11-Buluwgh Al-Maraam: Kitabu Cha Nikaah: Mlango Wa: Al-‘Iddah (Kukaa Eda) Na Al-Ihdaad (Matanga)

بُلُوغُ الْمَرام

Buluwgh Al-Maraam

 

كِتَابُ اَلنِّكَاحِ

Kitabu cha Nikaah (Ndoa)

 

 بَابُ اَلْعِدَّةِ وَالْإِحْدَادِ

11-Mlango Wa Al-‘Iddah (Kukaa Eda)[1] Na Al-Ihdaad (Matanga)[2]

 

 

 

 

 

944.

عَنْ اَلْمِسْوَرِ بْنِ مَخْرَمَةَ{ أَنَّ سُبَيْعَةَ الْأَسْلَمِيَّةَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا نُفِسَتْ بَعْدَ وَفَاةِ زَوْجِهَا بِلَيَالٍ، فَجَاءَتْ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ فَاسْتَأْذَنَتْهُ أَنْ تَنْكِحَ، فَأَذِنَ لَهَا، فَنَكَحَتْ} رَوَاهُ اَلْبُخَارِيُّ  وَأَصْلُهُ فِي " اَلصَّحِيحَيْنِ

وَفِي لَفْظٍ: {أَنَّهَا وَضَعَتْ بَعْدَ وَفَاةِ زَوْجِهَا بِأَرْبَعِينَ لَيْلَةً}

وَفِي لَفْظٍ لِمُسْلِمٍ، قَالَ اَلزُّهْرِيُّ: {وَلَا أَرَى بَأْسًا أَنْ تَزَوَّجَ وَهِيَ فِي دَمِهَا، غَيْرَ أَنَّهُ لَا يَقْرَبُهَا زَوْجُهَا حتَّى تَطْهُرَ}

Kutoka kwa Al-Mis-war bin Makhramah amesema kuwa Subay’a Al-Aslamiyyah[3] (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) alijifungua baada tu ya kufariki mumewe kwa siku chache, akamuendea Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akimuomba idhini aolewe, Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akamruhusu akaolewa.” [Imetolewa na Al-Bukhaariy na asili ya Hadiyth hii imo katika Swahiyh Al-Bukhaariy na Swahiyh Muslim]

 

Katika tamshi lingine: “…alijifungua baada ya mumewe kufariki kwa siku arubaini.”

 

Katika tamshi lingine la Muslim inasema: Az-Zuhriy[4] amesema: “Sioni kama pana ubaya akiolewa baada ya kujifungua hata kama yuko damuni (Nifaas), isipokuwa tu mumewe hawezi kumkaribia (kumjamii) mpaka atwahirike.”

 

 

 

945.

وَعَنْ عَائِشَةَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا قَالَتْ: {أُمِرَتْ بَرِيرَةُ أَنْ تَعْتَدَّ بِثَلَاثِ حِيَضٍ} رَوَاهُ اِبْنُ مَاجَهْ، وَرُوَاتُهُ ثِقَاتٌ، لَكِنَّهُ مَعْلُولٌ 

Kutoka kwa ‘Aaishah (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema: “Bariyrah aliamrishwa akae eda hedhi tatu.”[5] [Imetolewa na Ibn Maajah, Wapokezi wake ni madhubuti lakini ina ‘illah]

 

 

 

946.

وَعَنْ اَلشَّعْبِيِّ، عَنْ فَاطِمَةَ بِنْتِ قَيْسٍ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا، {عَنِ اَلنَّبِيِّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  فِي اَلْمُطَلَّقَةِ ثَلَاثًا: "لَيْسَ لَهَا سُكْنَى وَلَا نَفَقَةٌ"} رَوَاهُ مُسْلِمٌ 

Kutoka kwa Ash-Sha’biyy[6] kutoka kwa Faatwimah bint Qays (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema kuwa: Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema kuhusu mwanamke aliyeachwa talaka tatu: “Hana maskani wala chakula.”[7] [Imetolewa na Muslim]

 

 

 

947.

وَعَنْ أُمِّ عَطِيَّةَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا أَنَّ رَسُولَ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ:{لَا تَحِدَّ اِمْرَأَةٌ عَلَى مَيِّتٍ فَوْقَ ثَلَاثٍ إِلَّا عَلَى زَوْجٍ أَرْبَعَةَ أَشْهُرٍ وَعَشْرًا، وَلَا تَلْبَسْ ثَوْبًا مَصْبُوغًا، إِلَّا ثَوْبَ عَصْبٍ، وَلَا تَكْتَحِلْ، وَلَا تَمَسَّ طِيبًا، إِلَّا إِذَا طَهُرَتْ نُبْذَةً مِنْ قُسْطٍ أَوْ أَظْفَارٍ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ، وَهَذَا لَفْظُ مُسْلِمٍ  وَلِأَبِي دَاوُدَ، وَالنَّسَائِيِّ مِنْ اَلزِّيَادَةِ:{ وَلَا تَخْتَضِبْ}

