Mke Wangu Amevaliwa Na Majini Wa Mahaba? Hapendi Kutenda Kitendo Cha Ndoa Na Mimi

 

 SWALI:

 

Asalaam alakum warahmatllahi wabarakatu

Baada ya salam napenda kuwashukuru kwa mengi mnayo tufundisha kwa kweli mengi tulikuwa hatuyajuwi lakini baada yakujiunga na ukumbi huu wa alhidaaya tumejuwa mengi. Natoa shukurani kwa namna mnavyo tuelimisha tumefaidika mengi kutoka kwenu Mwenyezi Mungu awazidishie kila la kheri amin.

a)Suali langu mimi kwa kweli mke wangu hapendi kusikia nikimwambia neno kuhusu kufanya jimai kila nikimwambia ananiambia eti amechoka pengine huniweka katika hali hiyo muda wa siku tatu nakua hata usingizi sipati sasa mimi nataka nijuwe nini hukumu yake kwa maana mimi siko radhi kwa kitendo hiki anachonifanya baada ya kujifungua mtoto wa kwanza ndio alipoanza tabia hii leo zaidi ya miaka minane kwa kweli nimevumulia sasa mimi ninachowaomba mumpe mawaidha kuhusu kitendo hiko anachonifanyia.

b) swali, nasikia watu wakisema fulani ana jini wa mahaba akiwa mwanamke au mwanaume na wengi kama hawa huwa mara nyingi ndoa zao huvunjika akiwa mwanamke unamkuta daima hana raha na mme wake hamjali pia upande wa mwanaumme nae unamkuta hamjali mke wake sasa nataka mnifahamishe ni kweli mambo haya yapo? Ikiwa ni kweli watu hawa watahukumiwa vipi? Nashukuru nasubiri jibu kutoka kwenu.

 


JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Aliyetukuka Mola  wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allahu 'anhum jamiy'an) na watangu wema mpaka Siku ya Qiyaamah.

 

Kwanza tunashukuru kuona kwamba mnafaidika na mengi kutoka Alhidaaya.com na tunapenda kutoa shukurani kwa du'aa zenu nzuri mnazotuombea nyote mnaotuma maswali yenu pamoja na wengineo wanaoingia Alhidaaya.com  kutafuta faida mbali mbali. Tunamuomba Allaah (Subhaana wa Ta'aala)   Atutakabalie hizo du'aa na Atuzidishie uwezo wa kuelimishana kwa kadiri Anavyotujaalia. Aamiyn

 

Shukrani kwa swali lako hilo muhimu kuhusu mas-ala kama hayo ambayo yanaweza kumuweka mwanamume mahali pabaya kwani inaweza kumpelekea kuzini ili kutimiza uchu wake. Jambo hili kwa hakika lina vipengele vingi kama vifuatavyo:

 

  1. Huenda mke hakutaki tena lakini hataki kukuambia.
  2. Huenda baada ya uzazi akawa yale matamanio hayapo tena.
  3. Huenda akawa amekumbwa na jini ambalo linastarehe naye hivyo kutoweza kufanya jimai na wewe, kwani jini lina nguvu zaidi kuliko mwanadamu. Ingawa hili lina mvutano baina ya wanachuoni kuhusu kuwezekana au kutokuwezekana.

 

Ingia katika kiungo kifuatacho hapa chini usome makala kuhusiana na uhusiano wa majini na wanaadamu:

 

Bonyeza hapa:

 

Mfululizo Wa Mada Ya Majini (4)

 

Kuhusu nukta ya kwanza: Ili kuweza kurekebisha jambo hilo inafaa muzungumze kama mke na mume na uwazi na murekebishe pale panapokuwa na tatizo. Ikiwa hutaweza kukaa na kuzungumza mas-ala hayo basi utakaa na huku unaudhika na tatizo litabaki palepale.

