Sunnah Gani Za Kabla Na Baada ya Swalah Ya Ijumaa Zinapasa Kuswaliwa?

SWALI:

Nawashukuru mashehe wetu kutujibia masuali kwani hatuna pengine pa kuuliza hasa huku nchi za nje ni shida kupata mtu wa kuuliza masuali hivo tunafanya mambo bila kujua ipasavo. Mungu awalipe mema mingi mzidi kutuhudumia na kutuelemisha.

Nauliza kuhusu suna za ijumaa napokwenda kusali msikitini je, nisali kwanza tahiya ya masjid, kisha nisali tena zile suna za kablia 4 na baada ya sala nisali zile 2 za baadia? Maana nimesikia hakuna haja kusali suna siku ya ijumaa.

Na je ikiwa nasali nyumbani hiyo sala ya ijuma inakuwaje hizo suna nisali vipi? Asanteni sana.

 


 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa ndugu yetu muulizaji swali. Awali ya yote ni kuwa si kweli kuwa hakuna Swalah za Sunnah kabla ya Swalah ya Ijumaa. Kisha ni kuwa pindi anapoingia Msikitini siku ya Ijumaa anafaa mtu aswali Sunnatut Tahiyyat Al-Masjid (Sunnah ya kuusalimu Msikiti). Sunnah hii ni muhimu na inafaa itekelezwe hata kama Imaam tayari amepanda juu ya Minbar na anahutubu inafaa uiswali kwa kuifanya wepesi na si kurefusha. [Muslim na Ahmad].

 

Mbali na hiyo Sunnah, kutokana na Hadiyth ifuatayo hapa chini, imepokelewa kuwa Wanachuoni kuwa wanaonelea kuwa mtu anaweza kuswali Swalaah kwa idadi yoyote bila kujifunga na kiwango maalum kwani hakuna Sunnah ya kabla ya Ijumaa iliyothibiti. Kwa hivyo, Muislamu akifika mapema anaweza akipenda kuswali idadi yoyote anayoweza yeye bila kujikalifisha.

يستحب لمن أتى الجمعة أن يتطوع بالصلاة قبلها، بما تيسر له، من حين دخوله إلى المسجد، إلى أن يخرج الإمام على الناس، من غير أن يكون ذلك مقيدا بعدد مخصوص، فيصلي ركعتين، أو أربعا، أو ما شاء الله له أن يصلي .
روى البخاري (883) ومسلم (857) عَنْ سَلْمَانَ الْفَارِسِيِّ قَالَ: قَالَ النَّبِيُّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ: (لَا يَغْتَسِلُ رَجُلٌ يَوْمَ الْجُمُعَةِ وَيَتَطَهَّرُ مَا اسْتَطَاعَ مِنْ طُهْرٍ وَيَدَّهِنُ مِنْ دُهْنِهِ أَوْ يَمَسُّ مِنْ طِيبِ بَيْتِهِ ثُمَّ يَخْرُجُ فَلَا يُفَرِّقُ بَيْنَ اثْنَيْنِ ثُمَّ يُصَلِّي مَا كُتِبَ لَهُ، ثُمَّ يُنْصِتُ إِذَا تَكَلَّمَ الْإِمَامُ إِلَّا غُفِرَ لَهُ مَا بَيْنَهُ وَبَيْنَ الْجُمُعَةِ الْأُخْرَى) .

 

فقد جاء في فضل التنفل قبل صلاة الجمعة، ما رواه البخاري (910) عن سلمان الفارسي رضي الله عنه قال : قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: (مَنْ اغْتَسَلَ يَوْمَ الْجُمُعَةِ، وَتَطَهَّرَ بِمَا اسْتَطَاعَ مِنْ طُهْر، ثُمَّ ادَّهَنَ أَوْ مَسَّ مِنْ طِيبٍ، ثُمَّ رَاحَ فَلَمْ يُفَرِّقْ بَيْنَ اثْنَيْنِ، فَصَلَّى مَا كُتِبَ لَهُ، ثُمَّ إِذَا خَرَجَ الْإِمَامُ أَنْصَتَ، غُفِرَ لَهُ مَا بَيْنَهُ وَبَيْنَ الْجُمُعَةِ الْأُخْرَى ) .

 

“…kisha akaswali kiasi chake alichokadiriwa…[Al-Bukhaariy na Muslim]. Hii ni sehemu ya Hadiyth ndefu yenye adabu za mtu anayejitayarisha kwenda Msikitini siku ya Ijumaa mpaka kumalizika kwa Swalah yenyewe.

 

Shaykh al-Islaam Ibn Taymiyyah (Allaah Amrehemu) amesema: “Ni bora kwa anayekwenda kwenye Swalah ya Ijumaa ajishughulishe na kuswali mpaka afike Imaam kama ilivyo katika kauli ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam): “…Kisha akaswali alichoandikiwa... [Al-Bukhaariy kutoka kwa Salmaan al-Faarisiy (Radhiya Allaahu ‘anhu)].

 

Katika athari za Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) ni kuwa walipofika Msikitini Ijumaa wanaswali walivyoweza, wapo waliokuwa wakiswali rakaa 10, wengine 12 na wengine 8 na wengine chini ya hapo. Hivyo, wamesema wengi miongoni mwa ma-Imaam kuwa hakuna kabla ya Ijumaa idadi maalumu za Sunnah” [Dkt. Swaalih Fawzaan, Al-Mulakhkhasw Al-Fiqhiy, Mj. 1, uk. 250 – 251 kutoka kitabu cha Fataawa].

 

Hata hivyo, Wanachuoni wengi wanaona kuwa haijathibiti Swalaah Sunnah kabla ya Ijumaa.

 

Ama baada ya Swalah ya Ijumaa unaweza kuswali mbili au nne. Ataswali nne hapo hapo msikitini, au ataswali mbili atakaporudi nyumbani kwake. Zote zimethibiti kwenye Hadiyth sahihi za Mtume (Swallaa Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kama zifuatavyo:

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Akiswali mmoja wenu Ijumaa, aswali baada yake nne.[Muslim kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu)].

 

Na Ibn ‘Umar (Radhiya Allaahu ‘anhuma) amesema:Hakika yeye (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akiswali baada ya Ijumaa Rak’ah mbili” [Al-Bukhaariy na Muslim].

 

Swalah ya Ijumaa inaswaliwa Msikitini peke yake. Ikiwa kwa sababu moja au nyingine hukuweza kuiswali Msikitini basi inafaa kwako uswali Swalah ya Adhuhuri. Ikiwa utaswali Swalah ya Adhuhuri huko nyumbani utaswali Sunnah za kawaida – kabla Rak’ah nne na baada Rak’ah mbili.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share