وَلِلنَّسَائِيِّ: "وَلَا تَمْتَشِطْ" 

Kutoka kwa Ummi ‘Atwiyyah (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema kuwa Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mwanamke haombolezi maiti zaidi ya siku tatu, isipokuwa juu ya mumewe miezi minne na siku kumi.[8] Wala asivae nguo ya rangi isipokuwa nguo ya ‘aswbi,[9] wala asijipake wanja, wala asiguse manukato isipokuwa atakapotwahirika (atajipaka) kiasi kidogo tu cha Qustwi au adhwfaari.”[10] [Al-Bukhaariy, Muslim na tamshi hili ni la Muslim]

 

Katika Riwaayah ya Abuu Daawuwd na An-Nisaaiy amezidisha: “…wala asipake hina.”

 

Na kwa An-Nasaaiy: “…wala asijichane.”

 

 

 

948.

وَعَنْ أُمِّ سَلَمَةَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا قَالَتْ: {جَعَلْتُ عَلَى عَيْنِي صَبْرًا، بَعْدَ أَنْ تُوُفِّيَ أَبُو سَلَمَةَ، فَقَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  "إِنَّهُ يَشِبُ اَلْوَجْهَ، فَلَا تَجْعَلِيهِ إِلَّا بِاللَّيْلِ، وَانْزِعِيهِ بِالنَّهَارِ، وَلَا تَمْتَشِطِي بِالطِّيبِ، وَلَا بِالْحِنَّاءِ، فَإِنَّهُ خِضَابٌ". قُلْتُ: بِأَيِّ شَيْءٍ أَمْتَشِطُ ؟ قَالَ: "بِالسِّدْرِ"} رَوَاهُ أَبُو دَاوُدَ، وَالنَّسَائِيُّ، وَإِسْنَادُهُ حَسَنٌ 

Kutoka kwa Ummi Salamah (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema: Nilipaka swabira (aina ya dawa) machoni mwangu baada ya Abuu Salamah kufariki. Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akaniambia: “Hiyo hurembesha uso kwa hiyo jipake usiku, na mchana iondoe. Wala usijichane kwa manukato wala kwa hina,[11] kwani hiyo ni rangi.” Nikasema: “Nijichane kwa nini?” Akasema: “Kwa majani ya mkunazi.” [Imetolewa na Abuu Daawuwd na An-Nasaaiy na Isnaad yake ni hasan]

 

 

 

949.

وَعَنْهَا رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا، {أَنَّ اِمْرَأَةً قَالَتْ: يَا رَسُولَ اَللَّهِ! إِنَّ اِبْنَتِي مَاتَ عَنْهَا زَوْجُهَا، وَقَدْ اِشْتَكَتْ عَيْنَهَا، أَفَنَكْحُلُهَا ؟ قَالَ: "لَا"} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ

Kutoka kwa Ummu Salamah (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema kuwa: Mwanamke mmoja alisema Ee Rasuli wa Allaah! Binti yangu amefiwa na mumewe na jicho lake linauma, je tumpake wanja? Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akasema: “Hapana.” [Al-Bukhaariy, Muslim]

 

 

 

950.

وَعَنْ جَابِرٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: {طُلِّقَتْ خَالَتِي، فَأَرَادَتْ أَنْ تَجُدَّ نَخْلَهَا فَزَجَرَهَا رَجُلٌ أَنْ تَخْرُجَ، فَأَتَتْ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  فَقَالَ: بَلْ جُدِّي نَخْلَكِ، فَإِنَّكَ عَسَى أَنْ تَصَدَّقِي، أَوْ تَفْعَلِي مَعْرُوفًا} رَوَاهُ مُسْلِمٌ

Kutoka kwa Jaabir (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: “Khaalat wangu (Mama mdogo/mkubwa) alitalikiwa, akataka kuenda kukata mitende yake, mtu mmoja akamkanya asitoke.[12] Akamuendea Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ). Akasema: “Nenda ukakate mitende yako kwani pengine ukatoa Swadaqah au ukafanya wema.”[13] [Imetolewa na Muslim]

 

 

 

951.

وَعَنْ فُرَيْعَةَ بِنْتِ مَالِكٍ، {أَنَّ زَوْجَهَا خَرَجَ فِي طَلَبِ أَعْبُدٍ لَهُ فَقَتَلُوهُ. قَالَتْ: فَسَأَلْتُ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  أَنْ أَرْجِعَ إِلَى أَهْلِي; فَإِنَّ زَوْجِي لَمْ يَتْرُكْ لِي مَسْكَنًا يَمْلِكُهُ وَلَا نَفَقَةً، فَقَالَ: "نَعَمْ". فَلَمَّا كُنْتُ فِي اَلْحُجْرَةِ نَادَانِي، فَقَالَ: " اُمْكُثِي فِي بَيْتِكَ حَتَّى يَبْلُغَ اَلْكِتَابُ أَجَلَهُ". قَالَتْ: فَاعْتَدَدْتُ فِيهِ أَرْبَعَةَ أَشْهُرٍ وَعَشْرًا، قَالَتْ: فَقَضَى بِهِ بَعْدَ ذَلِكَ عُثْمَانُ}  أَخْرَجَهُ أَحْمَدُ، وَالْأَرْبَعَةُ، وَصَحَّحَهُ اَلتِّرْمِذِيُّ، والذُّهْلِيُّ، وَابْنُ حِبَّانَ، وَالْحَاكِمُ وَغَيْرُهُمْ 

