Mkimbizi Anapokea Pato La Serikali Kwa Kudanganya Je Anaweza Kutoa Humo Zakaah Dhahabu Zake Au Sadaqah?

 

SWALI:

 

Assalaam alaykum Warahmatullah Wabarakatuh,ama baada ya maamkizi hayo mema ya kiislam sina budi kmshukuru ALLAH AZZA WA JALLA kwa kuniwezesha kuvuta pumzi leo hii na kukaa hapa ili kuwasilisha swali langu. Pili shukran alhidaaaya kwa mengi mema mnayotupa na ujira wenu INshaallah mtaukuta Akhera.

Swali langu ni kuwa mimi ni mkimbizi naishi ulaya na ninapokea mapato yangu ukimbizini na kama unavyojuwa kuwa tumedanganya kwanza na sina sina kazi, hivyo ninapata malipo kupitia hapo, na nina dhahabu ambazo ni kiwango cha kutolewa zaka na ninataka kutowa zaka, Je itawezekana kutowa kupitia fedha hizo-

Pili, pia kupitia fedha hizo nataka nipeleke kwetu na niwape watu wengine kama swadaka je inawezekana, sheikh naomba majibu yako kupitia mail yangu


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Ndugu yetu katika Uislamu ilikuwa vyema useme hivi: Mimi nimedanganya na ninapata posho kwa huko kudanganya kwangu nini hukumu ya hilo posho?

Hukumu yake ni kuwa si halali yako.

Ndugu yetu katika Uislamu, pia ilikuwa vyema useme hivi: ‘Nina dhahabu ambazo zimefikia kiwango cha kutolewa Zakaah na ninataka kutoa Zakaah. Je, inafaa niitolee hiyo dhahabu iliyofikia kiwango, Zakaah?

 

Hukumu yake kama dhahabu imefikia kiwango unatakiwa utoe Zakaah na kama tulivyoeleza kuwa fedha unazozipata kwa kudanganya si halali yako hivyo toa hizo dhahabu kama ni Zakaah yako.

Ndugu yetuu katika Uislamu, pia ilikuwa vyema useme hivi: ‘wakimbizi na wakaazi wa hapa nilipo hupewa posho kuendesha maisha yao ya kila siku na mimi kiuhakika sina haja ya hilo posho kwani nina uwezo mkubwa hata nikawa na dhahabu; hivyo basi hilo posho analostahiki kila mkaazi asiye na kazi, kwa kuwa silihitaji hili posho nataka nipeleke kwetu na niwape watu wengine kama swadaka.’

 

Wenye kupewa hilo posho hupewa kwa kuwa ni katika mipango ya hapo ulipo kuwa kila mkaazi wao asiyejiweza au asiye na kazi asaidiwe. Ama wewe unajiweza na unaweza kufanya kazi hivyo basi si halali kwako hilo posho wala si halali kuwapa wengine kisichokuwa halali kwako na ukategemea malipo kwa Mola.

Bonyeza viungo vifuatavyo upate maelezo zaidi:

 

Kutoa Sadaka Na Pesa Za Kusaidiwa Na Serikali Na Zile Za Chumo La Haraam

Pesa Alizozichuma Kusema Uongo Azifanye Nini?

Pesa Anazopata Kwa Kuongopa Serikalini Zinafaa Kutumika Kwa Matumizi yake na kufanyia Mambo Ya Kheri?

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share