kwa waumini  ni:

Du'aa na kuwaombea maghfirah.

 

Kupata daraja ya Pepo karibu naye Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  :

عن ابن مسْعُودٍ رضي اللَّه عنْهُ أنَّ رسُول اللَّهِ صَلّى اللهُ عَلَيْهِ وسَلَّم قال : (( أَوْلى النَّاسِ بي يوْمَ الْقِيامةِ أَكْثَرُهُم عَليَّ صلاةً)) رواه الترمذي وقال : حديثٌ حسنٌ

Imetoka kwa ibn Mas'uud رضي اللَّه عنْهُ kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  

amesema, ( (watu wa mwanzo kwangu (watakaokuwa karibu yangu)  siku

ya Qiyaamah ni wale wanaoniswalia sana)) 

[At-Tirmidhy na kasema ni Hadiythi Hasan]  

Vile vile kumuombea Du'aa, mfano du'aa baada ya adhaan ni fadhila kwetu kuwa atakayefanya hivyo atakuwa miongoni mwa atakayeombewa Shufaa na Mtume صلى الله عليه وآله وسلم siku ya Qiyaamah.

        4)    Kudhihirisha mapenzi yetu kwake

Muumini ni yule mwenye kumpenda khaswa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kabla ya kupenda chochote hata nafsi yake kwani ilipoteremka aya hii:

((النَّبِيُّ أَوْلَى بِالْمُؤْمِنِينَ مِنْ أَنفُسِهِمْ))  

((Nabii ni bora zaidi kwa Waumini kuliko nafsi zao)) [Al-Ahzaab:6].

'Umar رضي الله عنه  alisema kuwa yeye anampenda Mtume kuliko chochote ila nafsi yake. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akamuambia 'Umar kuwa hadi ampende hata kuliko nafsi yake ndipo yatakapothibitika mapenzi yake, naye 'Umar akakubali kuwa anampenda kuliko hata nafsi yake. Kwa hiyo na sisi waumini tuwe na mapenzi makubwa ya kumpenda na dalili mojawapo ni kupenda kumswalia.

        5)    Kumswalia kwetu ni thawabu alizokwishaahidiwa.

Allaah سبحانه وتعالى Amekwishamuahidi Mtume Wake kuwa atapata malipo mengi yasiyokatika:

((وَإِنَّ لَكَ لَأَجْرًا غَيْرَ مَمْنُونٍ))

((Na kwa hakika wewe una malipo yasiyokatika)) [Al-Qalam: 3]

Mbali ya kuwa ni malipo yake kwa sababu ya utume wake na kufikisha ujumbe kwa tabu na maudhi, vile vile kumswalia kwetu kila siku kama katika Swalah kila mara na kuswaliwa na Umma mzima wa Kiislamu tokea utume wake hadi siku Qiyaamah ni mojawapo ya kuthibitisha kauli ya Allaah سبحانه وتعالى  hiyo.

Mwisho kama ulivyosema kuwa sisi ndio tuliokuwa njia panda na tunaohitaji kuombeana, bila shaka tunahitaji kufanya hivyo, na kwa hiyo pia kumswalia Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ni kutuzidishia uzito wa mizani zetu za mambo mema na kufanya nyepesi mizani za mambo maovu.

 

        Wa Allaahu A'alam