Imaam Muhammad Bin 'Abdil-Wahhaab (رحمه الله):

 

 

Imaam Muhammad Bin 'Abdil-Wahhaab - Maisha Yake Na Harakati Zake

Shaykh ‘Abdul-‘Aziyz Bin ‘Abdillaah Bin Baaz

 

 Imetarjumiwa na Alhidaaya.com

 

 

Imaam Muhammad bin ‘Abdil-Wahhaab alikuwa ni mtu muhimu, mwana da’awah mashuhuri na Mwanachuoni hodari aliyekuwa katika karne ya kumi na mbili. Alielimishwa na baba yake mzazi kwenye mji wa Uyayna, kijiji cha Yamamah ndani ya Najd, kaskazini magharibi ya mji wa Riyadh. Alijifunza kusoma Qur-aan katika umri wake mdogo na akaihifadhi akiwa chini ya umri wa miaka kumi. Akafanya bidii kwenye masomo yake na kuendelea kujifunza chini ya usimamizi wa baba yake. Shaykh ‘Abdul-Wahhaab bin Sulayman ambaye alikuwa mwanafalsafa na jaji mkuu wa Uyaynah.

 

Alipobaleghe Shaykh alisafiri kutoka Makkah kwenda Madiynah kusoma waliyoyasoma watu wengine maarufu walioko huko, na baadaye alielekea Iraq (Basrah) kutafuta elimu zaidi.Hatimaye akaamua kuanza harakati zake hapo Iraq. Alianza kuwafundisha watu Tawhiyd na Sunnah za Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Akawatangazia waislam kuwa ni wajibu kufuata dini yao kwa uhakika kutokana na Qur-aan na Sunnah. Alijiingiza katika mijadala na kushauriana na wanachuoni na akawa maarufu. Japokuwa baadhi ya wanavyuoni wadhaifu wasiokuwa na hoja walimpinga na kumfanya akabiliane na misukosuko, vitisho na kukasirikiwa, ndipo alipoamua kuondoka Basrah kuelekea Az-Zubayr kupitia Al-Ahsan na mwisho kufika Huraymila ambapo pia alikabiliana na misukosuko na mateso zaidi chini ya mikono ya madhalimu.

 

Kwa sababu aliwajumuisha waja wema na kuwatenga madhalimu. Pia aliwashawishi watawala kuwahukumu wadhalimu kiuhakika. Hiyo ilisababisha baadhi ya watu kuyaweka maisha yake hatiani lakini Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) alimnusuru. Baadaye akaamua kurudi kwao Uyayna, ingawa kipindi hicho kulikuwa chini ya utawala wa mtoto wa mfalme ‘Uthman bin Muhammad bin Muammar, ambaye alimpokea Shaykh kwa ukarimu na kumuahidi kumuunga mkono na kumsaidia kuwaita watu katika Uislam.

 

Watu wa Najd kwa kipindi hicho walikuwa wakiishi kwa sheria ya kutokuamini na kuikubali imani yoyote ile.

 

Dini ya kuamini miungu mingi ilikuwa imeenea kote, watu walikuwa wakiabudu kubaa (makaburi yaliyojengewa) miti, mawe, mapango, au mtu yeyote aliyedai kuwa ni (walii) mtakatifu. Uchawi na utabiri (unajimu) pia vilisambaa. Ndipo Shaykh alipoona kwamba imani ya miungu mingi inatawala watu na hakuna hata mmoja asiyependezewa na hilo, hakuna hata mmoja aliyekuwa tayari kuwaita watu warudi kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’alaaa). Akaamua kujitumikisha peke yake kwa uvumilivu katika konde (mahali pa uwanja). Akajua hakuna lolote kitachofaulu ila jihaad, uvumilivu na kufikwa na matatizo.

 

Shaykh akaendelea kuwarudisha watu kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na kuwaongoza katika njia nyoofu na mapenzi yanayosababishwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Hatimaye Shaykh akawa maarufu ndani na nje ya Uyaynah. Watu wakawa wanakuja Uyayna kuja kumuona kutoka maeneo ya jirani na vijijini. Na pia akaanza kuwaandikia wanavyuoni wengi kuwaomba wamuunge mkono na wabaki na juhudi ya kusaidia dini ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) na kupigana kuipinga ibada ya miungu mingi. Wanavyuoni wengi kutoka Najd, Makkah na Madiynah walikubali maombi yake, ingawa baadhi hawakuyakubali waliyapinga na wakamkatisha tamaa na harakati zake, kumlaani na kumweka mbali nao.

