037-Lu-ulu-un-Manthuwrun: Mwenye Iymaan Kweli Amkirimu Mgeni, Na Aseme Ya Kheri Au Anyamaze

 

Lu-ulu-un-Manthuwrun

 

(Mkusanyiko Wa Hadiyth Mbali Mbali Na Mafunzo Yake)

 

Hadiyth Ya 37

 

Mwenye Iymaan Kweli Amkirimu Mgeni, Na Aseme Ya Kheri Au Anyamaze

 

Alhidaaya.com

 

 

 

عَنْ أَبِي شُرَيْحٍ الْخُزَاعِيِّ (رضي الله عنه) أَنَّ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ: ((مَنْ كَانَ يُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الأَخِرِ فَلْيُحْسِنْ إِلَى جَارِهِ،  وَمَنْ كَانَ يُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الأَخِرِ فَلْيُكْرِمْ ضَيْفَهُ،  وَمَنْ كَانَ يُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الأَخِرِ فَلْيَقُلْ خَيْرًا أَوْ لِيَسْكُتْ)) مسلم وروي البخاري بعضه

Imepokelewa kutoka kwa Abu Shurayh Al-Khuzaa’iyy( (رضي الله عنه)  kwamba Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم)  amesema: ((Anayemwamini Allaah na Siku ya Mwisho, basi amfanyie wema jirani yake, na anayemwamini Allaah na Siku ya Mwisho,  basi amkirimu mgeni wake, na anayemwamini Allaah na Siku ya Mwisho, basi azungumze kheri au anyamaze)) [Muslim na amepokea Al-Bukhaariy baadhi yake]

 

 

Mafunzo Na Mwongozo:

 

 

1. Kumkirimu mgeni na kutokusema maovu ni mojawapo wa uthibitisho wa kumwamini Allaah (سبحانه وتعالى)  na Siku ya Mwisho. Rejea Hadiyth namba (36).

 

 

2. Ukarimu ni miongoni mwa tabia njema za Muumin na sababu ya kuingia Jannah.

 

3. Umuhimu wa kuchunga na kuzuia ulimi usiseme maneno ya upuuzi, kwani kila linalotamkwa linaandikwa na litaulizwa. Anasema Allaah (سبحانه وتعالى):

 

 إِذْ يَتَلَقَّى الْمُتَلَقِّيَانِ عَنِ الْيَمِينِ وَعَنِ الشِّمَالِ قَعِيدٌ﴿١٧﴾

Pale wanapopokea wapokeaji wawili (Malaika) wanaokaa kuliani na kushotoni. 

 

 

مَّا يَلْفِظُ مِن قَوْلٍ إِلَّا لَدَيْهِ رَقِيبٌ عَتِيدٌ﴿١٨﴾

Hatamki kauli yeyote isipokuwa anaye mchungaji aliyejitayarisha (kurekodi). [Qaaf: 17-18]

 

Hadiyth: ((Kwa hakika mja atazungumza neno ambalo halizingatii [kuwa ni la kheri au la shari] ateleze nalo motoni umbali zaidi ya umbali ulioko baina ya Mashariki na Magharibi)). [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Rejea Hadiyth namba (86), (87), (93), (94),

 

4. Ulimi unaonena maovu unasababisha kila aina ya shari, kwa mgeni, jirani na jamii nzima kwa ujumla. Na Allaah (سبحانه وتعالى)  Anaamrisha kusema na watu yaliyo mema:

 

  وَقُولُوا لِلنَّاسِ حُسْنًا

Na semeni na watu kwa uzuri  [Al-Baqarah: (2: 83)]

 

 

5. Inapendekeza kukaa kimya panapokuwa hakuna faida ya kusema jambo na hiyo ni sifa mojawapo miongoni mwa sifa zitakazompatia Muislamu Jannah ya Al-Firdaws kwani hivyo ni kujiepusha na porojo na upuuzi. [Al-Muuminuwn: (23: 3]

 

Rejea pia Al-Furqaan (25: 72)

 

Share