Khadiyjah Bint Khuwaylid (رضي الله عنها): Mama Wa Waumini Wa Kwanza

 

Khadiyjah Bint Khuwaylid (رضي الله عنها): Mama Wa Waumini Wa Kwanza

 

Muhammad Faraj Salem Al Saiy (Rahimahu Allaah)

 

Alhidaaya.com

  

 

 

 

 

Nasaba Yake

 

Anaolewa na Atiyq bin Aidh

 

Anaolewa na Abu Haalah

 

Hakupata kulisujudia sanamu

 

Anamuajiri Muhammad

 

Rudi naye Makkah haraka sana

 

Sifa za aliyetakaswa

 

Lakini umri wangu mkubwa

 

Anaolewa na Muhammad

 

Kuzaliwa kwa Qaasim

 

Sikubali kuachana naye

 

Aliy (Radhwiya Allaahu anhu)

 

Anakwenda Ghaari Hiraa

 

Zammiluwniy Zammiluwniy

 

Mpe Khadiyjah Salaam

 

Kufariki kwa Bibi Khadiyjah

 

Baadhi ya sifa zake

 

Mafunzo 

 

 

 

 

Nasaba yake

 

Jina lake ni Khadiyjah binti Khuwaylid bin Asad bin Abdil-‘Uzza Qusway bin Kilaab anayetokana na kabila la ki Quraysh  aliyezaliwa katika mwaka wa 68 kabla ya Hijrah yaani mwaka 556 baada ya Nabiy Issa (Alayhis-salaam).

 

Wazee wake walimlea kwa heshima na adabu ya hali ya juu na alikuwa akijulikana kwa jina la ‘Aliyetakasika’ hata kabla ya kuja kwa Uislamu.

 

 

Anaolewa na Atiyq bin Aidh

 

Imepokelewa kuwa siku moja vijana wa kabila la Kikureshi walipokuwa wamekaa karibu na Al-Ka’bah wakizungumza, aliinuka mmoja wao anayeitwa Al-Haarith akasema:

“Enyi ndugu zangu nimetia nia ya kuowa”.

Mmojawao akamwambia:

“Uamuzi mzuri huo, kwani tokea alipofariki mama yako na baada ya baba yako kuowa mke mwingine umekuwa unaishi peke yako”.

Mwengine akasema:

“Umefanya vizuri kuamua kuoa, kwani kila mwanamke anatamani kuolewa na mtu kama wewe, maana baba yako ni katika watu wanaoheshimika katika kabila la Kikureshi, na wewe unamiliki mali nyingi sana, sidhani kama yupo mwanamke atakayekukataa”.

Al Harith Akawatizama wenzake kwa muda, kisha akasema:

“Nyinyi mnadhania hivyo kwa sababu ni rafiki zangu, lakini mnakosea”.

“Tunakosea vipi?  Hebu tufahamishe”.

Akawaambia:

“Nilitaka kumuowa Khadiyjah, lakini baba yake alinikatalia kwa sababu eti anasema kuwa kabila langu ni duni kuliko kabila lake”.

Wenzake wakasema:

“Bila shaka hiyo, kwani Khadiyjah ni binti wa Khuwaylid bin Asad naye ni mtu mtukufu miongoni mwa mabwana wa kabila la Kikureshi mwenye kumiliki mali nyingi sana na nyumba kubwa ambayo daima inapokea wageni mbali mbali wanaokuja Makkah”.

Mwengine akasema:

“Na Khadiyjah binti yake ni uwa katika mauwa ya Makkah, kwani yeye ni mzuri wa umbo na mbora wa mwenendo na tabia, na sifa zake njema pamoja na hekima na uhodari wa kuyapima mambo katika akili yake, vyote hivyo vinajulikana na kila mtu”.

Walipokuwa katika hali ile alipita mbele yao mtu mrefu, mwingi wa haiba aliyevaa nguo zilizoshonwa vizuri na kupambwa, pamoja na kilemba, na nyuma yake kundi la watu lilikuwa likimfuata.

Watu wote walinyamaza kimya huku wakimtazama mtu huyo alipokuwa akipita, kisha mmoja wao akasema kwa sauti ndogo hafifu:

“Huyu ndiye Khuwaylid baba yake Khadiyjah, na walio nyuma yake ni watu wa kabila lake”.

Mwengine akasema:

“Amekuja kutufu Al-Ka’bah kama kawaida yake ya kila siku”.

Baada ya kutufu Al-Ka’bah, Khuwaylid akatafuta mahala karibu na Al-Ka’bah ili aweze kukaa na kujipumzisha, na alipokuwa katika hali ile, kijana mmoja aliiunuka na kwenda kumkabili.

Kijana huyo alikuwa mwenye sura na umbile la kupendeza ambaye kutokana na vazi lake alionyesha kuwa ni mtu tajiri sana, na nyuma yake pia kundi la watu lilikuwa  likimfuata kwa heshima na adabu.

Mtu huyo alikuwa ni Atiq bin Aidh, mmoja katika watu wanaoheshimika miongoni mwa matajiri wakubwa wa kabila la Kikureshi.anayetokana na kabila la Bani Makhzum.

Mmoja katika wale vijana akasema:

“Mtizameni vizuri! Mtu huyu anapigiwa mifano katika ushujaa na ukarimu”.

Baada ya kumkabili Khuwaylid bin Asad, Atiq akamwambia:

“Asubuhi njema ee Khuwaylid”.

Khuwaylid akamjibu:

“Njema kwako pia ee Atiq”.

Atiq:

“Nimekuja kwa ajili ya mazungumzo na wewe ee mwana wa ‘ammi yangu, lakini mazungumzo yenyewe hayafai kuzungumzwa hapa penye Al-Ka’bah mbele ya watu”.

Khuwaylid akamwambia:

“Karibu nyumbani kwangu”.

Siku ya pili yake Atiq akamwendea nyumbani kwake na kumwambia:

“Nimekuja kumposa binti yako ee bin ‘ammi yangu”.

Khuwaylid akamuuliza:

“Umekuja kumposa Khadiyjah au Hala?”

“Bali nimekuja kumposa Khadiyjah ee bin ‘ammi yangu”.

“Vyema, lakini itabidi kwanza nimuulize Khadiyjah mwenyewe ili nijuwe rai yake."

Atiq akasema kwa mshangao:

“Lakini wewe ni baba yake na unanijuwa mimi vizuri na unaijuwa daraja yangu katika kabila la Kikureshi pamoja na mwenendo na tabia zangu”.

Khuwaylid akamjibu:

“Bila shaka ee bin ‘ammi yangu natambuwa yote hayo, natambua vizuri pia kuwa anakustahikia mwanamke yeyote wa Kikureshi, isipokuwa mimi siwezi kuamua lolote juu ya Khadiyjah mpaka kwanza nimuulize mwenyewe na aridhike.”

Atiq akaondoka huku akisema kumwambia Khuwaylid:

“Vyema, fanya hivyo na mimi nitasubiri”.

