047-Swahiyh Fiqh As-Sunnah: Mlango Wa Twahara: Tatu: Kupaka Juu Ya Kinachofunika Kichwa

 

Swahiyh Fiqh As-Sunnah

 

Mlango Wa Twahara

 

047-Tatu: Kupaka Juu Ya Kinachofunika Kichwa

 

Alhidaaya.com

 

 

1- Kupaka Juu Ya Kilemba Katika Wudhuu

 

Inajuzu kupukusa juu ya kilemba – badala ya kupukusa kichwa – wakati wa kutawadha kwa hali yoyote. Na haya ni madhehebu ya Ahmad, Is-haaq, Abu Thawr, Al-Awzaa'iy, Ibn Hazm na Ibn Taymiyah. Nayo ni kauli ya Abu Bakr, 'Umar, Anas na Maswahaba wengineo (Radhwiya Allaahu ‘anhum). [Masaail Abuu Daawuud (8), Al-Mughniy (1/300), Al-Majuu'u (1/406), Al-Awsatw (1/468), Al-Muhalla (2/58) na Majmu'u Al-Fataawaa (21/184)].

 

Na bila shaka, hilo limethibiti toka kwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

Imepokelewa toka kwa 'Amri bin Umayyah Adh-Dhumariy akisema: "Nilimwona Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akipukusa juu ya khufu mbili na kilemba". [Hadiyth Swahiyh: Imefanyiwa “ikhraaji” na Al-Bukhaariy (205)].

 

Kauli kama hiyo hiyo imepokelewa toka kwa Al-Mughiyrah bin Shu'ubah. [Hadiyth Swahiyh: Imefanyiwa “ikhraaji” na Al-Muslim (275)].

 

Pia imepokelewa toka kwa Bilaal akisema: "Nilimwona Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akipukusa juu ya khufu mbili na khimaar”.[Hadiyth Swahiyh: Imefanyiwa “ikhraaji” na Muslim (285)].

 

Khimaar hapa ni kile chenye kufunika kichwa, na makusudio ni kilemba.

 

Na kwa upande mwingine, Abuu Haniyfah na wenziwe, Maalik na Ash-Shaafi'iy, wameelekea kwingine wakisema kuwa mwenye kutawadha hapukusi juu ya kilemba tu, bali hupukusa juu yake pamoja na utosi, na utosi unakuwa ni fardhi na kilemba ni Sunnah (ziada) kwa kujengea juu ya kujuzisha kwao kupaka sehemu tu ya kichwa!! [Haashiyat Ibn 'Aabidiyn (1/181), Haashiyat Ad-Dusuwqiy (1/164) na Al-Majmu'u (1/407)].

 

Lakini pamoja na hivyo, Ash-Shaafi'iy anasema: “Ikiwa Hadiyth ya kupukusa juu ya kilemba ni Swahiyh, basi hiyo ndiyo kauli yangu”. Na bila shaka yoyote Hadiyth hiyo ni Swahiyh, kwa hiyo ndiyo kauli yake.

 

Wenye kupinga kupukusa juu ya kilemba wametoa hoja kwa Hadiyth ya Jaabir bin ‘Abdillaah aliyesema: "Nilimwona Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akikivuta nyuma kilemba chake na akapukusa juu ya utosi wake". [Sikuipata na wala haipo katika kitabu chochote kati ya vitabu vya Hadiyth nilivyonavyo. Na Ibn Al-Mundhir ameitaja bila ya Isnaad (1/469)].

 

Sijaipata Sanad yoyote ya Hadiyth hii!!

 

Na kwa Hadiyth ya Al-Mughiyrah akisema kwamba Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipukusa juu ya kilemba chake, na juu ya utosi na khufu zake mbili". [Hadiyth Swahiyh: Imetajwa katika mlango wa wudhuu].

 

Ninasema: "Kauli yenye nguvu ni kuwa inajuzu kwa hali yoyote kupukusa juu ya kilemba kwa kuthibiti kuelezewa hilo toka kwa Rasuli (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), na kwa kufanywa hilo na Makhalifa wawili waliokuja baada yake, na kukosa uzito hoja iliyotolewa na wenye kulipinga hilo. [Angalia hoja zao na zilivyojibiwa katika "Al-Muhalla" (2/61)]. Lakini pamoja na hivyo, ni bora kupukusa sehemu ya utosi pamoja na kilemba ili kuepuka mahitilafiano. Na Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.

 

2- Kupukusa Mwanamke Juu Ya Ushungi / Mtandio

 

Shaykh wa Uislam anasema: "Ikiwa mwanamke atahofia baridi au mfano wa baridi, basi atapukusa juu ya ushungi wake, kwani Ummu Salamah alikuwa akipukusa juu ya ushungi wake. Lakini akipukusa ushungi, anatakiwa apukuse baadhi ya nywele zake. Na ikiwa hakuhitajia hilo, basi hapa kuna mvutano baina ya Maulamaa.” [Majmu'u Al-Fataawaa (21/218)].