 

Shaykh na watu aliokuwa nao wakajigawanya katika matabaka mawili, kundi moja wakiwemo watu waliokosa elimu na maarifa ya kujua chochote kuhusu Uislaam na wakafuata ushetani, wakibadili mambo ya kheri, na kufanya ushirikina n.k.

 

Ilimradi waliyafuata yale mababu zao waliyokuwa wakiyafanya. Na Qur-aan inaelezea habari ya watu hawa  Tumewakuta wazee wetu wakitumia dini kwa njia yao na sisi kwa hakika tumefuata nyao zao 

 

Na kundi la pili, kwa upande mmoja walikuwa na elimu lakini walimkabili Shaykh kinyume kutokana na wivu na vilevile walihofia watu wangewauliza juu ya imani zao za asili ya kwamba kwa nini wamekaa kimya na hawakuwaonya na haya na yale juu ya Ibliys mpaka alipowajia Muhammad ‘Abdul-Wahhaab?

 

Lakini Shaykh aliendelea kwa ustahamilivu kutafuta msaada wa Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa misukosuko na kila jambo. Alijitahidi kwa dhati kuisoma Qur-aan na vitabu mbalimbali vya manufaa na maana. Pia alikuwa mtaalamu katika kuitafsiri na kuiandika kama ilivyo, na akafanya kazi kubwa ya kusoma maisha ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na maisha ya Maswahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhu)

 

Shaykh akaendelea kufundisha na kutoa da’awah (kulingania), hatimaye akashawishika kidhati na kwa vitendo kuondoa dini ya miungu mingi pale alipoona baadhi ya watu ni wagumu kurudi katika Uislaam. siku moja akamwambia gavana (mtawala) wa mji hebu twende tukalivunje lile zege lililojengewa juu ya kaburi la Zayd bin Al-Khattwaab (Radhwiya Allaahu 'anhu) (Zayd bin Al-Khattwaab alikuwa kaka wa ‘Umar bin Al-Khattwaab (Radhwiya Allaahu 'anhu) na ni shahidi, ambaye alikufa katika vita dhidi ya Musaylamah Al-Khaddhaab 12 H akazikwa na baadaye watu wake wakamjengea zege juu ya kaburi lake. Na imeamriwa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kulaani kitendo cha kujengea zege, kuta au Misikiti juu ya makaburi. Vilevile ngome hiyo imewasababisha watu kuwa na imani ya miungu mingi hivyo hakuna njia ila kuivunja ngome hiyo.

 

Mwana wa mfalme akakubali na akaanda jeshi la watu wake mia sita na wakapiga gwaride mpaka kwenye kaburi hilo wakiongozwa na Shaykh. Ama baada ya kukaribia ngome hiyo, watu wakaja kuilinda ngome hiyo lakini baada ya kuliona jeshi la mtoto wa mfalme wakabadili mawazo. Ndipo Shaykh akachukua hatua ya kulivunja na kuiondoa ngome hiyo. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Ameliondoa kwa mikono yake na alhamdullilah, hakuna hata kipande kilichobaki hadi hii leo. Vilevile kulikuwa na mangome mengine, mapango, miti n.k vyote vilivyunjwa na kuondolewa. Hakuishia hapo, Shaykh aliendelea na harakati zake za maneno na vitendo ambapo ilimfanya azidi kuwa maarufu.hata siku moja mwanamke mmoja alimjia na kumwambia kuwa amefanya zinaa. Baada ya kuamini kwamba amesema ukweli, kaolewa na kakiri kosa lake bila ya ukaidi, naye Shaykh akaamuru kutokana na Sunnah aadhibiwe kwa kupigwa mawe mwanamke huyo mpaka afe, kwani yeye sasa amekuwa ni jaji wa Uyayna.

