004-Hakimu Wa Kiislamu: Taratibu Za Utendaji Katika Kukusanya Kitabu Hiki

 

TARATIBU ZA UTENDAJI KATIKA

KUKIKUSANYA KITABU HICHI

 

 

Ni jambo linaloeleweka ya kwamba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Ameziweka kanuni za ulimwengu huu katika aina mbili. Aina ya mwanzo ni ile ambayo Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Ndiye Mwendeshaji wa kila kitu, kwa mfano mwenendo wa jua na mwezi. Aina ya pili ni ile ambayo mwanaadamu anahitajika kuzifuata kanuni Alizowekewa na Muumba wake. Hizi nazo pia zimegawika sehemu mbili. Sehemu ya mwanzo ni kanuni ambazo Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Amekwisha zitolea hukumu, kwa mfano taratibu za uendeshaji wa makosa ya jinai kama vile zinaa na ulevi. Sehemu ya pili ni zile ambazo Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Ameziwacha wazi kwa wanaadamu kuzitolea ufafanuzi kwa kutumia vyanzo vya Qur-aan na Sunnah. Hapa ndipo tunapopata tawi la mwenendo wa kesi.

 

Qur-aan ni mwongozo wa Uislamu ikifafanuliwa vyema kwa kutumia Sunnah ya Habibul-Mustafa (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Kwa kutumia Sunnah hii ndipo tunapata fursa ya kutolea fafanuzi baadhi ya vifungu vya Shari’ah ya Kiislamu. Wanavyuoni kwa kupitia vikao vyao Shuura na mamlaka ya Shari’ah ndogo za Kiislamu pia wameweza kutumia fursa zao katika kutolea maelezo mwenendo huu wa kesi.

 

Mwenendo wa kesi ni ule utaratibu wa kushughulikia migogoro. Katika kitabu chetu hichi tumetumia zaidi kesi baina ya wanaadamu wenyewe sio yale makosa ambayo Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Amekwishayatolea maamuzi kama vile zinaa na ulevi. Ingawa kwa upande fulani mifano ya huduud (jinai zenye hukumu zake) imeelezewa ili kupata ladha baina ya jinai na madai pamoja na kuweka wazi hoja kwa lengo la kueleweka vyema.

 

Kazi ya kukusanya vyanzo vya Shari’ah sio kazi nyepesi hata kidogo. Ikikumbukwa kwamba Uislamu unaruhusu kanuni zake kufafanuliwa kupitia vyanzo vikuu vya Shari’ah ambavyo ni Qur-aan na Sunnah. Halikadhalika ni dhambi kubwa kumzulia Muumba maelezo ambayo Hajayatoa na vivyo hivyo kwa Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Kazi hii ya kukusanya Shari’ah hizi tunaifanya baina ya hadhari mbili kama zilivyoelezwa ndani ya Qur-aan:

 

{{Hiyo ni mipaka ya Mwenyezi Mungu. Na anayemtii Mwenyezi Mungu na Mtume Wake, (Mwenyezi Mungu) Atamwingiza katika Bustani zipitazo mito mbele yake; wakae humo milele. Na huko ndiko kufaulu kukubwa.}} [Suratun-Nisaa: 13]

 

Aayah hiyo ya juu inatuhimiza kumtwii Mwenyezi Mungu na Mtume Wake. Utiifu huu ndio unatupelekea kuchambua maelezo ya Shari’ah ili kupata muongozo ulio adilifu usioendana na dhulma. Kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) na Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwa pamoja wameiharamisha dhulma.

 

Lakini Aayah inayofuatia ya Suratun-Nisaa inaeleza kwamba mwenye kumuasi Yeye Muumba pamoja na Mtume Wake basi wajitayarishie makaazi ya Motoni:

 

{{Na anayemwasi Mwenyezi Mungu na Mtume Wake, na kuiruka mipaka Yake, (Mwenyezi Mungu) Atamwingiza Motoni, huko atakaa milele, na atapata adhabu zifedheheshazo.}} [Suratun-Nisaa: 14]

 

Kumzulia vifungu vya Shari’ah Muumba na Mtume Wake ni dhambi kubwa mbele ya Mola Mlezi na ni uasi mbaya dhidi ya Uislamu. Malipo yake ndio huo Moto ufedheheshao. Ni kusema kwamba, uangalifu wa hali ya juu unahitajika katika kutoa maelezo ya masuala ya Shari’ah ya Kiislamu. Kwani kutojali mipaka ya Mola Mlezi katika ufafanuzi huu kutasababisha Muislamu kuporomoka katika uasi.

 

Inaeleweka pia kwamba mwenye kumuongoza Muislamu mwenziwe katika khayr atapata naye malipo sawa sawa na yule mwenye kuifanya hiyo khayra, na mwenye kumuongoza mtu katika upotovu naye atapata malipo sawa. Hivyo, tumechukua jukumu kubwa la kuutolea ufafanuzi Ummah wa Kiislamu haswa kwa wazungumzaji wa Kiswahili. Lakini, tutakuwa mas-uul iwapo kitabu hichi kitakuwa ni sababu ya Waislamu kupotea (Allaah Atulinde na kuangamia huku). Na iwapo itabainika mbele ya Mahkama ya Mola wa Mbingu na Ardhi kwamba kitabu hichi kimepoteza zaidi kuliko kuongoza basi adhabu kubwa itatuwajibikia juu yetu. Hakika hizi kazi sio katika masuala ya kuyavamia na kuyachezea hata kidogo!

