Mume Asi Hatimizi Fardhi

SWALI:

ASSALAMU ALAIKUM

 

Je nifanye aje? Mume wangu hatowe zaka, kila siku kutowa zaka ni kusema  kumukumbusha, kusali  taraweh awo kiyamu layli ni kusema, wala hafanyi, kusali swalatul subhi ni bigumu sana , natoka kitandani kusali analala anasali saa yoyote anaamuka, natiya alarm kwa kuamuka kusali  anatowa,roho yangu inaumwa sana kwa vitendo viake, akifanya kosa lolote namu uliza, ananijibu kwamba amelifanya kwa ju ya wangine (marafiki) , uzinifu na bingine byo, roho yangu basi sisahawi kila kitu kibaya alicho nitendeya kwaju anakuwa ataongeza I don't trust him any more.Anataka afuate  ideas zake tu zangu hataki.na  ni older than me 11 years.NIKISEMA KIDOGO TU ANATOMBOKA SANA without respect watoto wanasikiya. Je twiko katika mwezi mutukufu wa ramazani, nahitaji naama yenu (advises). KWANGU NA KWAKE.
ASSALAU ALAIKUMU

 


JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Shukrani nyingi kutoka kwetu kwa dada yetu na tunaomba samahani sana kwa kuchelewa kukujibu swali lako na pia tunashukuru kwa kujitahidi kujieleza kwa lugha ya Kiswahili kadiri ulivyojaaliwa. Tunasikitika sana kusikia yanayokukumba katika maisha yako ya unyumba. Juu ya yote hayo inatakiwa tufahamu kuwa baada ya dhiki ni faraja. Anasema Allaah Aliyetukuka: “Basi kwa hakika pamoja na uzito upo wepesi” [94: 5]. 

Tatizo hili mara nyingi linatokea kwetu wengi na pia kwa kwa sababu mara nyingi huenda hatukuoana kwa misingi ya Kidini. Huenda kuwa tumekutana au kuoanana sehemu na hapo hapo kupendana kwa misingi ya uzuri, kabila, nasaba, hadhi, cheo, mali, na kadhalika. Lakini hebu tusikilize nasiha ya Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kuhusu mas-ala hayo ya ndoa pale aliposema: “Mwanamke huolewa kwa mojawapo ya sababu NNE: Mali yake, uzuri wake, cheo (nasaba) chake au Dini yake. Chagua mwenye Dini usije kupata khasara” (Al-Bukhaariy). Pia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amewausia wanawake wachague mume mwenye Dini na maadili mema.

Kwa ajili ya misingi hii ya kuchaguana ndio tunakumbana na haya matatizo. Ni nasiha kwa ndugu na dada zetu wachukue nasiha hizi kwa umakinifu katika kutekeleza wajibu huu muhimu wa ndoa ili tusije kujuta baadaye.

Nasiha ambayo tunaweza kumpatia dada yetu na wengine wenye matatizo kama yake ni kufuata kwao muongozo wa Kiislamu ili kutatua migogoro. Mgogoro huu ni mkubwa sana hasa ikizingatiwa kuwa mume ametoka katika muongozo wa Kiislamu na hatekelezi amali nyingi za msingi na nguzo za Uislamu ambazo zinamtoa mtu katika Imani na Uislamu kama Swalah na Zakah. Inabidi dada yetu uchukue jukumu la kuweza kuwasiliana na Imamu au Shaykh aliye karibu nawe ili aje kuzungumza na kumpatia mawaidha na nasiha mumeo, huenda kwa kufanya hivyo akajirudi na kutubia kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala).

Lau hukufanikiwa katika njia hiyo basi itabidi uitishe mkutano au kikao baina ya wazazi wako, wazazi wake, wewe mwenyewe na mumeo. Hapo inatakiwa uweke wazi na bayana kabisa yote yale anayofanya au kukufanyia. Ikiwa watu wote hao watakuja na kuangalia tatizo kwa ikhlasi na kutaka suluhu basi Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ameahidi kuwa suluhu itapatikana katika kikao hicho. Lau hakutapatikana uamuzi wowote au kushindwa kuafikiana kwa sababu ya ukosefu wa ikhlasi na yeye mwenyewe hataki kubadilika na mienendo yake miovu, hapo itabidi uende ukashitaki kwa Qadhi, ikiwa yupo katika mji unaoishi. Ikiwa hayupo basi nenda kwa Shaykh aliyewafungisha ndoa yenu au Shaykh mwengine yeyote muadilifu ili aisikilize kesi yenu na hapo akupatie ‘Faskh Nikaah’ (kuachishwa na mumeo).

Hili ndio nasaha ambazo tunaweza kukupa na ndio suluhisho kwako baada ya juhudi zote hizo ambazo utakuwa umezifanya. Na jambo hili litakuwa kheri kwako na kwa dini yako. Hiyo ni kuwa ikiwa hataki kubadilika kimaadili na kukiwa kukaa naye huenda kukasababisha akakushawishi au ukashawishika kumfuata katika mwenendo wake huo, na kukuharibia dini yako ambayo ndiyo njia ya kukupatia pepo yako, basi ni bora kuwa mbali naye kwa kuihifadhi dini yako. Haina maana kuwa ni jambo zuri kukimbilia hatua hiyo ya kutengana, bali zitakaposhindikana njia zote hizo za kuleta kheri basi kutakuwa hakuna budi.

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Amuongoze mumeo na Amrudishe katika njia nyoofu. Hivyo hivyo, tunamuomba Akulinde wewe na upotofu wa aina yoyote na Akutatulie tatizo lako hilo na mambo yako mengine kwani Yeye ni Muweza wa hayo yote.

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share