 

Ndipo mtoto wa mfalme wa Al-Ahsa na vijiji vilivyomzunguka kutia wasiwasi juu ya nafasi aliyokuwa nayo Shaykh na kukhofu kutokana na kufanya makosa, kuiba, kuua ambayo yalikuwa ni mambo ya kawaida kwao. Ndipo mtoto wa mfalme huyo akamwandikia barua ya vitisho na kumuamuru mtoto wa mfalme wa Uyayna kumuua Shaykh, na mtoto wa mfalme wa Uyayna akamwendea Shaykh na kumwambia kuwa jahili amemtumia ujumbe wa yeye kufanya kadha wa kadha ingawa yeye hakusudii kufanya lolote isipokuwa ana hofu kubwa ya kupigana na mtoto wa mfalme huyo (Al-Ahsa) basi akamuomba afikirie kuondoka/kuhama. Shaykh akajibu, “Mimi sina kikubwa ninachokifanya ila kuwaita watu katika Uislam na kukiri kidhati na kuamini kwamba hakuna Mola apaswaye kuabudiwa ila Allaah na Muhammad ni mjumbe Wake. Yeyote atakayeushika haraka Uislam na akauunga mkono ukweli wake basi Allaah Atamsaidia yeye na atamfanya kuwa kiongozi wa nchi za maadui. Na kama utateseka na ukastahamili na kuikubali hii Dini, basi kuwa na fuhara ya kwamba Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) atakusaidia na atakulinda na mtoto wa mfalme (jahili wa al-ahsa) na wengineo. Allaah pia atakupa nguvu juu ya nchi yake na watu wake”. Lakini ‘Uthmaan akasema “Ah! Shaykh, lakini sisi hatuwezi kupigana naye wala kukidhi matakwa yake.” Kwa hiyo Shaykh akaamua kuondoka Uyaynah kuelekea Dariyyah tena kwa mguu kwa sababu Uthman hakumpatia usafiri wa aina yoyote.

 

Alipofika Dariyyah, akafikia na kukaa katika nyumba moja ya mtu mwema na mwenye umaarufu mzuri hapo Dariyyah, lakini alimhofia mtoto wa mfalme Muhammad Bin Sa’ud. Na Shaykh akamwambia “kuwa mwenye kushukuru na omba yaliyo mema mimi sina kikubwa ninachokifanya ila kuwaita watu katika dini ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) naye ataipa ushindi”.

 

 

Habari za Shaykh kuwasili hapo Dariyyah zikamfikia Muhammad bin Sa’ud. Inasemekana mkewe ndio aliyemjulisha habari hizo mwanzo. Mkewe alikuwa mkarimu na mchamungu na akamfahamisha mumewe kwa kumwambia, “Hii ni bahati kubwa/njema umeletewa kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) mtu ambaye anawaita watu katika Uislaam, anawaita katika Qur-aan na Sunnah za Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) bahati iliyoje? Mkimbilie haraka na umuunge mkono wala usimpinge au kumkataza kwa hayo” Muhammad Bin Sa’ud akakubali ushauri wa mkewe na akaenda kwa Shaykh na akafanya mkataba naye kwamba asiondoke nchini hapo.

 

Hapa ndipo Shaykh akaamua kuishi Dariyyah. Watu mbalimbali wakaanza kuja kwake kusoma kutoka sehemu mbalimbali kama Uyayna, Iraq, Manfooha, Riyadh na sehemu mbalimbali za jirani. Akaheshimika, akapendwa na akaungwa mkono na watu . Shaykh akapanga hotuba (mawaidha) kwa vipengele (mada) tofauti kama Imani, Qur-aan tukufu, Qur-aan na mafunzo ndani yake, haki na sheria za kiislam, hadith na maelekezo yake, na mengineyo. Akaanda darasa kwa umma na pia kwa watu maalum. Na akaendelea na harakati na shughuli za kulingania hapo Dariyyah. Aliwaandikia wanavyuoni pamoja na watawala malalamiko na maonyo yake juu ya suala la kuabudu miungu mingi na kuleta na kubadili mambo yaliyokusudiwa yawe kuwa mambo mapya yasiyofaa. Kutokana na kitendo cha kuwasiliana na wanavyuoni na watawala juu ya kupigania haki kwa ajili ya Allaah, Shaykh akawa maarufu. Harakati zake zikaendelea na kuenea kwenye nchi za Kiislam na nchi nyinginezo. Kama ijulikanavyo kila jema halikosi ubaya basi na kila mlinganiaji hakosi maadui, Allaah, Mwenye neema kubwa Amesema katika Qur-aan:

