Zakaah Ya Dhahabu Kiasi Gani?

Zakaah Ya Dhahabu Kiasi Gani?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

SWALI:

 

A/alleykum.

Naomba nifafanuliwe zaidi kuhusu zaka ya dhahabu. Mfano mimi nina dhahabu gramu 100, jee natakiwa nitoe zaka shilingi Ngapi za Tanzania?

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Kwanza tafadhali bonyea viungo vifuatavyo upate kutambua haramisho la kufupisha Maamkizi ya Kiislamu na mengineyo:

Hukmu Ya Kufupisha Thanaa (Kumtukuza Allaah) Na Kumswalia Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) Na Maamkizi Ya Kiislam

 

Ama kuhusu Swali lako, inafaa sisi tufahamu masharti ya kutoa Zakaah ikiwa ni pesa taslimu, dhahabu au fedha au vito vyengine vya thamani. Miongoni mwa masharti haya ni:

 

1-Niswaab: Hiki ni kiwango cha chini ambacho mtu akiwa nacho ni lazima atoe Zakaah ya 2.5%. Ama kwa dhahabu ni gramu 82.5.

 

2-Hawl: Kupitiwa hiyo dhahabu na mwaka mzima wa Hijriy (mwandamo).  

 

Haya ni masharti ya msingi katika mas-ala hayo ya Zakaah.

 

Tukichukua mfano uliotoa ya kwamba una gramu mia za dhahabu. Kiwango hichi kikipitiwa na mwaka itabidi utoe 2.5%. Asilimia hiyo itakuwa ni sawa na kiwango cha gramu 2.5 ya dhahabu. Upo msemo unaosema kuwa watu wa Makkah wanajua vilivyo kwa watu wao. Nawe ikiwa ni mkaazi wa Tanzania au Kenya utajua maduka ya masonara. Kwa hiyo kabla ya kutoa Zakaah zako unafaa uende ukawaulize gramu moja ya dhahabu ni shilingi ngapi. Ikiwa gramu moja ni 20,000 itabidi baada ya mwaka utoe shilingi 50,000.

Ni bora zaidi kwa kuwa hela hii ni ndogo umpatie anayestahiki mmoja wa kupewa Zakaah ili imsaidie kwa kiasi kikubwa zaidi, kuliko kuigawa na kuwapa wengi kidogo kidogo. Watu wanaofaa kupewa Zakaah wametajwa katika kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

((إِنَّمَا الصَّدَقَاتُ لِلْفُقَرَاءِ وَالْمَسَاكِينِ وَالْعَامِلِينَ عَلَيْهَا وَالْمُؤَلَّفَةِ قُلُوبُهُمْ وَفِي الرِّقَابِ وَالْغَارِمِينَ وَفِي سَبِيلِ اللَّـهِ وَابْنِ السَّبِيلِ ۖ فَرِيضَةً مِّنَ اللَّـهِ ۗ وَاللَّـهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ))

((Hakika Zakaah ni kwa ajili ya mafakiri na masikini na wanaozitumikia, na wanaotiwa nguvu nyoyo zao (katika Uislamu) na kuwakomboa mateka, na wenye deni na katika Njia ya Allaah na msafiri (aliyeharibikiwa). Ni faradhi itokayo kwa Allaah. Na Allaah ni Mjuzi wa yote, Mwenye hikmah wa yote)). [At-Tawbah (9:60)]

 

Kwa faida ziyada, bonyeza viungo vifuatavyo:

08-Swahiyh Fiqh As-Sunnah: Mlango Wa Zakaah: Zakaah Ya Dhahabu Na Fedha (Silver)

019-Kutoa Zakaah: Dhahabu Na Fedha

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share