Baada ya Atiq kuondoka, Khuwaylid akaingia kwa binti yake Khadiyjah na kumjulisha juu ya Atiq, akamwambia:

“Ee Khadiyjah, kwa hakika Atiq amekuja kukuposa, nini rai yako?”

Khadiyjah akasema kumwambia babake:

“Nini rai yako wewe kwanza ee baba yangu?”

Baba yake akamwambia:

“Yeye ni bwana katika mabwana wa Kabila la Bani Makhzum na ana mali nyingi sana”.

Bibi Khadiyjah akasema:

“Baba yangu, mimi sikuulizi juu ya sifa hizo, bali nataka kujuwa juu ya sifa zake nyingine kama vile ushujaa na ukarimu na kwamba hawafanyii ubakhili wenye kuhitaji wanapomwendea.”

Baba yake akamwambia:

“Atiq bin Aaidh yuko kama ulivyosema ee Khadiyjah. Yeye ni shujaa, mkarimu anayependa wageni. Hakika sifa zote unazozitafuta anazo mwanamume huyu”.

Bibi Khadiyjah akasema:

“Basi, ikiwa ni hivyo fanya vile unavyoona wewe kuwa ni sawa ee baba yangu”.

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahuu anha) akaolewa na Atiq wakapata mtoto waliyempa jina la Hind, na wakaishi kwa wema mpaka alipofariki mumewe jambo lililomfanya Bi Khadiyjah awe na huzuni kubwa.

 

 

 

Anaolewa na Abu Haalah

 

 

Haukupita muda mrefu bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) akaolewa na Nibaash bin Zirarah Al Tamiymiy aliyekuja kujulikana kwa jina la ‘Abu Haalah” na wakapata watoto wawili waliowapa majina ya Hind na Haalah. Waliishi kwa wema mpaka mumewe wa pili naye pia alipofariki dunia, na haukupita muda mrefu baba yake Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) naye pia akafariki dunia, jambo lililozidisha huzuni moyoni mwake. (zipo Riwaayah zinazosema kuwa baba yake bi Khadiyjah alifariki dunia baada ya binti yake kuolewa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na kwamba yeye ndiye aliyeifunga ndoa yao. Hata hivyo Riwaaya zenye nguvu zaidi zinasema kuwa alifariki kabla ya bibi Khadiyjah kuolewa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na kwamba aliyefunga ndoa ya bibi Khadiyjah na Nabiy  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa kaka yake anayeitwa Amru bin Khuwaylid.

 

 

Baada ya misiba hiyo iliyofuatiliana, Bibi Khadiyjah aliyerithi mali nyingi sana kutoka kwa baba yake na kutoka kwa waume zake waliofariki, aliamua kujitenga na watu akawa anajishughulisha na ulezi wa wanawe.

 

Watu wengi walipeleka posa kutaka kumuoa, lakini Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) aliwakataa kwa sababu alihisi kuwa wote hao walikuwa wakimtaka kwa ajili ya tamaa ya mali yake na uzuri wake.

 

 

 

Hakupata kulisujudia sanamu

 

Baada ya kupatwa na misiba miwili hiyo, (kufiwa na mumewe wa pili na kufiwa na baba yake) Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) aliishi akiwa mwingi wa huzuni na mwingi wa kutafakari. alijitenga mbali na watu na aliacha hata kwenda kutufu Al-Ka’bah kama alivyokuwa akifanya hapo mwanzo.

 

Inajulikana kuwa Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) hakupata hata siku moja kuyasujudia masanamu yaliyokuwepo hapo, na hii ni siri aliyomjulisha bin ami yake maarufu Waraqah bin Nawfil aliyekuwa akifuata dini ya Manasara.

 

Waraqah bin Nawfil huyu alikuwa mwenye taqwa ya Allaah ya hali ya juu na alikuwa akisoma sana vitabu vilivyotangulia na kwa ajili hiyo alikuwa akijulikana sana miongoni mwa waarabu wa Makkah kwa taqwa yake mbele ya Allaah na  wema wake.

 

Siku moja Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) akiwa na uso uliojaa huzuni alikwenda kumtembelea bin ami yake h

uyo aliyemuuliza:

“Kuna nini binti ami yangu, mbona nakuona una huzuni nyingi?”

Bibi Khadiyjah akamwambia:

“Sijaiona tena furaha tokea alipofariki baba yangu, na mali nyingi niliyoirithi haikuweza kuziba pengo lake”.

 

Waraqah akamwambia:

“Usihuzunike ee binti ami yangu, utakuja kuonana naye Aakhirah”.

 

Bibi Khadiyjah akashangaa:

“Aakhirah? Ni kitu gani hicho kinachoitwa Aakhirah ee bin ami yangu?”

Waraqah:

“Hayo ni maisha baada ya kifo, na katika maisha hayo kila nafsi itapata jaza yake kutokana na yale yaliyotanguliza mikono yake”.

Bibi Khadiyjah akauliza huku akitetemeka:

“Ina maana kuwa baba yangu hivi sasa yuhai?”

Waraqah akamwambia:

“Ndiyo, roho yake iko hai, isipokuwa mwili wake ushachanganyika na udongo wa ardhi”.

Bibi Khadiyjah akaanza kusema huku mwili wake ukiwa unamtetemeka:

“Bin ami yangu, nataka kukupa siri niliyoizuwia moyoni mwangu tokea nilipokuwa mtoto mdogo mwenye umri wa miaka sita”.

Waraqah akasema:

“Sema ee binti ami yangu wala usiwe na khofu”.

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) akasema:

“Nilipokuwa na umri wa miaka sita hivi, nilikwenda siku moja pamoja na baba yangu penye Al-Ka’bah  nikamuona akisimama mbele ya masanamu yaliyotengenezwa kwa mawe kisha anayakabili na kukiinamisha kichwa chake kwa kuyaheshimu. Nikamuuliza:

“Nini haya masanamu ee baba yangu?”

Akaniambia:

“Hii ni miungu tunayoiabudu”.

Nikashangazwa nikiwa bado mdogo, vipi watu wanayaabudu mawe yasiyoweza kudhuru wala kunufaisha?”

Waraqah akamtizama Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) huku akitabasamu, kisha akamwambia:

“Uliwahi kumhadithia mtu yeyote katika watu wa nyumbani?”

Bibi Khadiyjah akasema:

“Abadan, abadan. Sijapata kumhadithia mtu yeyote, kwani nilikuwa nikiogopa sana, nikaificha siri hii mpaka nilipokuja kukuhadithia wewe sasa hivi. Nini rai yako ee bin ami yangu?”

Waraqah akamwambia:

“Huo ndio ukweli wenyewe. Yale ni mawe tu yasiyodhuru wala kunufaisha. Na atatokea katika zama zetu hizi Rasuli anayesubiriwa atakayeyavunja masanamu haya na kuondoa ushirikina na uonevu katika ardhi”.

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahuu anhaa) akauliza:

“Na lini atakuja Rasuli huyo?”

Waraqah akasema:

“Allaah Ndiye Anayejuwa zaidi, isipokuwa vitabu vinasema kuwa; atatokea Nabiy katika wakati huu wetu na yeye ndiye atakayekuwa mwisho wa Manabii”.

