Swahiyh Fiqh As-Sunnah
كِتَابُ الزَّوَاجِ
Kitabu Cha Ndoa
النُّشُوْزُ وَعِلَاجُهُ
Uasi Wa Mke Kwa Mume Na Njia Za Kuutibu
02: Hatua Za Kutibu Uasi Wa Mke: (a) Hatua Ya Kwanza: Atamnasihi
Mwanamke akionyesha alama za uasi kama kununa akiamuriwa jambo, kupinga agizo, kukunja uso, kuzungumza kwa maneno makali, kujivuta vuta akitakwa tendo la ndoa na kadhalika, au akaonyesha wazi uasi kama kumkatalia mumewe tendo la ndoa, kutoka bila idhini, kukataa kusafiri pamoja naye na mfano wa hayo, basi hapo mume ameruhusiwa kutibu tatizo hilo kwa njia zilizotajwa hatua kwa hatua ndani ya Qur-aan Tukufu. Hatua hizo ni kama ifuatavyo:
1- Atamnasihi:
Mume atamnasihi mkewe kwa ulaini na utulivu. Atamkumbusha utiifu Aliomwajibishia Allaah kwa mumewe, atamtia utashi wa kupata thawabu za Allaah Ta'aalaa kutokana na utiifu huo, na kwamba akiwajibika ipasavyo atakuwa katika kundi la wanawake wema, wanyenyekevu na wenye kujilinda. Kadhalika, atamhofisha kupatwa na Adhabu ya Allaah, na kwamba kama ataendelea na uasi, basi yeye ana haki ya kumsusa, kisha kumpiga.
Baadhi ya wanawake huwa wasikivu wakajirekebisha; wakaacha ukaidi, wakajibishana vyema na nasaha, vishajiisho na vitisho. Hawa haifai tena kwa mume kuwasusa wala kuwapiga. Allaah Ta'aalaa Anasema:
"فَإِنْ أَطَعْنَكُمْ فَلَا تَبْغُوا عَلَيْهِنَّ سَبِيلًا ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلِيًّا كَبِيرًا"
"Wakikutiini, basi msitafute njia dhidi yao (ya kuwaudhi). Hakika Allaah daima Ni Mwenye Uluwa, Mkubwa wa Dhati, Vitendo na Sifa". [An-Nisaa: 34]
Lakini pia kuna wanawake ambao hawaathiriwi na chochote; si nasaha wala mawaidha. Kwa mwanamke kama huyu, mume atahamia katika hatua ya pili ya kumweka sawa ambayo ni kumsusa kitanda.