Nigawe Kwa Nani Urithi Wa Mama Mkristo

SWALI:

Asalaam Alaykum Warahmatullah Wabarakatuh

Mama yangu ambaye ni Mkristo amefariki.  Nikagaiwa baadhi ya nguo zake. Kisheria mimi siruhusiwi kuzivaa. Je? Naweza kuzigawa kwa watu kama mke mwenzangu, au watoto wake, ambao hawana uhusiano naye wa damu? Naelewa sipati thawabu. Lakini ni watu gani wengine ambao naweza kuwagawia nguo hizo? Je, na wanangu (Waislam) pia hawatakiwi kuzivaa nguo hizo?

Shukran Jazilla.

Asalaam Alaykum Warahmatullah Wabarakatuh.

 

 


 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Aliyetukuka Mola  wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allahu 'anhum jamiy'an) na watangu wema mpaka Siku ya Qiyaamah.

Shukran kwa swali hili muhimu, na hakika ni kuwa Muislamu hamrithi asiyekuwa Muislamu wala kinyume chake.

Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) anasema katika hadiyth iliyopokelewa na Usaamah bin Zayd: ((Muislam hamrithi kafiri na kafiri hamrithi Muislam)) Al-Bukhaariy na Muslim.

Lakini ikiwa atapatiwa bila ya yeye kuomba au kutaka kama urithi yeye anafaa kuchukua kwa msingi wa Akhaffudh Dhararayn (Dhara dogo kati ya madhara mawili). Huu ni kama ule msingi wa kuchukua pesa za riba (na kuzitoa kwenye maendeleo ya jamii bila kutegemea kupata ujira juu ya hilo) uliotolewa na wanazuoni kwani kuiacha italeta madhara makubwa sana kwa Uislamu na Waislamu. Hivyo, msingi huu ni kama wa kuchukua huo urithi lakini haifai katika hali zote hizo mbili kutumia kwa faida yako au ya jamaa zako wanaokutegemea wala usitarajie thawabu kutoka kwa Allah (Subhaanahu wa Ta'ala).

Kwa muhtasari ni kuwa waweza kuzichukua ikiwa umepewa bila kuomba na kuzitoa kwenye mashirika ya misaada ya Kiislam (Charity Organizations) au kwa wenye kuhitaji miongoni mwa maskini na mafakiri na wasiojiweza, lakini wasiwe jamaa wa karibu ambao jukumu lako kuwaangalia katika masrufu yao ya kila siku.

Na Allaah Anajua zaidi.

 

Share