Bibi Khadiyjah akauliza:

“Na katika kundi lipi atatokea Nabiy huyo?”

Waraqah akasema:

“Allaahu A’lam, lakini Mayahudi wanasema kuwa atakuwa katika wao, na vitabu vinasema kuwa atakuwa miongoni mwa Waarabu”.

Bibi Khadiyjah:

“Na uliyajuaje yote haya ee bin ami yangu?”

Waraqah:

“Haya yameandikwa katika Tuwraat kitabu cha Mayahudi na katika Injiyl kitabu cha Manasara”.

Bibi Khadiyjah akaondoka hapo huku mawazo yake yote yakiwa juu ya huyo Nabiy mpya aliyebashiriwa na bin ami yake atakayeuondoa ushirikina na dhulma na jeuri iliyopindukia mipaka, lakini wakati huo huo mazungumzo hayo yalimsaidia sana katika kupunguza uzito uliokuwepo kifuani pake na huzuni aliyokuwa nayo, na kwa ajili hiyo akaanza tena kufanya shughuli zake za kawaida pamoja na za kibiashara.

 

 

Anamuajiri Muhammad

 

Katika shughuli zake za kibiashara bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahuu anhaa) alikuwa akiwaajiri wanaume wawili kila mwaka. Mmoja kwa ajili ya kwenda Sham wakati wa Kusini na mwengine kwa ajili ya kwenda Yemen wakati wa Kaskazi. Na hivi ndivyo yalivyokuwa maisha ya kibiashara Bara ya Arabu yote.

Wakati huo huo Muhammad bin Abdillah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) (kabla ya kupewa Unabii) alikuwa akiishi pamoja na ami yake Abu Twaalib baada ya kufariki kwa babu yake Abdul-Muttwalib, na alikuwa akimsaidia ami yake katika shughuli za kibiashara na katika kuchunga kondoo na mbuzi mpaka alipofikia umri wa miaka ishirini na mitano, na kutokana na  uaminifu wake na ukweli wake, watu wa Makkah walikuwa wakimuheshimu sana.

 

Hii ukijumuisha pia kuwa Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hakupata hata siku moja kuyasujudia masanamu waliyokuwa wakiyaabudu na kuyaogopa wala hakupata kunywa pombe, na hakuwa akijishughulisha na anasa wala starehe ya aina yoyote ile katika starehe walizokuwa wakijishughulisha nazo vijana wa wakati ule.

Alikuwa mwema, msema kweli, muaminifu, mwenye tabia na mwenendo mwema uliompendeza kila mtu, na alikuwa na haiba kubwa sana pale Makkah hata akawa maarufu miongoni mwao kwa jina la ‘Asw-Swaadiqul-Amiyn’, bimaana Mkweli Mwaminifu. Au ‘Muhammad Al-Amiyn’, na maana yake ni Muhammad muaminifu.

 

Sifa zote hizo zilikuwa zikimfikia bibi Khadiyjah aliyekuwa mfanya biashara maarufu pale Makkah pamoja na sifa nyingine mbali mbali, na pia zilikuwa zikimfikia khabari za kusafiri kwake pamoja na ami yake Abu Twaalib katika shughuli za kibiashara kwenda nchi ya Sham, na kwamba ami yake alikuwa akipata faida kubwa sana tokea alipoanza kushirikiana naye katika shughuli hizo.

khabari hizo zikawa zinamshughulisha sana bibi Khadiyjah na usiku mmoja katika siku za joto alipokuwa amekaa juu ya dari la nyumba yake pamoja na mwanamke mmoja aitwae Nafiysah binti Munabbih, bibi Khadiyjah alikuwa akitazama chini sana huku akitafakari, jambo lililomfanya Nafiysah amuulize:

“Unatafakari juu ya nini ee Khadiyjah?”

Bi Khadiyjah:

“Natafakari juu ya jambo la ajabu sana”.

Bi Nafiysah:

“Unanificha mimi?”

Bi Khadiyjah:

“Mimi siwezi kukuficha kitu ee Nafiysah, jambo lenyewe linahusiana na Muhammad bin Abdillah!”.

Bi Nafiysah:

“Ah! Muhammad Muaminifu. Unataka nini kwake?”

Bi Khadiyjah:

“Muhammad Muaminifu husafiri baadhi ya wakati kwa ajili ya shughuli za kibiashara pamoja na ami yake Abu Twaalib, ningefurahi kama angekubali pia kushughulikia biashara zangu maana yeye ni mtu wa pekee ninayeweza kumuaminisha katika mali yangu. Lakini sijuwi vipi nitaweza kumjulisha?”

Nafiysah:

“Mimi, mimi ndiye nitakayemjulisha ee Khadiyjah, lakini nitazungumza na ‘ammi yake Abu Twaalib maana naona haya kumkabili Muhammad juu ya jambo hili.”

Abu Twaalib akalikubali ombi hilo na akamnasihi Muhammad akubali pia, na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia ‘ammi yake:

“Ikiwa wewe unaona sawa, basi na mimi nimekubali”.

Bibi Khadiyjah alifurahi sana alipojulishwa kuwa Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amelikubali ombi lake, akatayarisha msafara wa biashara na kumtaka mtumishi wake Maysara afuatane na Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwa ajili ya kumhudumia na kumshughulikia katika safari ndefu hiyo.

Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akafanikiwa kuuza bidhaa zote za bibi Khadiyjah katika masoko ya Sham na akarudi akiwa amempatia faida kubwa sana kuliko alivyowahi kupata miaka yote iliyopita.

 

 

 

Rudi naye Makkah haraka sana

 

Tokea waliporudi kutoka safari ya Sham yule kijana Maisarah aliyevutiwa sana na tabia na mwenendo wa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)  alouona walipokuwa safarini, akawa anamuhadithia bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) juu ya yale aliyokuwa akiyaona safarini walipokuwa wakienda na walipokuwa wakirudi na baadhi ya miujiza iliyokuwa ikitokea.

Bibi Khadiyjah naye aliyekuwa wakati wake wote anawaza juu ya Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akipenda kila mara kuhadithiwa juu ya sifa zake hizo, na siku moja alipokuwa amekaa pamoja na mtumishi wake huyo, akamwambia:

“Enhe! Hebu nihadithie vizuri juu ya safari yako na Muhammad”.

Maisarah akasema:

“Sikupata kuona mtu bora wa kusafiri naye kuliko yeye. Alikuwa mtulivu, hana kiburi, mkarimu na mpole sana. Nilikuwa ninapoumwa ananishughulikia na ninapochoka ananisaidia, na alikuwa akigawana na mimi sawa sawa chakula chake na maji yake. Kwa hakika alikuwa akinitendea kama kwamba ni ndugu yake.

Lakini jambo lililonistaajabisha zaidi ee bi Khadiyjah,” akaendelea kusema: “Kulikuwa na kiwingu kilichokuwa kikimfuata wakati wote tokea tulipoondoka mpaka tuliporudi. Kilikuwa kikimfuata na kumkinga na jua kali wala hakuwa akihisi joto hata kidogo wakati wote wa safari.