 

وَكَذَٰلِكَ جَعَلْنَا لِكُلِّ نَبِيٍّ عَدُوًّا شَيَاطِينَ الْإِنسِ وَالْجِنِّ يُوحِي بَعْضُهُمْ إِلَىٰ بَعْضٍ زُخْرُفَ الْقَوْلِ غُرُورًا ۚ وَلَوْ شَاءَ رَبُّكَ مَا فَعَلُوهُ ۖ فَذَرْهُمْ وَمَا يَفْتَرُونَ ﴿١١٢﴾

Na hivyo ndivyo Tulivyojaalia kwa kila Nabiy maadui - mashaytwaan katika wana Aadam na majini wakidokezana wenyewe kwa wenyewe maneno ya kupambapamba na ya ghururi. Na lau Angetaka Rabb wako wasingeliyafanya hayo. Basi waachilie mbali na wanayoyatunga. [ Al-An’aam: 112].

 

 

Baada ya Shaykh kuwa maarufu kwa ajili ya da’awah yake, na maandishi yake kuwafikia wengi miongoni mwa watu, wengi waliokuwa na chuki wakabainika kama wapinzani. Kundi moja lililokuwa na wanavyuoni wadhaifu liliamini mambo ya kweli kuwa uongo na mambo ya uongo kuwa kweli, pia waliamini kujengea kuta makaburi na kuweka jiwe la kumbukumbu katika kaburi (Kiislam) ni mambo yanayoendana. Na kundi la pili walikuwa wakijihusisha na elimu na ujuzi lakini walikosa ujuzi wa kujua ukweli wa malengo ya Shaykh. Na kundi la tatu ndio walimpinga kabisa kutokana na kuhofu kufukuzwa katika nafasi au vyeo vyao. Walionyesha unyanyasaji ili watu wanaouunga mkono malengo ya Uislam wasifike walikodhamiria ili wawanyang’anye nafasi au vyeo vyao na hata miji yao. Kwa hivyo tunaona wengine walimpinga kwa ajili ya Dini, wakati wengine walimpinga kisiasa bali walijificha kielimu ndani ya dini ili kufaidika na uadui wa wanavyuoni hao dhidi yake. Saa nyingine wapinzani wake walidai kuwa Shaykh alikuwa ni mfuasi wa Khawaarij, na saa nyingine walimlaumu bila hata kujijua na nje ya upeo wa elimu zao nk. Hivyo malumbano hayo ya majibishano ya maneno yaliendelea katika mijadala kwa mabishano. Aliwaandikia na wao walimrudishia majibu na yeye aliwahakikishia kuwa waliyoyajua si ya kweli ndipo wingi wa namba za maswali na majibu yakawajumuisha watu na wakazidi kuongezeka. Na Alhamdullilahi, mambo mengi yaliandikwa na kuchapishwa katika vitabu. Baadaye Shaykh akajiingiza katika Jihaad 1158 H, aliwaandikia watu waingie katika ukumbi wa Jihaad na kuacha kuabudu miungu mingi ibada ambayo ilikuwa imeenea nchini kwao.

 

Ndipo Shaykh akafanya juhudi ya kutangaza Jihaad kwa miaka hamsini (50) kutoka 1158 A.H mpaka 1206 akafariki. Aliukabili ugumu kuwa wepesi katika kila lengo lake kama Jihaad, kulingania, kutokubali malumbano na mabishano mpaka watu wakaamini upesi na walikubali kuvunja mazege na kuta zilizokuwa juu ya makaburi hayo na wakafuata na kukubali shari’ah za Kiislam, na kuzivunja sheria na masharti yote yaliyowekwa na mababa na mababu zao. Na baada ya kifo cha Shaykh, watoto wake, wajukuu zake na waliomuunga mkono waliendeleza malengo yake na mataabiko kwa ajili ya Allaah.

 

Share