 

Juu ya yote hayo, Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anamlipa mja wake kutokana na niyah. Wala hakuna kitu muhimu anachohitajika Muislamu kukichunga kama niyah yake kama alivyosema Abu Sufyaan bin Sa'iyd ath-Thawriy (Rahimahu Allaahu):

 

((Hakuna kitu ninachojishughulisha nacho zaidi kuliko niyah yangu.))[1]

 

Hivyo tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kupitia nia zetu za khayr kujaalia kazi hii ni miongoni mwa zitakazofanya mizani ya ‘amali njema kupanda juu.

 

Upotevu mkubwa uliowakumba Waislamu wa leo ni kutokana na kuacha mafunzo sahihi ya Kiislamu. Walianza kudharau fardhi ya elimu wakatumbukia katika udhalilifu wa hali ya juu. Waislamu wakajikuta hawaelewi baina ya mwenendo wa Kiislamu na ule usio kuwa wa Kiislamu. Hata migogoro yao imekuwa ikisimamiwa katika taratibu zilizo nje ya Uislamu.

 

Tunaamini kwamba, iwapo Muislamu atasoma kwa ajili ya Allaah na kuelewa vyema mafunzo ya Shari’ah za Kiislamu atakuwa mbali katika kumuasi Mola wake. Na iwapo atateleza basi Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa Rahmah Zake Atamuongoza katika uongofu.

 

Inakuwa ni jambo la kusikitisha kwa mtu aliyebobea katika fani ya Shari’ah anapomuona mtu akikosa haki yake kwa kukosa tu kufuata taratibu sahihi za kufungua kesi. Hili katika Uislamu laweza kuepukwa, lakini kwa masikitiko makubwa hizi ni njia ambazo weledi wa Shari’ah wamekuwa wakizitumia. Na ndio sababu ya Waislamu kukosa haki zao za msingi.

 

Waislamu haiwaisaidii kukaa kitako na kutosimamia haki zao kwa hoja ya kwamba Mahkama za leo sio za Kiislamu. Ni kupitia Mahkama hizi hizi twaweza kwa kutumia hizo hizo Sheria walizoziweka wanaadamu kuweza kujitetea. Kujitetea huku kunawezekana kusiwe na mafanikio lakini dhimma mbele ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) itakuwa imepunguwa kwa kiwango kikubwa. Tukielewa kwamba ndani kabisa katika vifungu vya Sheria alivyovitunga mwanaadamu ni vyenye kudai haki na uadilifu. Hivi ndivyo vifungu ambavyo vitatumika kudai haki zetu. Kinyume cha vifungu hivi, ni vile visivyoendana kabisa na Uislamu, basi hivyo vitakataliwa na kutosimamiwa.

 

Ni kawaida ya kesi kufunguliwa baada ya kutokezea mgogoro. Ndipo hapa ambapo Muislamu anatakiwa aelewe nini na wapi anakwenda kukidai. Baadaye utafuata utaratibu wa kulisikiliza dai na kutolea ushahidi. Hatimaye hukumu itatolewa na upande usioridhika kupatiwa haki ya rufaa. Hizi ni taratibu ambazo kitabu hichi kimejitahidi kuyatolea ufafanuzi.

 

Utaratibu uliotumika katika kukikusanya kitabu hichi ni kuchukua fafanuzi na maelezo kutoka Shari’ah na baadaye kuyatafutia kulingana kwake na Sheria za nchi. Shari’ah kwa hapa tunakusudia zile za Kiislamu wakati Sheria ni hizi azitungazo mwanaadamu.

 

Halikadhalika, Sheria sio zile tu zilizopitishwa na Bunge ama Baraza la Wawakilishi. Bali pia zinaambatana na hukumu zinazotolewa na Mahakimu. Hivyo, iwapo Hakimu aliwahi kutoa hukumu hapo kabla, ikitokea tena kesi kama hiyo kwa pande (za watu) zilizo tofauti anahitajika kutumia uzoefu wa hukumu ile ile iliyopita. Hivyo, kitabu hiki kimekusanya hukumu za kesi tofauti zilizowahi kusomwa hapa Afrika Mashariki, Uingereza na pia India.

 

Kitabu hiki kimetoa maelezo pia kwa Hakimu. Kwa mfano uteuzi na wajibu wake katika misingi ya Uislamu. Kwa upande wa Zanzibar, kuna kanuni na muongozo maalum unaohitajika kufuatwa na Mahakimu pamoja na wafanyakazi wengine wa Mahkama. Anahitajika kutojishirikisha katika rushwa wala kupendelea upande mmoja. Namna anavyohitajika kuwa ni mambo mengi. Wajibu wa kufuata muongozo huu umo ndani ya Sheria ya Tume ya Uajiri ya Mahkama ya mwaka 2003 ya Zanzibar.