Isitoshe, Muhammad hapendi kusema sana, na kila tunaposimama kwa ajili ya kupumzika alikuwa akijitenga peke yake na alikuwa akipenda kutizama mbinguni kwa khushuu na mdomo wake ulikuwa daima ukitikisika huku akisema maneno yasiyosikika”.

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) aliyekuwa na shauku ya kutaka kujuwa zaidi khabari za Muhammad akasema:

“Enhe! Kisha? Endelea, nini kilichotokea baadaye?”

Maisarah akasema:

“Tulipokuwa tukirudi Makkah, tulisimama mahali muda mdogo kwa ajili ya kujipumzisha, na mimi nikaondoka kwenda kutafuta chakula cha ngamia, na mahali hapo palikuwa na mti mkubwa sana na Muhammad alikaa chini ya mti huo huku akitizama mbinguni kama kawaida yake kama kwamba anatafuta kitu, na karibu na mahali hapo palikuwa na hekalu Swalihina mmoja aitwae Nastwur aliyenijia mimi na kuniuliza:

“Nani huyu kijana aliyekaa chini ya mti ule?”

Nikamwambia;

“Huyu ni kijana anayetokana na mabwana wa kabila la ki Quraysh”.

Akaniambia:

“Umeona lolote lisilo la kawaida kutoka kwake?”

Nikamwambia:

“Nimeona kiwingu kikimfuata kikimkinga kutokana na jua kali tokea tulipoondoka na wala hakikumuacha abadan”.

Akauliza tena:

“Macho yake yakoje?”

Nikamjibu:

“Meusi na makubwa na katika weupe wake umo wekundu khafifu ndani yake”.

Akasema:

“Kijana huyu atakuwa na shani kubwa, rudi naye Makkah haraka sana, kwani hakupata kukaa chini ya mti huu isipokuwa Nabiy”.

 

Maneno haya yalimtia kizunguzungu bibi Khadiyjah na tokea alipoondoka hapo akawa usiku na mchana hana analowaza isipokuwa juu ya Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

 

 

Sifa za aliyetakaswa

 

 

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) akaanza kufikiri huku akikumbuka na kuunganisha maneno ya Maisarah na maneno aliyoambiwa na bin ‘ammi yake Waraqah bin Nawfil, akawa anajisemesha:

“Kwa nini isinipitikie wakati wote huu? Huyu ndiye kijana anayetokana na mabwana wa kabila la ki Quraysh anayejulikana kwa ukweli na uaminifu na upole na ukarimu, na ma-Quraysh wote wanamuheshimu na kumtukuza kutokana na kujitenga kwake mbali na tabia zote mbaya walizokuwa nazo vijana wa kabila la ki-Quraysh  na wengineo.

Na huyu ndiye kijana aliyesafiri na mali yangu na kunipatia faida kubwa sana, na huyu ndiye kijana ambaye kiwingu kilikuwa kikimkinga kutokana na juwa kali tokea alipoianza safari yake mpaka aliporudi. Na huyu ndiye kijana ambaye Swalihina Nastwur amesema juu yake kuwa atakuwa na shani kubwa akamtaka Maisarah arudi naye Makkah haraka sana”.

 

Bibi Khadiyjah akawa anawaza na kukumbuka yote hayo mpaka akawa na uhakika ndani ya moyo wake kuwa sifa kama hizi haziwezi kumuandama mtu wa kawaida.

Sifa njema kama hizi ambazo si kila mtu anaweza kuwa nazo hazipatikani isipokuwa kwa watu waliochaguliwa na kutakaswa.

 

Kutokana na yote haya, bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) akazidi kujishughulisha na kuwaza juu ya Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

 

 

Lakini umri wangu mkubwa

 

Baada ya kuwaza na kufikiri muda mrefu, bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) akafikia uamuzi wa kutaka kuolewa na Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

“Kwa nini nisimtake Muhammad aniowe? Inagawaje fikra hii ni mfano wa ndoto, lakini ni jambo linalowezekana. Lakini vipi? Nani atakayekubali kunifikishia ombi langu?”

Alipokuwa katika hali ile, mlango ukagongwa.

“Nani anayegonga mlango?”

“Mimi dada yako Haalah.”

Bibi Khadiyjah akamkaribisha dada yake.

“Ahlan wa sahlan, karibu ee Haalah”

Haalah:

“Ahsante Khadiyjah vipi hali zenu?”

Khadiyjah:

“Hatujambo, ziara hii ya ghafla naona.”

Khadiyjah:

“Bila shaka ee dada yangu, kwani nimekuja kukujulia hali yako tu”.

Khadiyjah:

“Kuijua hali yangu tu! Mbona unasema maneno ya kiajabu, au kuna jambo unataka kunificha?”

Haalah akamtizama dada yake mtizamo wa kuchunguza, kisha akamwambia:

“Abadan, hakuna la kukuficha isipokuwa mchana wa leo ulinichukuwa usingizi nikakuota unatembea mfano wa mtu aliyepotea katika njia ya kiza na nyuma yako sauti inakwambia: “Nenda mbele, nenda mbele”. Nikaona bora nije kukujulia hali yako, ingawaje sijuwi ndoto hiyo tafsiri yake nini”.

 

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu  anhaa) akatabasamu kidogo kisha akasema:

“Kusema kweli mimi siku hizi ninaishi ndani ya mawazo mengi sana.”

Haalah:

“Unawaza juu ya nini na wewe upo katika neema kubwa kama hii?”

Khadiyjah:

“Muhammad, ee dada yangu. Nafikiri juu ya sifa zake na utukufu wake ambao hajapata kuufikia hata mmoja katika watu wa kabila la ki-Quraysh.”

Haalah:

“Na nini mwisho wa fikra hizo?”

Khadiyjah:

“Nataka aniowe”.

Haalah:

“Basi muombe akuowe”.

Bibi Khadiyjah akamjibu kwa uoga:

“Naogopa asije akanikataa, kwani yeye ni kijana anayeheshimika kupita vijana wote”

Haalah:

“Na wewe pia dada yangu ni mtu mtukufu unayeheshimika na watu wote”.

Khadiyjah:

“Lakini umri wangu mkubwa unaokaribia miaka arubaini, na nishaolewa mara mbili, wakati yeye bado ni kijana mwenye umri wa miaka ishirini na mitano na bado hajapata kuowa. Vipi Muhammad atakubali kumuowa mwanamke aliye na umri sawa na mama yake aliyekwisha olewa mara mbili na ana watoto?”

Haalah akasema:

“Nani aliyekujulisha na Muhammad mara ya mwanzo hata ukaweza kumpa mali yako aifanyie biashara?”

Khadiyjah:

“Rafiki yangu mmoja anayeitwa Nafiysah”.

Haalah:

“Basi Nafiysah huyo huyo ndiye atakayeweza kukufikishia ombi lako hilo”.

