Kuandika Aayah Za Qur-aan Katika Ukuta

 

 

Kuandika Aayah Za Qur-aan Katika Ukuta

 

Alhidaaya.com

 

 

 

SWALI:

 

Assalama alaekum wa Rahmatu llahi wa barakatu.

 

Swali jee inafaa kuandika aya za Quraan katika ukuta wa nyumba compound wall. 

 

JIBU:

 

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Hebu tulitazame swali hili kwa makini. Je, hizi Aayah ambazo zitaandikwa kwenye ukuta wa nyumba zimeandikwa kwa lengo gani? Ikiwa lengo ni kuondoa hasadi, au urogi, au kuwa kama kinga kutokana na mashaytwaan hilo litakuwa halifai kwani kuondoa hayo yote Aayah zinatakiwa zisomwe sio kuandikwa. Na kufanya hivyo kutampelekea mtu katika ushirikina.

 

Inatakiwa tuelewe na kufahamu kuwa Qur-aan haikuletwa kutundikwa nyumbani au kuandikwa ukutani bali kusomwa na kuongoza wanaadamu. Hivyo, inatakiwa iwe katika vifua vya watu pamoja na kutiwa katika matendo ya wanaadamu ili wapate ufanisi hapa duniani na Kesho Aakhirah. Allaah ('Azza wa Jalla)  Anasema:

 

ذَٰلِكَ الْكِتَابُ لَا رَيْبَ ۛ فِيهِ ۛ هُدًى لِّلْمُتَّقِينَ ﴿٢﴾

Hiki ni Kitabu kisicho na shaka ndani yake, ni mwongozo kwa wenye taqwa [Al-Baqarah: 2]

 

 

Na Anasema pia Allaah ('Azza wa Jalla):

 

شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِي أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَىٰ وَالْفُرْقَانِ ۚ  

Mwezi wa Ramadhwaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan ili iwe mwongozo kwa watu na hoja bayana za mwongozo na pambanuo (la haki na batili). [Al-Baqarah: 185]

 

 

Kwa hiyo, Qur-aan inatakiwa iwapatie uongofu Waumini na hilo halitopatikana kwa kuandika Aayah kwenye kuta bali kusomwa, kuifahamu na kufuata maagizo yake pamoja na kuacha makatazo yaliyo ndani. Na kwa wanaadamu wengine pia ni lazima waisome ndio wapate uongofu, Aayah ambazo ni chache zilizoandikwa katika ukuta hazitowafaidisha bali itakuwa ni kuzifanyia Aayah hizo mzaha na hilo halifai.

 

 

Wengine utakuta wanatoa hoja dhaifu kuwa kuwekwa Aayah ukutani kunamkumbusha mtu Qur-aan! Lakini je, kumkumbusha huko kuisoma Qur-aan ni kwa kwa pale tu anapoiona na akirudi kwake au akienda kwengine husahaulika.  Muumin, mwenye imani ya kweli huisoma Qur-aan kila siku na haihitajii kukumbushwa na Qur-aan za kutani.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share