Wakristo Ni Ahlul-Kitaab Na Hali Wanaamini Waungu Watatu (Utatu Mtakatifu)?

 

SWALI:

Assalaam Alaykum!

Nashukuru kwa ujumbe wa ijumaa ambao mara nyingi hutupa mafunzo hasa sie ambao pengine hatupati nafasi za kuhudhuria mawaidha masjid. Nimepitia ujumbe wa jana na kukuta mambo ya kuwaoa ahlul kitaab. Niliposoma kwa ndani zaidi naona pameelezwa kuwa wakristo nao pia ni Ahlil kitaab. Hapa ndio nilipo changanyikiwa.

Wajua sie watu wenye elimu ndogo mara nyingi twajifunza kwa kukariri na unapomsikia mtu anaeleza vingine unatatizika sana katika mambo haya ya "Shubhaat".

Ninavyo jua mimi wakristo hawa ndio ambao wana waungu watatu. Kwa imani zao wao wanadai kuwa kuna mungu mwana, mungu mama na mungu roho mtakatifu. Sina uhakika na wakriso wote duniani kuwa wana amini hivi lakini nilipo kuwa chuoni nilikutana na wakristo tokea karibu nchi 30 tofauti duniani na hawa wote waliamini kuwa na utatu katika uungu.

Ahlul kitaabi ninao wajua mimi ni wale walomfuata nabii Issa (Alayhis Salaam) na hawakuwahi kumshirikisha Allah (Subhaanahu Wataala). Wakati nabii Issa (Alayhis Salaam) anakaribia kukamilisha kipindi chake cha utume aliwaambia wafuasi wake kuwa kuna mtume anaeitwa Ahmad (SwallaAllahu Alayhi Wassallaam) ambae atashika hatamu za uongozi baada yake.

Sasa mimi naomba ufafanuzi hapa kuhusu hawa ahlul kitabi ambao pia ni wakristo sheikh wangu? Wanapatika nchi gani labda na wanafuata kitabu gani mana kama ni Taurati sidhani kama hawa waristo wa leo wanayo ikiwa kitabu chao cha biblia wanakibadilisha kila leo.

Nawatakia kila la kheri.

 


JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kuwaoa Ahlul Kitaab. Awali ya yote ni kuwa taqriban wanazuoni wote wameafikiana kuwa Ahlul Kitaab wanajumuisha Mayahudi na Wakristo kwa mujibu wa Qur-aan na Sunnah za Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Hili ni suala lenye utata kidogo kwa sababu ya misimamo tofauti ya wanazuoni. Na utata mwengine unakuja kwa sababu ya kuchukua baadhi ya ibara na mistari ya Biblia ambayo kwa uhakika si kigezo chetu katika suala hilo na mengineyo. “Shubuhaat” ni jambo ambalo Muislamu hafai kulifanya kwani hilo ndilo alilotuambia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) katika Hadiyth ya an-Nu‘maan bin Bashiyr (Radhiya Allaahu ‘anhuma):

Yeyote mwenye kuepuka ya Shubuhaat, ameihifadhi Dini na heshima yake. Na yeyote mwenye kuingia katika Shubuhaat ameingia katika haramu” (al-Bukhaariy na Muslim).

 

Hakika ni kuwa hata Wakristo waliokuwa wakati wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) walikuwa wana waungu watatu. Na hao Wakristo walikuwa na Imani hiyo unayoizungumza na kwa ajili hiyo Allaah Aliyetukuka Akasema:

Kwa hakika wamekufuru waliosema: Allaah ni wa tatu wa Utatu. Hali hakuna mungu ila Mungu Mmoja. Na ikiwa hawaachi hayo wanayoyasema, kwa yakini itawakamata adhabu chungu wale wanaokufuru” (5: 73).

Si hilo tu bali pia walikuwa wanamuabudu mama yake, ‘Iysa, yaani Maryam na Allaah Akawakataza kwa kauli Yake:

Masihi mwana wa Maryam si chochote ila ni Mtume. Wamekwishapita Mitume kabla yake. Na mama yake ni mwanamke mkweli. Wote wawili walikuwa wakila chakula. Angalia jinsi Tunavyowabainishia Aayah, kisha angalia vipi wanavyogeuzwa” (5: 75).