Kisha Haalah akamuaga dada yake na kuondoka

 

 

 

Anaolewa na Muhammad

 

Ziara ya Haalah ilikuwa mfano wa ufunguo wa kheri katika nafsi ya bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa), kwani siku ya pili yake Nafiysah alipokuja kumtembelea bibi Khadiyjah, akamhadithia juu ya mazungumzo yaliyopita baina yake na baina ya dada yake Haalah, na Nafiysah akakubali kuchukuwa jukumu la kulifikisha ombi hilo kwa Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)

Alipoondoka, Nafiysah alielekea moja kwa moja mpaka nyumbani kwa Abu Twaalib alipokuwa akiishi Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)

na alipomuona akamwambia:

“Ee Muhammad, wewe una umri wa miaka ishirini na tano na mpaka sasa bado hujaowa.”

Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akashangazwa sana na maneno hayo, akamuuliza:

“Kipi kilichokufanya ujishughulishe na jambo hili ee Nafiysah?”

Nafiysah:

“Bibi anayeheshimika anataka umuowe, nini rai yako?”

Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

 

“Bibi gani huyo?”

Nafiysah:

“Bibi huyo ni Khadiyjah binti Khuwaylid, na wewe unamuelewa vizuri juu ya heshima yake na utukufu wake na sifa zake zote njema”.

Muhammad ((Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)

“Naam, hakika yeye ni mtu anayeheshimika, lakini mimi sina mali hata niweze kumuowa.”

Nafiysah:

“Yeye hana haja ya mahari, kwani unajuwa vizuri kuwa yeye hana shida ya mali na anao utajiri mkubwa”.

Muhammad:

“Mimi utajiri haunishughulishi, kwani mali inakuja na kuondoka, na Khadiyjah pia ni mwanamke mzuri wa umbo na tabia na mwenendo, lakini niache nimshauri ‘ammi yangu kwanza juu ya jambo hili”.

‘Ammi yake akamwambia:

“Ee Muhammad, hii ni bahati iliyokujia kutoka mbinguni. Naapa kuwa Khadiyjah ni mwanamke aliyetakasika kupita wote katika Makkah na mwenye akili na uwezo wa kupima mambo kupita wote, na mwenye hekima kupita wote na anayetokana na ukoo bora kupita wote. Wangapi wenye mali na jaha walitaka kumuoa akawakataa, na leo anakutaka wewe wakati huna mali yoyote, hii ni bahati kubwa.

Kubali ee mwana wa ndugu yangu, kwani asingekutaka isipokuwa amekuwekea heshima kubwa sana”.

Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akakubali, na bibi Khadiyjah akafanya arusi kubwa sana iliyohudhuriwa na watu wengi, na wanyama wengi sana wakachinjwa siku hiyo na kila muhitaji alifaidika.

 

 

 

Kuzaliwa kwa Qaasim

 

 

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahuu anhaa) alizaa na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) watoto sita. Wanaume wawili na wanawake wanne. Watoto wa kiume aliwapa majina ya Qaasim na Abdullaah, aliyekuwa akijulikana pia kwa jina la Atw-Twaahir. Na watoto wa kike ni Ruqayyah na Zaynab na Ummu Kulthuwm na Faatwimah (Radhwiya Allaahu ‘anhunna).

 

Katika mwaka wao wa mwanzo tokea kuoana walijaaliwa kupata mtoto wa kiume waliyempa jina la Qaasim, wakafurahi sana, na kwa ajili hiyo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akawa anajulikana kwa jina la ‘Abal-Qaasim’, na maana yake ni 'baba yake Qaasim'.

Lakini Qaasim hakuishi muda mrefu, kwani alifariki dunia akiwa na umri wa miaka miwili, na wazee wake walihuzunika sana, lakini walisubiri na kumshukuru Allaah.

 

Kisha akazaliwa Abdullaah aliyefariki pia akiwa mtoto mchanga, kisha Zaynab, kisha Ruqayyah aliyefanana na mama yake, kisha akazaliwa Ummu Kulthuwm, kisha akazaliwa Faatwimah aliyefanana sana na baba yake hasa katika mwendo na sauti.

 

 

 

Sikubali kuachana naye

 

Siku moja Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) aliingia nyumbani akiwa amemshika mkono mtoto mdogo, akamkabili Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)  na kumwambia:

“Mtoto huyu nakupa zawadi, mchukuwe, atakusaidia na kukuhudumia”.

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)  akamtizama mtoto yule machoni akaona dalili ya hekima ndani yake, akamuuliza:

“Jina lako nani na ilikuwaje ukatekwa?”

Mtoto akajibu:

“Jina langu ni Zayd bin Haarithah, natokana na kabila la Kalbin na nilikamatwa na kundi la mabedui walionileta katika soko la Akadha na kuniuza huko”.

Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)  akafurahishwa naye, akawa anampenda na kumkirimu sana, na Zayd naye alikuwa akimpenda sana Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na katika nyakati za usiku pale Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)  anapojishughulisha na kutafakari na kuomba, mtoto huyo alikuwa karibu yake kwa ajili ya kumtumikia.

 

Baba yake Zayd alipopata khabari za kutekwa kwa mwanawe na baada ya kuulizia ulizia na kujulishwa kuwa mwanawe alikuwa amemilikiwa na Muhammad bin Abdillaah, akaifunga safari ya kuelekea Makkah na alipowasili alisimama mbele ya Al-Ka’bah akasema kwa sauti kubwa:

“Enyi watu wa Makkah! Nyinyi ni watu wakarimu mnaohudumia mahujaji na mnaowasaidia mateka. Nimekujieni kwa ajili ya mwanangu aliye mikononi mwenu nataka munirudishie mwenyewe”.

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliposikia maneno hayo akatangulia mbele na kumkabili Haarithah huku akiwa amemshika mkono Zayd, akainama na kumuuliza:

“Unawajua ni nani hawa?”

Zayd akasema:

“Ndiyo. Huyu ni baba yangu na yule ni ‘ammi yangu”.

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia:

“Basi wazee wako hawa wamekuja kukuchukua ili urudi nao”.

Kisha akamuacha mkono na kumtanguliza mbele yao.

Zayd (Radhwiya Allaahu ‘anhu) akamkabili baba yake na kumwambia:

“Baba yangu, mimi sikubali kuachana na mtu huyu abadan, huyu ni mtu adhimu mwenye moyo mkubwa uliobarikiwa, na kama mmoja wenu ataishi naye siku moja tu, basi hatokubali kuachana naye maisha yake yote.”

Kisha akamkabili Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na kumwambia:

“Sitomchaguwa mwengine isipokuwa wewe tu. Wewe ndiye baba yangu na wewe ndiye ‘ammi yangu”.

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alitokwa machozi ya furaha, akamshika mkono Zayd huku akiyafuta machozi yake, kisha akasogea naye mpaka penye uwanja wa Al-Ka’bah na kusema kwa sauti kubwa:

“Shuhudieni kuwa Zayd ni mwanangu, ananirithi na mimi namrithi”.

Maneno haya yalimfurahisha sana hata Haarithah baba yake Zayd kwa kujuwa kuwa mwanawe si kama ameachwa huru tu, bali amekuwa mwana wa Muhammad Mkweli Mwaminifu. Na hii ilikuwa ndiyo kawaida iliyokuwa ikitumika wakati ule.

