08-Umuhimu Na Fadhila Za Tawhiyd: Tawhiyd Ni Lengo Kuu La Kuumbwa Wana Aadam Na Majini

 

Umuhimu Na Fadhila Za Tawhiyd

 

08-Tawhiyd Ni Lengo Kuu La Kuumbwa Wana Aadam na Majini

 

 

 

 

Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ﴿٥٦﴾

Na Sikuumba majini na wana Aadam isipokuwa waniabudu. [Adh-Dhaariyaat: 56]

 

Anatujulisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwamba Ametuumba kwa hikmah nayo ni kumpwekesha katika ‘ibaadah wala hakutuumba kwa kuwa Ana haja nasi kwani yeye ni Al-Ghaniyy (Mkwasi Asiyehitaji kitu) kama Anavyosema:

 

يَا أَيُّهَا النَّاسُ أَنتُمُ الْفُقَرَاءُ إِلَى اللَّـهِ ۖ وَاللَّـهُ هُوَ الْغَنِيُّ الْحَمِيدُ﴿١٥﴾

Enyi watu!  Nyinyi ni mafakiri kwa Allaah! Na Allaah Ndiye Mkwasi,  Mwenye kustahiki kuhimidiwa kwa yote. [Faatwir: 15]

 

Akathibitisha hayo Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anapoendelea kusema baada ya Aayah iliyotangulia ya Suwrah Adh-Dhaariyaat:

 

مَا أُرِيدُ مِنْهُم مِّن رِّزْقٍ وَمَا أُرِيدُ أَن يُطْعِمُونِ﴿٥٧﴾

Sitaki kutoka kwao riziki yoyote, na wala Sitaki wanilishe. [Adh-Dhaariyaat: 57]

 

Akatujulisha kwamba Hahitaji lolote kutoka kwa waja Wake, bali waja ndio wanaomhitaji Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwani Yeye Ndiye Anayewaruzuku na Anawaendeshea maisha yao na Ndiye Anayewapangia na kuwatengeneza mambo yao. Yeye ni Allaah, Anayestahiki kuabudiwa kwa haki Naye Ndiye Muumba wa kila kitu:

 

ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ ۖ لَا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ ۖ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ فَاعْبُدُوهُ ۚ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ وَكِيلٌ ﴿١٠٢﴾

Huyo kwenu Ndiye Allaah, Rabb wenu. Hapana muabudiwa wa haki ila Yeye Muumbaji wa kila kitu, basi mwabuduni Yeye Pekee. Naye juu ya kila kitu ni Mdhamini Anayetegemewa kwa yote.  [Al-An’aam: 102]

 

Na Anasema pia:

 

ذَٰلِكُمُ اللَّـهُ رَبُّكُمْ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ لَّا إِلَـٰهَ إِلَّا هُوَ ۖ فَأَنَّىٰ تُؤْفَكُونَ﴿٦٢﴾

  Huyo Ndiye Allaah Rabb wenu, Muumba wa kila kitu, hakuna Muabudiwa wa haki ila Yeye; basi vipi mnaghilibiwa?   [Ghaafir: 62]

 

Viumbe hao, wanajumuika Malaika, majini na wana Aadam. Wote hao wanastahiki kumwambudu kwa kuwa ni haki ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kutoka kwao na lau kama watamshirikisha, basi Atawaadhibu hata ikiwa Malaika watamshirikisha, kama Anavyosema:

 

وَمَن يَقُلْ مِنْهُمْ إِنِّي إِلَـٰهٌ مِّن دُونِهِ فَذَٰلِكَ نَجْزِيهِ جَهَنَّمَ ۚ كَذَٰلِكَ نَجْزِي الظَّالِمِينَ ﴿٢٩﴾

Na yeyote yule miongoni mwao atakayesema: “Mimi ni mwabudiwa badala Yake,” basi huyo Tutamlipa Jahannam. Hivyo ndivyo Tunavyolipa madhalimu.   [Al-Anbiyaa: 29]

 

Na atakayemshirikisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) hatoweza kufidia kuepuka na adhabu ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) hata akiwa na dhahabu inayojaa ardhini! Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 

  إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا وَمَاتُوا وَهُمْ كُفَّارٌ فَلَن يُقْبَلَ مِنْ أَحَدِهِم مِّلْءُ الْأَرْضِ ذَهَبًا وَلَوِ افْتَدَىٰ بِهِ ۗ أُولَـٰئِكَ لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ وَمَا لَهُم مِّن نَّاصِرِينَ ﴿٩١﴾

Hakika wale waliokufuru na wakafa nao wakiwa makafiri, basi haitakubaliwa kutoka kwa mmoja wao dhahabu ya ujazo wa dunia nzima lau wakitaka kujifidia nayo. Hao watapata adhabu iumizayo na hawatopata mwenye kuwanusuru. [Aal-‘Imraan: 91]

 

Share