Kuelezewa kuwa wote wawili walikuwa wanakula chakula ni kuonyesha kuwa hao hawawezi kuwa wana sifa ya uungu. Kwa hiyo utatu huo ni madai batili nay a uovu, na madai hayo ya utatu yalikuwa hata kwa Wakristo waliokuwa katika enzi za Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Pia tufahamu kuwa si Wakriso wote duniani kuwa wanaamini hivyo kwani wapo wengine ambao hawaamini utatu mtakatifu. Na hao ambao hawaamini hivyo walikuwepo wakati wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), mfano ni kina Najjaash, mfalme wa Uhabashi ambaye baada ya kusomewa Aayah za Surah Maryam na Ja‘far bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu) alisema tofauti yenu na yetu haizidi msitari huu (akachora msitari kwenye ardhi), na tunafahamu kuwa baadaye Najjaash huyo alifariki hali akiwa keshasilimu.

Hata hivyo, wale wenye kuamini utatu ni wengi kwa kiasi kikubwa sana.

 

Ama wale waliomfuata Nabii ‘Iysa (‘Alayhis Salaam) walikuwa ni Waislamu kwa mujibu wa Qur-aan. Allaah Aliyetukuka Anasema:

‘Iysa alipohisi kuwa kati yao pana ukafiri alisema: Nani wasaidizi wangu kwa Allaah? Wanafunzi wake wakasema: Sisi ni wasaidizi wa Allaah. Tumemuamini Allaah, na shuhudia kwamba sisi hakika ni Waislamu” (3: 52).

Na zipo Aayah nyingine katika Qur-aan zinazotufahamisha hilo. Na kwa kuwa walikuwa ni Waislamu hawakuwahi kumshirikisha Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala). Ukristo ulianza muda mwingi baada ya kuondoka duniani Nabii ‘Iysa (‘Alayhis Salaam).

 

Wapo wanazuoni wengine wanasema hawa Wakristo wa sasa si Ahlul Kitaab kwa kuwa Nabii ‘Iysa (‘Alayhis Salaam) alitumwa kwa kondoo waliopotea wa wana wa Israili. Na kwa kuwa hawa Wakristo wa sasa ni wana wa Israili hawawezi kuwa Ahlil Kitaab. Lakini muono huo wa wanazuoni hao hauna dalili yoyote bali kinyume chake ndio sahihi kabisa. Tunakuta kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipowatuma Maswahaba zake kwenda kulingania baadhi ya makabila ya Kiarabu yalioingia katika Ukristo alikuwa akiwausia kutowavamia au kuwaua watawa walio jitenga katika hekalu zao. Na kuwa hawa walikuwa wanachukuliwa kuwa ni Ahlul Kitaab na ndivyo walivyochukuliwa Wahabashi. Tunaona kuwa Waarabu wakati huo na Wahabashi hawakuwa ni wana wa Israili lakini walikuwa wanajulikana kama Ahlul Kitaab.

 

Kwa muhtasari wa maneno ni kuwa kila anayejiita kuwa yeye Mkristo basi anachukuliwa hivyo. Kwa jinsi hiyo watakuwa wanapatikana katika nchi zote hapa duniani. Na wao ikiwa ni Wakristo wanafuata Biblia ambacho ni mkusanyiko wa vitabu vingi ilhali Mayahudi wanafuata Agano la Kale peke yake katika hiyo Biblia. Na tufahamu ya kuwa wakati wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) tayari Biblia ilikuwepo ikitumika na Wakristo hata Waraqah bin Nawfal binamu ya Khadijah bint Khuwaylid (Radhiya Allaahu ‘anha), mkewe Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa anazo nyaraka hizo kwa Kiarabu wakati Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anapewa Utume. Mbali ya kuwa Biblia hiyo imetiwa mikono ya waandishi kama inavyosema yenyewe katika kitabu cha Yeremia 8: 8.

 

Kubadilishwa kwa vitabu hivyo ni wazi kwani Allaah Aliyetukuka Hakutoa dhamana ya kuvihifadhi. Na kubadilishwa huko kulikuwepo kukifanywa na Mayahudi wakati wa Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mwenyewe. Kuhusu kubadilishwa huko tunaelezewa na Allaah Aliyetukuka:

Basi ole wao wanaoandika kitabu kwa mikono yao, kisha wakasema: Hiki kimetoka kwa Allaah, ili wachumie kwacho pato dogo. Basi ole wao kwa yale iliyoandika mikono yao, na ole wao kwa yale wanayoyachuma” (2: 79).

 

Tunamuomba Allaah Aliyetukuka Atuongoze katika njia nyoofu na Atuepushe na upotevu wa njia zote potofu.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share