 

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akimpenda sana Zayd (Radhwiya Allaahu ‘anhu) hata akawa anajulikana kwa jina la Zayd bin Muhammad mpaka pale ilipoteremshwa Aayah ya tano ya Suwratul-aAhzab iliyoharamisha mtu kuitwa kwa ubini usiokuwa wa baba yake.

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

ادْعُوهُمْ لِآبَائِهِمْ هُوَ أَقْسَطُ عِندَ اللَّـهِ ۚ فَإِن لَّمْ تَعْلَمُوا آبَاءَهُمْ فَإِخْوَانُكُمْ فِي الدِّينِ وَمَوَالِيكُمْ ۚ  

Waiteni kwa (majina ya) baba zao, huo ndio uadilifu zaidi mbele ya Allaah. Na ikiwa hamuwajui baba zao, basi ni ndugu zenu katika Dini na walio katika ulinzi wenu.  [Al-Ahzaab: 5]

 

 

Kisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)  Akaharamishas pia mtu kurithiwa na mwanawe wa kupanga (adopted child) katika Aayah ya 75 ya Suwratul Anfaal Anaposema:

 

وَأُولُو الْأَرْحَامِ بَعْضُهُمْ أَوْلَىٰ بِبَعْضٍ فِي كِتَابِ اللَّـهِ ۗ إِنَّ اللَّـهَ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ﴿٧٥﴾

Na ndugu wa uhusiano wa damu wanastahikiana wenyewe kwa wenyewe (kwa kurithiana), katika shariy’ah ya Allaah. Hakika Allaah ni Mjuzi wa kila kitu [Al-Anfaal: 75]

 

 

 

 

Aliy (Radhwiya Allaahu ‘anhu)

 

 

Katika nyumba ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwepo mtoto mwingine wa kiume naye ni Hind mtoto wa bibi Khadiyjah kwa mume wake wa  pili ’Abu Haalah’, na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akimpenda sana na akamlea malezi bora, akamuonyesha mapenzi na huruma na alikuwa akimtendea kama anavyowatendea wanawe.

Alipotimia miaka minane, Aliy (Radhwiya Allaahu 'anhu)  naye akachukuliwa na Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na kulelewa katika nyumba ya bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwa ajili ya kumpunguzia ‘ammi yake Abu Twaalib mzigo wa ulezi baada ya ‘ammi yake kupata shida mbali mbali.

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) alimpokea Aliy (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwa furaha na akamlea na kumuenzi kama anavyowalea na kuwaenzi wanawe.

 

 

 

Anakwenda Ghaar Hiraa

 

 

Siku moja Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alimwambia bi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kuwa anahisi moyoni mwake kama kwamba anatakiwa ende penye pango linaloitwa Ghaari Hiraa nje kidogo ya mji wa Makkah.

 

Bi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) akamwambia:

“Haya nenda, lakini pango hilo liko nje ya mji na mimi nakuogopea wewe kubaki huko peke yako”.

Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  akamwambia:

“Usiogope Khadiyjah, kwani Allaah yuko pamoja nami”.

 

Baada ya bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kumtayarishia chakula pamoja na baadhi ya mahitajio yake, Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  akaondoka na kuelekea Ghaari Hiraa kwa ajili ya kukaa huko na kutafakari juu ya Allaah.

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akipenda kwenda pangoni hapo na kukaa kimya huku akitazama juu mbinguni. Alikuwa akiziangalia nyota na sayari, juwa na mawingu, mvua na upepo huku akitafakari na kujiuliza:

“Nani aliyevitengeneza vyote hivi? Bila shaka ipo nguvu kubwa yenye uwezo wa kuumba uhai pamoja na kuvitengeneza vyote hivi”.

Akawa anaendelea katika hali hii ya kutafakari wakati mkewe bi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) akibaki nyumbani na kuendesha shughuli zake. Lakini bibi Khadiyjah alikuwa kila anapomfikiria mumewe akiwa peke yake pangoni tena nje ya mji alikuwa wakati wa mchana hana raha na wakati wa usiku hapati usingizi.

Alikuwa kila siku akimtuma mtu kwenda pangoni huko ili amletee khabari za Muhammad na pia kwa ajili ya kumpelekea maji na chakula na baadhi ya mahitajio yake, na mara nyingine alikuwa akienda yeye mwenyewe.

Siku moja Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alirudi nyumbani kutoka pangoni akiwa na hofu kubwa sana, na bibi Khadiyjah alipomuona katika hali ile akamuuliza:

“Kuna nini Muhammad?”

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia:

“Ee Khadiyjah! Nilipokuwa nikitembea huku na kule juu ya jabali, ghafla nikaona Nuru iking’ara juu yangu kisha nikasikia sauti ikiniita:

“Ee Muhammad, ee Muhammad”.

Bibi Khadiyjah akamuuliza:

“Na umeweza kujuwa sauti hiyo inatokea wapi ee Abal-Qaasim?”

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia:

“Sikuweza kujuwa ee Khadiyjah, na nilikuwa kila ninapoisikia sauti ninageuka huku na kule kumtafuta mwenye sauti hiyo na wala simuoni mtu, nikaingiwa na khofu na kuamua kurudi nyumbani”.

Bibi Khadiyjah akafanya haraka kumwendea bin ‘ammi yake Waraqa bin Nawfil na kumhadithia yote aliyohadithiwa na Muhammad, na Waraqah akamwambia:

“Ee binti wa ‘ammi yangu, hizi ni bishara njema kutoka mbinguni, mpe hongera zangu Muhammad na mwambie awe mvumilivu”.

 

 

 

Zammiluwniy, Zammiluwniy

 

Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akawa anaendelea kwenda Ghaari Hiraa, na bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) akawa anaendelea kumshughulikia kwa kuwatuma watumishi wampelekee vyakula na mahitajio yake ya kila siku na wakati mwingine yeye mwenyewe alikuwa akienda kumtembelea mumewe pangoni mpaka ilipofika siku ile aliporudi nyumbani Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akiwa anatetemeka huku meno yake yakigongana na kumwambia mkewe:

 

Zammiluwniy Zammiluwniy’ – na maana yake (nifunikeni, nifunikeni). Bibi Khadiyjah akamlaza mumewe kitandani kisha akamfunika huku akimpangusa jasho lililokuwa likimtoka kwa wingi kichwani na huku akimwambia maneno ya kumtuliza mpaka usingizi ulipomchukuwa.

 

Aliamka akiwa bado uoga unaonekana usoni pake na bibi Khadiyjah akamuuliza:

“Una nini ee Abal-Qaasim?”

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia:

“Nilikuwa nimekaa pangoni, ghafla nikaona nuru juu yangu iliyonipitia kama umeme, kisha nikamuona mtu anateremka kutoka mbinguni huku akinikaribia. Nikaingiwa na khofu, lakini mtu huyo akaninyanyua na kunibana kwa nguvu kifuani pake kisha akaniacha, kisha akaniambia:

Iqra-a” – (‘soma’)

Nikamjibu kuwa mimi sijuwi kusoma. Akaninyanyua tena na kunibana kwa nguvu zaidi kifuani pake kisha akaniacha na kuniambia tena:

“Iqra-a”

Nikamwambia:

Maa – ana biqaarii – (Mimi sijuwi kusoma).”