 

Ninasema: "Katika riwaya, [Al-Mudawwanah (1/42), Al-Ummu (1/26), Al-Badaai-'i (1/5) na Al-Mughniy (1/305)]…..Hanafiy, Maalik, Ash-Shaafi'iy na Hanbali, wameelekea mwelekeo wa kusema kuwa haijuzu kutokana na yale yaliyopokelewa toka kwa 'Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anha) kwamba yeye aliingiza mkono wake chini ya ushungi wake na akapukusa kichwa chake, akasema: "Hivi ndivyo alivyoniamuru Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)". [Sijapata kuiona bali ameitaja Al-Kaasaaniy katika Al-Badaai-'i (1/5), nami sijaiona katika kitabu chochote cha Hadiyth!!]

 

Wamesema: "Na kwa vile hicho ni kivazi cha kichwani kwa mwanamke na hakuna uzito katika kukiondosha, haijuzu kupukusa juu yake."

 

Al-Hasan Al-Baswriy amechukua msimamo wa kuwa inajuzu kupukusa juu ya ushungi. Hayo hayo wameyasema Mahanbal, - lakini wameshurutisha kuwa ni lazima mitandio au shungi ziwe zimezungushiwa chini ya koo!! – kwa kuchukulia kipimo cha kilemba, kwani khimaar kikawaida huvaliwa kichwani.

 

Ninasema: “Ingelikuwa Hadiyth ya 'Aaishah ni Swahiyh, basi ingelimaliza mjadala katika kuzuia kupukusa juu ya ushungi. Na kama si hivyo, basi kipimo kitachukuliwa juu ya kilemba. Na ili kuondosha wasiwasi, ni vyema mwanamke apukuse juu ya ushungi wake pamoja ncha ya utosi wake. Allaah Ndiye Ajuaye Zaidi.”

 

3- Kupukusa Juu Ya Kofia Katika Wudhuu

 

Jamhuri ya Maulamaa imeshikilia mwelekeo wa kuwa haijuzu wakati wa kutawadha kupukusa juu ya kofia badala ya kichwa, kwani fardhi ni kupukusa kichwa. Lakini hilo limeachiliwa katika kilemba kutokana na uzito wa kukivua kwa Jamhuri ya Maulamaa, au kwa matni ya Ahmad.

 

Ibn Hazm, Ibn Taymiyah na watafiti kati ya wadau wa taaluma hii, wameshikilia mwelekeo wa kujuzu kupukusa juu ya kofia.

[Al-Muhalla (2/58) na Majmu'u Al-Fataawaa (21/ 184-187, 214)].

 

Hii ni kwa vile, Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipopukusa juu ya kilemba, sisi tumejua kwa hilo kuwa si fardhi kugusanisha maji na kichwa, bali inajuzu kupukusa juu ya kitu chochote kilichovaliwa kichwani hata kama hakisitiri mahala pa lazima kuoshwa na wala haikuwa ni uzito kukivua. Na hili ndilo sawa, na Allaah Ndiye Ajuaye zaidi.

 

Faida

 

- Si Sharti Kuwa Na Twahara Wakati Wa Kuvaa Chenye Kufunika Kichwa Ili Ijuzu Kupukusa Juu Yake.

 

Hili halipimiwi na kupukusa juu ya khufu mbili, kwa vile hakuna sababu ya kuvikutanisha viwili hivyo, bali Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ameelezea ulazima wa twahara wakati wa kuvaa khufu mbili na wala hakulielezea hilo kwa upande wa kilemba na ushungi. Na lau kama ingelikuwa ni lazima, basi angelibainisha. [Al-Muhalla (2/64)]

 

Ninasema: “Hii ni kwa vile, khufu mbili ni badala ya kilicho fardhi kukiosha. Ama kichwa, fardhi yake ni kupukusa, na kilicho juu ya kichwa, huchukua hukmu yake. Kwa hiyo vimekuwa ni vitu viwili tofauti. Na Allaah Ndiye Ajuaye zaidi”.

 

- Hakuna Wakati Wala Muda Maalumu Wa Kupukusa Juu Ya Chenye Kufunika Kichwa

Ni kwa kutofaa kipimo cha kupukusa juu ya khufu mbili. Na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipukusa juu ya kilemba na khimaar na wala hakulipangia hilo wakati. Na hili limepokelewa toka kwa 'Umar bin Al-Khattwaab (Allah Amridhie). [Al-Muhalla (2/65)]

 

 

Share