 

Ili kukifanya kitabu kuwa na maelezo mafupi yenye maelezo ya kina, imebidi kutumia vifupisho vya maneno. Mfano wa vifupisho vilivyotumika ni kama ifuatavyo:

 

 

KIINGEREZA:

 

 

KIFUPISHO

KIREFU

MAANA

 

Cr.

 

Criminal

Jinai

E. A.

 

East Africa

Afrika Mashariki

E. A. C. A.

 

East African Court of Appeal

Mahkama ya Rufaa ya Afrika Mashariki

 

O.

Order

Kanuni

 

r.

Rule

Amri

 

R.

Republic

Jamhuri

 

S.

Section

Kifungu

 

V.

Versus

Dhidi ya

 

 

 

KISWAHILI:

 

 

KIFUPISHO

KIREFU

 

J.

Juzuu

 

uk.

Ukurasa

 

 

 

Halikadhalika, kwa lengo la kurahisisha marejeo pamoja na kutoa fafanuzi katika vipengele tofauti, kitabu hiki tumekigawa katika sura mbali mbali. Maelezo ya sura hizi ni kama zifuatazo:

 

Sura Ya Kwanza imesawazisha kwa kutolea fafanuzi za baadhi ya maneno muhimu na yaliyotumika sana ndani ya kitabu hiki. Bila ya shaka msomaji anaweza kukutana na maneno asiyoyaelewa maana yake kutokana na kitabu hiki kujikita katika mambo ya Shari’ah na Sheria kwa pamoja.

 

Sura Ya Pili ya kitabu hiki ndio imeanza kuingia rasmi katika mambo ya kesi kwa kutolea maelezo ya namna ya kufungua kesi na nani anastahiki kufungua kesi.

 

Sura Ya Tatu inaeleza kuhusu hati. Hizi ni zile hati (summons) anazopatiwa mtu na kuwajibika kufika Mahkamani katika tarehe iliyopangwa na wakati utakaoelezwa ndani ya hati hizo.

 

Sura Ya Nne inafafanua namna ya kusikiliza kesi. Hii ndio sura inayoeleza wapi Mahkama inaweza kukaa, wajibu wa hakimu kusikiliza maelezo ya pande zote za kesi, hatma ya yule anayekataa kujibu na namna gani ya kushugulikia kesi ambayo upande mmoja umekubali kushindwa, na imemalizia sura hii kwa kutoa maelezo ya kuakhirisha kesi.

 

Sura Ya Tano imekusanya maelezo ya ushahidi katika kesi. Sura hii imeanza kwa kutolea ufafanuzi wa dhana ya ushahidi, baadaye imeendelea na kufafanua kuhusu kiapo na nani anawajibika kuapa na nani anawajibika kuthibitisha malalamiko yake. Katika kesi kunawezekana kukakuwepo na mtaalamu wa masuala fulani, hili limeelezwa ndani ya sura hii pia. Sura ya tano imeangalia namna ya kumfahamu shahidi anayeletwa mbali, huu ni ufahamu wa khulqa zake na namna ya utoaji ushahidi wake. Ama maelezo mengine muhimu katika sura hii ni kuhusu ushahidi wa kimazingira na kutengua ushahidi wa mwenye kujirudi. Sura hii ya tano inamalizia na maelezo kuhusu namna na wakati gani wa kutoa tafsiri.

 

Sura Ya Sita kwa upande wake imetengwa kwa kutolea maelezo ya hukumu. Haya ni maelezo kuhusu namna ya kuitayarisha hukumu, namna ya kuisoma. Kwa kile kinachofuata baada ya kusomwa hukumu ni kikaza hukumu, rufaa, mapitio na marejeo. Hakimu amepewa mamlaka ya kutoa mawazo yake binafsi, hili limewekwa ndani ya sura hii ya sita. Suluhu ni katika njia nyepesi na salama ya kumaliza kesi. Hivyo, kitabu hiki hakijaacha kufafanua suluhu ndani ya sura hii. Maelezo mengine ni ushauri wa wanazuoni na kizuizi cha kufungua kesi kutokana na kupita muda mrefu.

 

Sura Ya Saba inaeleza kuhusu wafanyakazi wa mahkama, hawa ni wale makarani, wataalamu, wafasiri na wengineo.

 

Sura Ya Nane ambayo ni ya mwisho inamalizia na hitimisho.

 

Kwa mtiririko wa sura hizi pamoja na maelezo yake, tunatumai kwamba itaeleweka kiasi fulani kuhusu utendaji wa kazi hii na maelezo tuliyoyagusia mwanzoni katika kuwa makini pamoja na kuichunga niyah.



[1] Shaykh Bakr bin 'AbdiLlaah Abu Zayd, Sharhu Hilyat Twaalib al-'Ilmi, Iliyoshereheshwa na Shaykh Muhammad bin Swaalih al-'Uthaymiyn, Chapa ya Daaru Ibnul Haytham, Misri, (2002).

Share