Kisha akaninyanyua tena mara ya tatu na kunibana tena kifuani pake kisha akaniacha akaniambia tena:

 

 

اقْرَأْ بِاسْمِ رَبِّكَ الَّذِي خَلَقَ ﴿١﴾ خَلَقَ الْإِنسَانَ مِنْ عَلَقٍ ﴿٢﴾ اقْرَأْ وَرَبُّكَ الْأَكْرَمُ ﴿٣﴾ الَّذِي عَلَّمَ بِالْقَلَمِ ﴿٤﴾ عَلَّمَ الْإِنسَانَ مَا لَمْ يَعْلَمْ ﴿٥﴾

 

Soma kwa Jina la Rabb wako Aliyeumba. Amemuumba mwana-Aadam kutokana na pande la damu linaloning’inia. Soma na Rabb wako ni Mkarimu kushinda wote.  Ambaye Aliyefunza kwa kalamu. Amemfunza mwana-Aadam ambayo asiyoyajua. [Al-‘Alaq (96) 1- 5]

 

 

Maneno hayo yalimshituwa sana bibi Khadiyjah, akamtaka Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) avae nguo haraka na afuatane naye mpaka kwa Waraqah bin Nawfil ili amhadithie mwenyewe yale aliyoyaona, na Waraqah akamwambia:

“Huyu ndiye Malaika mkubwa ‘Jibriyl’ ambaye Allaah aliwateremshia Muwsaa na ‘Iysaa, yareti kama ningeliishi mpaka pale watu wako watakapokutoa nchini kwako”.

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamuuliza:

“Hivyo watakuja kunitoa?”

Waraqah akasema:

“Ndiyo, hapana aliyekuja na haya uliyokuja nayo wewe isipokuwa lazima atafanyiwa uadui, na nikijaaliwa kuishi mpaka siku hiyo, basi nitakusaidia mpaka utakapopata ushindi”.

 

Bibi Khadiyjah akarudi nyumbani haraka akiwa amefuatana na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) huku moyoni mwake akiona fahari kubwa kuwa baraka za utume zimeangukia nyumbani kwake.

Siku moja bibi Khadiyjah aliingia nyumbani kwake na kumuona Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akitetemeka mwili mzima juu ya tandiko lake huku akisema:

“Khadiyjah. Jibriyl amenijia tena, akaniambia:

 

 

يَا أَيُّهَا الْمُدَّثِّرُ﴿١﴾ قُمْ فَأَنذِرْ﴿٢﴾ وَرَبَّكَ فَكَبِّرْ﴿٣﴾ وَثِيَابَكَ فَطَهِّرْ﴿٤﴾ وَالرُّجْزَ فَاهْجُرْ﴿٥﴾ وَلَا تَمْنُن تَسْتَكْثِرُ﴿٦﴾ وَلِرَبِّكَ فَاصْبِرْ﴿٧﴾

Ee mwenye kujigubika! Simama na uonye .Na Rabb wako mtukuze. Na nguo zako toharisha. Na najisi (masanamu( epukana nayo. Na wala usifanye fadhila kwa ajili ya kutaraji kukithirishiwa. Na kwa ajili ya Rabb wako subiri. [Al-Muddath-thir: 1- 7]

 

 

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) akainua uso wake kutizama juu mbinguni huku akimshukuru Rabb wake, kisha akamtizama Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliyekuwa akionyesha kuwa amechoka sana na kumwambia:

“Tulia upumzike ee Muhammad”.

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akamwambia:

“Zimekwisha zama za kupumzika ee Khadiyjah. Na umewadia wakati wa jihaad. Jibriyl keshanijia na ananitaka niianze kazi ya kufikisha kwa watu Risala ya Allaah  utakaouondoa ushirikina pamoja na uchupaji wa mipaka.”

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) akamwambia mumewe:

Labbayka ee Rasuli wa Allaah, na mimi ni wa mwanzo kukuamini”.

Akasilimu bibi Khadiyjah pamoja na wanawe wote wakiwemo Aliy na Zayd (Radhwiya Allaahu ‘anhum), lakini haukupita muda mrefu Waraqah bin Nawfil alifariki dunia kabla ya kupewa Unabii Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) jambo lililomhuzunisha sana bibi Khadiyjah, kwani Waraqah alikuwa akiwasaidia sana katika kumliwaza Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wakati wa khofu, na kwa ajili hiyo bibi Khadiyjah akahisi kuwa mzigo huo sasa umemuangukia yeye.

Hata hivyo bibi Khadiyjah alikuwa akimsaidia sana Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) pale anapoona dhiki, hasa katika zile siku ambazo wahyi unakatika na Jibriyl anachelewa kumshukia, hapo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) humwendea bibi Khadiyjah na kumsikitikia na bibi Khadiyjah kwa upande wake humpoza na kumwambia:

“Hapana ee Muhammad. Wa-Allaahi Allaah Hawezi kukuhizi abadan, kwani wewe ni mkweli muaminifu, uliyetakasika mwenye kuwaendea watu wako na mwenye kuwasaidia wenye kuhitaji na kumuokoa mwenye dhiki”.

 

 

 

Mpe Khadiyjah Salaam

 

Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akawa anaendelea kwenda pangoni kwa kufanya ibada zake, na mara nyingi Jibriyl (Alayhis Salaam) alikuwa akimjia.

 

 

Imepokelewa kutoka kwa Abu Huraryah (Radhwiya Allaahu anhu) kuwa asubuhi moja bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) alipokuwa njiani kuelekea pangoni alikutana na mwanamume mmoja aliyemsalimia na kumuuliza juu ya Muhammad. Bibi Khadiyjah hakumjibu mtu huyo akihofia asije kuwa adui anayeweza kumdhuru Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Ikajulikana baadaye kuwa huyo alikuwa Jibriyl katika sura ya ki bin-Aadam. Kwani Jibriyl alitangulia kufika pangoni kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na kumwambia:

“Khadiyjah sasa hivi atawasili akiwa amebeba chakula na maji kwa ajili yako. Atakapowasili mpe Salaam zitokazo kwa Rabb wake na mpe bishara njema juu ya nyumba aliyokwishajengewa Jannah (Peponi)”.

 

Baada ya kutaabika njiani, bibi Khadiyjah aliwasili pangoni na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimpokea kwa furaha huku akimwambia:

“Bishara njema kwako ee Khadiyjah. Amenijia Jibriyl hivi punde na amenipa Salaam zitokazo kwa Rabb wako Anayekupa bishara njema juu ya nyumba uliyokwishajengewa huko Jannah (Peponi)”.