 

Kuhusu nukta ya pili: Hili ni tatizo ambalo huenda likapatikana kwa mwanamme au mwanamke. Mara nyingine mume anakuwa hana matamanio kwa mwanamke na mara nyingine huwa ni mwanamke mwenye tatizo hilo. Kwa hali hii inatakiwa mke apelekwe hospitali kwani ni tatizo lenye tiba.

 

Kuhusu Nukta ya Tatu: Hili ni tatizo ambalo ambalo mwanaume au mwanamke anaweza kukumbwa. Akiwa mwanaume anaweza kukumbwa na jini la kike ambalo linamuhangaisha na hivyo kushindwa kumtimizia mkewe kitendo cha ndoa. Na akiwa mwanamke anaweza kukumbwa na jini la kiume ambalo linalala naye na kumuhangaisha kimapenzi hivyo kutoweza kukutana na mwanaume kwani nguvu za jini ni kubwa. Baada ya jimai na mwanamke huwa mchofu hivyo kutoweza kufanya tendo la ndoa na mumewe.

 

Tatizo hilo lina tiba na tiba yake si kwenda na wachawi kama wanavyofanya wengi miongoni mwetu. Bali tiba yake mwanzo ni wewe kujitibu mwenyewe kwa 'RUQYA'; kusoma kisomo cha Qur-aan na du'aa na nyiradi zilizopo katika Hadiyth za Mtume (Swalla Llaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ambazo zinampatia kinga mwenye kusoma. Nazo zinapatikana katika kitabu cha Hiswnul-Muslim ambacho kinauzwa kwa bei khafifu kabisa na vile vile kipo tayari ALHIDAAYA katika kiungo kifuatacho:

 

Bonyeza hapa:

 

 

Hiswnul-Muslim: Du’aa Na Adhkaar Kusoma Na Kwa Kusikiliza (Toleo Lilohaririwa)

 

 

027-Hiswnul-Muslim: Nyiradi Za Asubuhi Na Jioni

 

Du'aa na Nyiradi hizo inatakiwa mtu asome asubuhi na jioni ili kujitibu kukumbwa na majini na pia kupata hifadhi na kinga kutoka kwa Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) mtu asikumbwe na majini, au asifikiwe na uchawi au uovu wowote.   

Katika Qur-aan ni Aayah kadhaa za Suratul Baqarah (1–5, 255–257 na 284–286), Suratul Ikhlaas  na Mu‘awwidhatayn. Na ikiwa mtu amekumbwa na jini basi anaweza kuchukuliwa kwa Shaykh ambaye anajua kisomo cha 'RUQYA' ya Shari'ah. Bonyeza viungo vifuatavyo kwa manufaa zaidi:

 

Tiba Gani Zimo Katika Qur-aan?

 

Hirizi Inafaa Kuvaliwa Kutibu Maradhi Ya Nafsi Na Jini?

 

Baina Ya Jinni Na Mchawi: Kiungo Kilichojificha

 

Shaytwaan Na Mwana Aadam

 

Pia ni muhimu kwa kumkinga mtoto kabla ya kuzaliwa kwa wanandoa kusoma dua wakati wanapofanya jimai nayo ni kusema: “Bismillahi Allahumma Jannibnash Shaytwaana wa Jannibish Shaytwaana Maa Razaqtanaa” (al-Bukhaariy). Anasema Mtume (Swalla Llaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akizaliwa mtoto hatasogelewa na Shaytani.

 

Jibu La Pili Kuhusu Kuwa Na Majini Wa Mahaba:

 

Kama tulivyojibu huko nyuma ni kuwa mwanamke au mwanamme anaweza kukumbwa na jini wa kiume au wa kike ambaye atakuwa anafanya naye mapenzi. Amali zote zinategemea na nia na kwa sababu nia yako haikuwa kufanya mapenzi na mwengine yeyote asiyekuwa mume au mke wako wewe hutakuwa na makosa lakini unahitajika kufanya juhudi ili kuweza kumtoa na kurudi katika maumbile yako ya kawaida.

 

Na Allah Anajua zaidi

 

 

 

 

Share