Mwanamke Mwenye Kupata Hedhi Akiwa Katika Hajj Afanye Nini?

 

Mwanamke Mwenye Kupata Hedhi Akiwa Katika Hajj Afanye Nini?

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Assallam allaikum warahmatullah wabarakatuh,

 

Ndungu wahusika, sina shaka email hii itawafika katika hali nzuri na afya njema.  Baada ya salam ningeomba . kuuliza swali juu ya ibada ya Hijja.

 

 

1. Je Mwanamke anapokuwa katika ibada ya hijja kwa bahati nzuri au mbaya mwanamke huyu akapata period yake wakati akitekeleza ibada hii

 

(a) Je anatakiwa aendelee na ibada hii au akatishe? kwani tunavyofahamu ndungu zetu hawa wanapokuwa kwenye hali hii hawaruhusiwi kusali bali wanaweza kufanya ibada nyenginezo kama kumtaka Allaah na ibada nyenginezo! please nifafanulize saidi... 

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Mwanamke mwenye kwenda Makkah kwa nia ya kutimiza fardhi ya Hijja, akapata hedhi yake, anatakiwa aendelee na ibada zote nyingine wanazofanya mahujaji isipokuwa kutufu Ka’abah ambayo ni sawa na Swalaah. Kwa hiyo ataacha pia kuswali kama ilivyo kawaida ya wanawake wanaopata hedhi kuwa wamezuilika kuswali na kufunga.

 

Dalili ni kutoka Hadiyth ifuatayo:

 

عن عائشة -رضي الله عنها- أن رسول الله -صلى الله عليه وسلم- دخل عليها وهي تبكي، فقال ((أنفست؟))"  (يعني: هل جاءتك الحيضة؟) فقالت: نعم، قال: ((إن هذا شيء كتبه الله على بنات آدم، فاقضي ما يقضي الحاج، غير ألا تطوفي بالبيت حتى تغتسل))" رواه البخاري ومسلم

Kutoka kwa bibi 'Aishah (Radhwiya Allahu 'anhaa) kwamba Nabiy (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliingia (katika hema lake) akamkuta analia akasema: ((Je umepata hedhi?)) akasema: "Ndio". Akasema: ((Hii ni amri Allah Aliyowaandikia wasichana wa Adam, fanya yote wanayofanya mahujaji isipokuwa kutufu Ka’abah hadi utoharike)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

 

Ibada nyingine zote zinazofanyika katika msimu wa Hajj ni zifuatazo:

 

- Kufanya Sa'ay (Kutembea Asw-Swafaa na Al-Marwa) mara saba.

- Kwenda Minaa kulala huko kwa ajili ya kutimiza nguzo nyingine.

- Kusimama 'Arafah

- Kulala Muzdalifah

- Kufanya jamaraat (kupiga mawe nguzo)

- Kuchinja

 

Na katika nyakati hizo zote anaruhusiwa kufanya dhikr za aina yoyote kama kuomba du'aa, kusoma Qur-aan, kusoma vitabu vya Dini, kufanya dhikr za tasbiyh (Subhaana Allaah) tahliyl (Laa ilaah Illa Allaah) tahmiyd (AlhamduliLLaah, takbiyr (Allaahu Akbar) na aina yoyote nyingine zilizothibitika katika Sunnah.

 

Atakapomaliza hedhi yake akakoga josho (ghuslu) atakwenda kufanya Twawaaf alizoshindwa kuzifanya, ikiwa ni Twawaaf ya 'Umrah au Twawaaf ya Ifaadhwah.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share