Kukata Kucha Akiwa Katika Hedhi Au Nifaas Inafaa?

Kukata Kucha Akiwa Katika Hedhi Au Nifaas Inafaa?

 

www.alhidaaya.com

 

 

 

SWALI:

 

Swali langu linahusu ukataji kucha. Je ninaweza kukata kucha nikiwa sina udhu?  Labda nikiwa ktk hedhi au nifasi?

 

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Tufahamu kuwa kukata kucha ni miongoni mwa maumbile ya mwana Aadam na hasa akiwa Muislamu mwenye kufuata Sunnah za Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Mama wa Waumini ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) ametufahamisha kuwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Mambo kumi ni katika fitwrah (maumbile ya asli ya Kiislam): “Kupunguza masharubu, kufuga ndevu, kupiga mswaki, kupitisha maji puani (kusafisha), kukata kucha, kusafisha penyo za vidole, kung’ofoa (kunyoa) nywele za kwapa, kunyoa nywele za sehemu za siri, na kujisafisha kwa maji baada ya kujisaidia na msimuliaji akasema kasahau la kumi, lakini inaweza kuwa ni kusafisha mdomo (kusukutua)” [Muslim na Abuu Daawuwd].

 

Na katika masimulizi mengine kumesemwa mambo matano, nayo ni kama yaliyomo katika hayo kumi. Na Hadiyth hiyo inasema: “Mambo matano ni katika sifa za fitwrah (Maumbile ya asli ya Kiislam au ya Tawhiyd); Kutahiriwa, kunyoa nywele za sehemu za siri, kukata masharubu, kukata kucha ziwe ndogo, na kunyofoa (kunyoa) nywele za kwapani” [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Kukata kucha ni katika mambo ya kujiwekea usafi wa mwili nalo linaweza kufanyika wakati wowote ule, ukiwa katika hedhi, nifasi na pia ikiwa huna wudhuu. 

 

Na ni bora zaidi kukata kucha kila Ijumaa zikiwa zimekua, na inatakikana Muislam asiziache kucha zake au nywele zake za sehemu za siri au makwapani kukaa zaidi ya siku arubaini bila kukatwa au kunyolewa.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share