Kujiangalia Katika Kioo Usiku Haifai?

 

SWALI:

Allah awalipe ndugu zangu katika Imani kwa kazi nzito mnayoifanya na awafanyie sahali ndani ya kazi hii, awafanyie sahali ndani ya maisha ya dunia na Akhera.

Swali: Nimepata kumsikia mmoja wa wahadhiri wa Kiislamu, akisema haifai kwa muislamu kujiangalia kwenye kioo wakati wa usiku. Naomba ufafanuzi juu ya kauli hii. Asante

 


 

 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani zetu za dhati kwa ndugu yetu aliyeuliza swali hilo. Ingekuwa ni bora kwa ndugu aliyesikia muhadhara huo kutuandikia nasw ya Hadiyth ili tupate kuiangalia. Mas-ala ya kujitazama kwenye kioo yamekuja kwa ujumla bila kuainisha wakati wenyewe.

Miongoni mwa Hadiyth ni kile kitendo cha ‘Abdullaah bin ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhuma) aliyejitazama mara moja kwenye kioo kwa kitu kilichokuwa kikimsumbua akiwa katika hali ya Ihraam (Maalik). ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) ameHadiythia kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipokuwa akijitazama kwenye kioo alikuwa akisema:

Sifa zote njema anastahiki Allaah, Ee Allaah! Nijaalie niwe na tabia nzuri kama Ulivyolifanya umbile langu kuwa zuri(Ibn As-Sinniy).

 

Hizi Hadiyth ni za jumla kumaanisha wakati wowote. Kwa hiyo, kutofaa jambo lolote ni lazima kuwe na dalili. Twatumai utakuwa umepata picha sahihi ya suala hilo.

 

Na Allaah Anajua zaidi.

 

Share