Kukosa Radhi Za Mzazi Kwa Kuolewa Na Asiyetakiwa Na Mzazi Bila Sababu Za Kisheria

 

 

SWALI:

Assalam aleykum wa rahmatullah wa barakatuh.Hili ni suala kuhusu dua ya mzazi kwa mwanawe. Mzazi anamwambia mwanawe, ukiolewa au ukikubali kuolewa na mtu flani basi huna radhi zangu. Inafikilia hadi mtoto yuko kati aidha achague wazazi au yule atakae kumuoa. Wazazi waliulizia kuhusu yule kijana; dini yake na tabia yake ikawa hamna jawabu lolote baya. Sababu ya kumkataa yule kijana hamna na mtoto wa kike yuataka kuolewa na yule kijana.

1. Sasa jee hii dua ya mzazi mbele ya Allaah inakubaliwa?

2. Jee yule mtoto wa kike afanyeje?

Tafadhali naomba jawabu na dalili kutokana na mafundisho yetu ya Kiislamu wa billahi taufiq

 

 


JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani kwa swali lako hilo zuri. Hakika ni kuwa hili ni tatizo kubwa wakati huu wetu katika jamii yetu. Kwa kuwa tumelifanya jambo rahisi na sahali kuwa gumu ndio tukaingia katika mtego pamoja na matatizo yake mengi. Hadi sasa imekuwa rahisi kumuoa Mkristo kuliko Muislamu na ilhali ilikuwa iwe ni kinyume cha hivyo.

Haya matatizo ambayo tunayapata kutoka kwa wazazi, wasichana, vijana ni kwa sababu tumekataa mwito wa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliotueleza: “Akikujieni ambaye munairidhia Dini na maadili yake, muozeni. Ikiwa hamtafanya hivyo kutakuwa na Fitna na uharibifu mkubwa” (at-Tirmidhiy).

Wazazi wanatakiwa kumlinda na kumhifadhi binti yao kupata mume mwema mcha Mngu sio kumlazimisha kuolewa au kutoolewa na mume fulani. Wazazi hawana uwezo huo kwa mujibu wa Hadiyth ya msichana aliyekuwa amechaguliwa mume na babake kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimwambia kuwa ikiwa hamtaki basi hakuna ndoa. Msichana akasema nimeridhia na uchaguzi wa babangu lakini nilikuwa nataka kuwafahamisha wanawake kuhusu haki zao (Al-Bukhaariy).

Ikiwa wazazi hawana lolote dhidi ya kijana anayetaka kumuoa binti yao ili kutoleta ubishano na mvurugano inabidi atumie njia za kuwafanya kuridhika katika uchaguzi wake. Inafaa amtumie mamake kwani mioyo ya kina mama inakuwa hafifu na kuweza kukubali au pia jamaa zake wengine ambao wako karibu nao. Haswa kwa kuwa mvulana ni mtu wa Dini na maadili mema.

Ikiwa wamekataa kata kata, itabidi msichana apeleke mashitaka yake kwa Qaadhi ikiwa yupo na ikiwa hakuna Qaadhi sehemu hiyo basi kwa Shaykh mjuzi wa sharia. Qaadhi atamuita baba ajieleze kwa nini anakataa bintiye asiolewe na mvulana huyo. Ikiwa hawana chochote cha kujitetea kwa kuwa kijana ni mzuri itabidi Qadhi amuombe akubali ndoa hiyo ifungwe. Lau hata baada ya hapo atakataa, Qaadhi atakuwa walii wa msichana na atamuozesha. Ndoa hiyo ni halali katika sharia, na vitisho vya wazazi kuwa watamlaani msichana haina uzito wowote katika sharia. Laana hiyo haimfikii mlengwa kabisa.

Ama kuhusu msichana afanyeje, ni vigumu sisi kusema chochote kwa kuwa hatujui hali halisi huko aliko. Yeye ndio muamuzi bora kwani anaishi katika mazingira hayo. Hapa ipo kanuni ya Ki-Fiqhi ambayo inasema: “Dhara lililo dogo (katika mambo mawili)”. Hiyo ina maana atazame kukubali kwake kuolewa ambayo ni haki yake atapata madhara gani na faida ipi na kuwatii wazazi kwa wanalolitaka kutakuwa na maslahi gani kwake au madhara gani? Katika hilo inafaa atazame mas-ala hayo kwa kina na sio juu juu tu.

Ushauri wetu mwingine ni kuwa aswali Swalah ya Istikhara kutaka ushauri kutoka kwa Allaah Aliyetukuka kwa jambo hilo. Lile ambalo litajitokeza baada ya Swalah hiyo ndilo litakalo kuwa ni kheri kwake hivyo alitimize bila kusita.

Soma hapa kuhusu Swalah ya Istikhaarah:

Kwa Nini Tuswali Istikhaarah Na Iswaliwe Kwa Ajili Ya Nini?

 

Muda Wa Swalah ya Istikhaarah

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share