 

 

 

Kufariki kwa Bibi Khadiyjah

 

Watu wakaanza kuingia katika Dini ya Kiislamu kwa wingi, na Abubakar (Radhwiya Allaahu anhu) alikuwa wa mwanzo katika wanaume akifuatiliwa na ‘Uthmaan bin ‘Affaan, Az-Zubayr  bin ‘Awaam, Abdur-Rahmaan bin ‘Awf, Sa’ad bin Abi Waqaas na Twalhah bin Ubaidillaah (Radhwiya Allaahu anhum). Wote hawa walisilimishwa na Abubakar siku ya mwanzo baada ya kusilimu yeye mwenyewe, akaenda nao kwa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), na wote hawa ni katika wale kumi waliobashiriwa na Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuwa wataingia Jannah.

 

Siku iliyofuata Abubakar (Radhwiya Allaahu anhu) aliwasilimisha vigogo wengine wanne na kuja nao mbele ya Rasuli wa Allaah  (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), nao ni ‘Uthmaan bin Madha-un, Abu Ubaydah Aamir bin Al-Jarraah, Abu Salamah na Al-Arqam bin Abi Arqam.

 

Bibi Khadiyjah naye aliitumia mali yake yote katika kuunusuru Uislaam, na kwa ajili hiyo nguvu ikaanza kuongezeka kidogo kidogo jambo lililowaghadhibisha sana ma Quraysh, wakaamua kuwazunguka na kuwapiga pande Waislaam muda wa miaka mitatu na kuwazuwia wasiweze kununua chochote, hata chakula. Ukawapitikia Waislamu wakati mgumu sana mpaka wakawa wanakula majani ya miti.

 

Waislaam wakahamia katika nyumba za Abu Twaalib, na bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) alikuwa wakati mwingine akihatarisha maisha yake kwa kununua chakula na kuwapelekea kwa siri.

 

Haukupita muda mrefu tokea kumalizika kupigwa pande huko alifariki dunia Abu Twaalib ‘ammi yake Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), na miezi miwili baadaye akafariki mama wa Waislaam Bibi Khadiyjah binti Khuwaylid (Radhwiya Allaahu anhaa) katika mwaka uliokuja kujulikana kama ‘mwaka wa huzuni’ kwa sababu katika mwaka huo Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alifiwa na wapenzi wake wawili hao waliokuwa wakimsaidia sana na kumkinga.

 

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) akiwa na umri wa miaka sitini na mitano alifariki katika mwezi wa Ramadhwaan mwaka wa kumi tokea Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kupewa Unabii. Zipo Riwaayah zinazosema kuwa alifariki miaka mitatu kabla ya Hijrah na Riwaayah nyingine zinasema miaka minne na nyingine zinasema mitano, na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mwenyewe ndiye aliyeteremka kaburini na kumzika na wakati huo hakukuwa na Swaalah ya Janaazah.

 

 

 

Baadhi ya sifa zake

 

Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hakupata kumpenda yeyote kati ya wake zake kama alivyompenda bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa), na hakuoa mke mwingine mpaka alipofariki bibi Khadiyjah.

 

Ingawaje baadaye alioa wake wengi akiwemo bibi ‘Aaishah bint Abubakar (Radhwiya Allaahu anhaa) aliyekuwa akipendwa sana kupita wake wenzake wote, lakini hakupata bahati aliyoipata bibi Khadiyjah.

Hebu tumsikilize bibi ‘Aaishah mwenyewe (Radhwiya Allaahu anhaa) akituhadithia: Amesema (Radhwiya Allaahu anhaa):

“Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa daima akimtaja Khadiyjah, na siku moja alikuja kututembelea Haalah dada yake Khadiyjah nyumbani kwetu Madiunah, na sauti yake ilikuwa imefanana sana na sauti ya Khadiyjah, na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipoisikia tu sauti yake akasema:

“Allahumma huyu ni Haalah dada yake Khadiyjah mfungulie mlango upesi”.

Anasema bibi ‘Aaishah:

“Nilimuonea wivu Khadiyjah nikasema kumwambia Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

“Nakuona unampenda sana Khadiyjah, huachi kumtaja kila siku kama kwamba hapana mwanamke mwengine duniani isipokuwa yeye. Khadiyjah hakuwa na chochote cha zaidi isipokuwa alikuwa mwanamke mzee, na Allaah Amekwishakupa aliye bora kuliko yeye”.

Anaendela kusema bibi ‘Aaishah;

“Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alinikiasirikia sana siku hiyo kwa kauli yangu ile akaniambia:

“Hapana wa-Allaahi! Hakunipa aliye bora kuliko yeye, kwani yeye aliniamini wakati watu waliponikadhibisha na akanisaidia kwa mali yake wakati watu waliponinyima, na kupitia kwake akaniruzuku watoto”.

Anasema bibi ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu anhaa):

“Nikajisemea moyoni mwangu; 'sitomsema tena vibaya Khadiyjah.”

 

Na katika hadithi nyingine anasema bibi ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu anhaa):

“Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa anapochinja mbuzi daima akipeleka nyama kwa marafiki wa Khadiyjah, na siku moja nilimuuliza kwa nini anafanya hivyo, akanijibu:

“Mimi nawapenda wote alokuwa akiwapenda”.

 

Bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) alikuwa wa mwanzo kupita wote kumuamini Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na wa mwanzo kusilimu miongoni mwa wanawake na wanaume, na wa mwanzo kuswali nyuma ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wakiwa peke yao nyumbani.

 

Alikuwa mara nyingi akimliwaza na kumtuliza Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anapodhikika au anapoadhibishwa au kukadhibishwa au kutukanwa au anapopata mateso ya aina yoyote kutoka kwa makafiri wa Makkah.

 

 

 

Mafunzo

 

1- Mtu asivunjike moyo hata kama ana tumaini dogo namna gani, kwani bibi Khadiyjah (Radhwiya Allaahu anhaa) aliliona tumaini ndani ya Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) pale alipokuwa akizihesabu sifa zake tukufu moja baada ya nyingine, akiwa na tumaini kuwa mtu huyu ndiye atakayekuwa Nabiy anayesubiriwa, juu ya kuwa hizo zilikuwa ni fikra njema tu, lakini hatimaye zikageuka kuwa ukweli halisi.

 

Alipotamani kuolewa naye, aliliona tumaini lake kuwa mfano wa ndoto, lakini hakuiacha iwe ndoto, bali alizindukana na kuifuatilia ndoto hiyo mpaka ikageuka kuwa kweli.

 

2- Mwenendo wa makafiri wa kuwazunguka Waislaam na kuwapiga pande na kuwafanyia vikwazo vya kiuchumi na vya kibiashara na kuwaacha wakiwa na njaa wakidhani kuwa mwisho wake watakuja kuwapigia magoti. Darsi hii inatufundisha kuwa mila za kikafiri ni namna moja tokea wakati wa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mpaka wakati wetu huu.

 

3- Mstahamilivu hula mbivu. Waislaam walistahamili kila aina ya tabu na adhabu, mateso na uadui uliokuja kutoka sehemu mbali mbali za ulimwengu tokea siku ya mwanzo, lakini ustahamilivu wao huo haukupotea bure, kwani hatimaye waliweza kupata dola yao na kupambana na adui zao waliokuja kuwapiga vita kutoka kila pembe ya dunia na kupata ushindi wa nyumba mbili. Nyumba ya dunia na nyumba ya Aakhirah.

 

 

Share