Fadhila Za Kusuluhisha Waliokhasimiana -1

 

Fadhila Za Kusuluhisha Waliokhasimiana

 

Alhidaaya.com

 

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)

 

 لَّا خَيْرَ فِي كَثِيرٍ مِّن نَّجْوَاهُمْ إِلَّا مَنْ أَمَرَ بِصَدَقَةٍ أَوْ مَعْرُوفٍ أَوْ إِصْلَاحٍ بَيْنَ النَّاسِ ۚ وَمَن يَفْعَلْ ذَٰلِكَ ابْتِغَاءَ مَرْضَاتِ اللَّـهِ فَسَوْفَ نُؤْتِيهِ أَجْرًا عَظِيمًا ﴿١١٤﴾

Hakuna khayr katika minong’ono yao mingi isipokuwa anayeamrisha swadaqah, au mema, au kusuluhisha baina ya watu. Na atakayefanya hivyo kutaka radhi za Allaah, basi Tutampa ujira adhimu. [An-Nisaa: 114]

 

Na kasema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa Sallam): 

((ألا أخبركم بأفضل من درجة الصيام والصلاة والصدقة ؟ إصلاح ذات البين وفساد ذات البين هي الحالقة))  رواه أحمد وأبو داود والترمذي صحيح الجامع

"Je, nikujulisheni lililo na daraja bora kuliko Swawm na Swalah na Sadaqah? Ni kusuluhisha baina ya watu. Na ama kuharibu uhusiano (baina ya watu) ni uharibifu" [Ahmad na Abu Daawuud na At-Tirmidhy katika Swahiyhul-Jaami'i]

 

Katika mambo ya kheri Aliyoyataja Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) watu wanapozungumza kwa siri ni kuamrishana kutoa sadaka au kutenda mema. Kisha Ametaja kuhusu kupatanisha watu, jambo ambalo mara kwa mara hutokea katika jamii na khaswa jamii yetu. Na bila ya shaka ugomvi na ikhtilaaf ni katika silaha ya hatari kabisa anayopenda kuitumia Shaytwaan kufarikisha watu watengane na kuchukiana baada ya kuwa ni ndugu au marafiki au majirani au baina ya mume na mke. Lakini Uislamu haukuacha kutilia hima jambo la kusuluhisha ugomvi kwa kutukumbusha fadhila zake kubwa katika Qur-aan na Sunnah kama tunavyoona katika Aayah na Hadiyth hapo juu.

 

Lakini inasikitisha kuona kwamba jambo hili la kusuluhisha halikutiliwa mkazo sana katika jamii yetu, kwani wangapi tunasikia miongoni mwetu kuwa 'fulani kagombana na fulani na hawasemeshani', kisha zikapita siku na miezi na miaka hawa watu wako katika hali hii jambo ambalo Nabiy Swalla Allaahu  amekataza kabisa zisipite zaidi ya siku tatu ndugu wa Kiislamu kuwa katika hali kama hiyo:   

 عن أبي أيوب الأنصاري رضي الله عنه قال : قال النبي صلى الله عليه وسلم : (( لا يَحِلُّ لِمُسْلِمٍ أَنْ يَهْجُرَ أَخَاهُ فَوْقَ ثَلَاثِ لَيَالٍ ، يَلْتَقِيَانِ فَيُعْرِضُ هَذَا وَيُعْرِضُ هَذَا ، وَخَيْرُهُمَا الَّذِي يَبْدَأُ بِالسَّلامِ  .(( رواه البخاري ومسلم و في رواية أبو داود بإسناد على شرط البخاري ومسلم

((فَمَنْ هَجَرَ فَوْقَ ثَلاَثٍ فَمَاتَ دَخَلَ النَارَ ))   

Imetoka kwa Abu Ayyuub Al-Answariy (Radhwiya 'anhu) ambaye alisema: Kasema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): "Haimpasi Muislamu amhame ndugu yake kwa zaidi ya siku tatu hata wanapokutana huyu anamgeuzia (uso) huyu na huyu anamgeuzia (uso) huyu. Na aliye mbora wao ni yule anayeanza kutoa salaam". [Al-Bukhariy na Muslim  na katika Riwayaah ya Abu Daawuud]

((Atakayemhama (mwenzake) kwa zaidi ya siku tatu akafariki basi ataingia  motoni))

 

Na huenda ikawa kila mmoja anataka kupatana na mwenziwe lakini Shaytwaan amewatia ari kuwa vipi aanze yeye? Na pia pengine huenda wakawa ni ndugu, au jamaa au jirani lakini hakuna mmoja wetu anayekimbilia kusuluhisha, sababu ni kwamba kila mmoja ameshughulika na kazi zake na maisha yake. Kwa hiyo tulichukulie hima jambo hili bila ya kuchelewesha kila inapotokea ugomvi baina ya ndugu wa Kiislamu na kufanya hivyo ni kumcha Allaah na kumtii Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na ndio sifa ya Waumini kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

فَاتَّقُواْ اللّهَ وَأَصْلِحُواْ ذَاتَ بِيْنِكُمْ وَأَطِيعُواْ اللّهَ وَرَسُولَهُ إِن كُنتُم مُّؤْمِنِينَ﴿١﴾

Basi mcheni Allaah na tengenezeni yaliyo baina yenu. Na mtiini Allaah na Rasuli Wake mkiwa ni Waumini.. [Al-Anfaal: 1]

 

Itaendelea sehemu ya pili In Shaa Allaah...

 

 

************

 

 

 

Share