Nimemdanganya Mume Wangu, Je, Nimeachika? Na Je, Inanipasa Nikae Eda?

 

SWALI:

Bibi na Bwana wameelewana kutumia koil kukinga kupata mtoto kwa mda. Kisha bwana ameamua koil bibi akaitowe. Bibi akamwambia bwana haya. Ikapita mdaa. Bwana akamuuliza bibi kama ile koil ameitoa? Bibi akadaganya mumewe kwamba koil kesha itowa. Baadae siku kadha bwana akamwambia bibi nafikiri kua koil hujaitoa umenidaganya. Na kama umenidaganya jua nishakuwacha. Bibi ana watoto watatu. WA miaka mitatu, na miwili na mmoja. Kazi ya ulezi pekee yake. Sababu bwana anafanya kazi kuazia jumatatu hadi ijumaa.   Swala langu ni, jee huyu mwanake kishawachika? Swala la pili kwa kua anahakika kua anatumia koil kutokupata mimba jee. Jee akiachika anakaa edaa? Insha’Allah nitapata majibu ya kuniridhisha. Asalaam aleikum.

 


 

JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allah Aliyetukuka Mola  wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu  'alayhi wa aalihi wa sallam), ahli zake, Swahaba zake (Radhiya Allahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

Shukran ndugu yetu kwa swali lako hilo na kwa hakika haya maswali ya talaka ni mengi na ni nyeti. Kama tulivyokariri mara kadhaa ya kwamba katika halali inayochukiza sana mbele ya Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) ni talaka. Hivyo, tunawanasihi wanaume wasiwe ni wenye kufanya haraka au mzaha au kuegemeza masharti au sharti katika mas-ala hayo ya talaka. Kwani Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anatuelezea umuhimu wa kukaa na wake zetu vizuri kama Alivyosema:

Na kaeni nao kwa wema, na ikiwa mmewachukia, basi huenda mkakichukia kitu, na Allaah Ametia kheri nyingi ndani yake” ().

 

Talaka amepatiwa mume kwa ajili ya utulivu wake na kuweza kusubiri na kuzingatia kabla ya kuchukua hatua yoyote kama hiyo ambayo inaathiri familia na kizazi kijacho. Inabidi mume apatiwe ushauri nasaha katika jambo la kuishi kwa wema na mkewe la sivyo basi matatizo haya yataendelea kuwepo, nyumba kama hiyo itavunjika hivyo kuwaletea matatizo watoto walioruzukiwa.

Inatakiwa kwamba mume na mke wanapopeana ahadi iwe kila mmoja afanye juhudi kutekeleza upande wake na kama panakuwa na matatizo ni lazima warudi tena katika meza na kushauriana na kufikia suluhisho muafaka. Talaka katika hilo lililopitika katika suala la mume na mke halikuwa ni suluhisho na inatakiwa mume aangalie maslahi ya mke ili kusiwe na matatizo.

Uongo katika Uislamu ni mbaya na ni miongoni mwa sifa za unafiki kwa mwenye kulifanya hilo. Na ni kosa ambalo Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema kuwa Muumini hawezi kuwa ana sifa hiyo japokuwa anaweza akafanya kosa jengine. Kwa kosa hilo anatakiwa mke aombe msamaha kwa Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) na atubie Kwake na asirudie tena kosa hilo na Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasamehe madhambi yote. Lakini mbali na kusema hayo swali la talaka katika hili suala lako bado limebakia pale pale na hili haliwezi kuondolewa kwake yeye kutubia.

Kama ulivyoashiria katika swali lako kuwa tayari mume amempatia talaka ya sharti na hivyo hiyo ni talaka moja tu ambayo bado ina fursa ya wao wawili kurudiana.

Katika talaka hii ambayo imetolewa na mume ni kuwa imeekewa sharti – “Bwana akamuuliza bibi kama ile koil ameitoa? Bibi akadaganya mumewe kwamba koil kesha itowa. Baadae siku kadha bwana akamwambia bibi nafikiri kua koil hujaitoa umenidaganya. Na kama umenidaganya jua nishakuwacha”. Hapa tunapata sharti moja:

1.       Ikiwa umenidanya jua nishakuacha.

Kwa muhtasari ni kuwa mke keshaachika na inabidi akae eda yake ya tohara tatu ambayo ni takriban miezi mitatu kufuata miandamo ya mwezi. Katika kipindi hiki cha eda, mume ikiwa hiyo ni talaka ya kwanza au ya pili anaweza kumrudia mkewe lakini ni nasaha yetu kuwa mtu au watu wenye uzoefu wazungumze na huyu bwana ili asiwe ni mwenye kuweka masharti kama hayo bali wawe ni wenye kushauriana na mkewe pindi anapoona kuna haja ya jambo fulani kufanyika katika njia fulani. Na pia mke anasihiwe asiwe ni mwenye kudanganya bali awe wazi kwa mumewe ili matatizo kama hayo yasiwe ni yenye kutokea tena katika maisha yao ya unyumba.

Tunamuomba Allah (Subhaanahu wa Ta'ala) Awape maelewano na masikilizano ili watu hao wawili warudi katika hayo yao ya awali kama mume na mke, na pia Awape hamu ya kushauriana katika mas-ala yote nyeti ili matatizo hayo yasiwe ni yenye kutokea tena.

 

Na Allaah Anajua zaidi.

 

 

Share