Kutoka kwa Furay’ah bint Maalik[14] amesema: Mumewe alitoka kuenda kuwatafuta watumwa wake, wakamuua. Akaeleza: Nikamuuliza Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) kuhusu kurudi kwa jamaa zangu kwani mume wangu hakuniachia maskani anayomiliki wala matumizi. Nabiy akaniambia: “Sawa.” Nilipokuwa chumbani aliniita akaniambia: “Kaa nyumbani mwako mpaka eda imalizike.”[15] Nikakaa Eda humo miezi minne na siku kumi. (Furay’ah) akasema: “Baada ya hapo ‘Uthmaan akahukumu kwa hukumu hiyo.” [Imetolewa na Ahmad na Al-Arba’ah (At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah) na akaisahihisha At-Tirmidhiy, Adh-Dhuhliyy, Ibn Hibbaan , Al-Haakim na wengineo]

 

 

 

952.

وَعَنْ فَاطِمَةَ بِنْتِ قَيْسٍ قَالَتْ: {يَا رَسُولَ اَللَّهِ! إِنَّ زَوْجِي طَلَّقَنِي ثَلَاثًا، وَأَخَافُ أَنْ يُقْتَحَمَ عَلَيَّ، قَالَ: فَأَمَرَهَا، فَتَحَوَّلَتْ} رَوَاهُ مُسْلِمٌ 

Kutoka kwa Faatwimah bint Qays amesema: “Ee Rasuli wa Allaah! Mume wangu ameniacha talaka tatu nami nachelea kushambuliwa.” Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akamuamrisha  ahame. [Imetolewa na Muslim]

 

 

 

953.

وَعَنْ عَمْرِو بْنِ الْعَاصِ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ قَالَ: {لَا تُلْبِسُوا عَلَيْنَا سُنَّةَ نَبِيِّنَا، عِدَّةُ أُمِّ اَلْوَلَدِ إِذَا تُوُفِّيَ عَنْهَا سَيِّدُهَا أَرْبَعَةَ أَشْهُرٍ وَعَشْرًا} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَأَبُو دَاوُدَ، وَابْنُ مَاجَهْ، وَصَحَّحَهُ اَلْحَاكِمُ، وَأَعَلَّهُ اَلدَّارَقُطْنِيُّ بِالِانْقِطَاعِ 

Kutoka kwa ‘Amr bin Al-‘Aasw (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: “Msituchanganye na Sunnah ya Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) wetu. Eda ya mjakazi (aliyezalishwa na bwana wake) bwana wake akifa ni miezi minne na siku kumi.”[16] [Imetolewa na Ahmad, Abuu Daawuwd na Ibn Maajah, na akaisahihisha Al-Haakim, na akaidhoofisha kwa kuwa Munqatw Ad-Daaraqutwniy]

 

 

 

954.

وَعَنْ عَائِشَةَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا قَالَتْ: {إِنَّمَا اَلْأَقْرَاءُ، اَلْأَطْهَارُ} أَخْرَجَهُ مَالِكٌ فِي قِصَّةٍ بِسَنَدٍ صَحِيحٍ 

Kutoka kwa ‘Aaishah (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema: “Quruwu tatu ni twahara.”[17] [Imetolewa na Maalik kwa Isnaad sahihi katika kisa fulani]

 

 

 

955.

وَعَنِ اِبْنِ عُمَرَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهُمَا قَالَ: {طَلَاقُ اَلْأَمَةِ تَطْلِيقَتَانِ، وَعِدَّتُهَا حَيْضَتَانِ}  رَوَاهُ اَلدَّارَقُطْنِيُّ  وَأَخْرَجَهُ مَرْفُوعًا وَضَعَّفَهُ   

وَأَخْرَجَهُ أَبُو دَاوُدَ، وَاَلتِّرْمِذِيُّ، وَابْنُ مَاجَهْ: مِنْ حَدِيثِ عَائِشَةَ، وَصَحَّحَهُ اَلْحَاكِمُ، وَخَالَفُوهُ، فَاتَّفَقُوا عَلَى ضَعْفِهِ 

Kutoka kwa Ibn ‘Umar (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) amesema: “Talaka ya mjakazi ni talaka mbili, na Eda yake ni hedhi mbili.”[18] [Imetolewa na Ad-Daaraqutwniyy ikiwa Marfuw’ na ameidhoofisha]

Na wameipokea Abuu Daawuwd, At-Tirmidhiy na Ibn Maajah kutoka katika Hadiyth ya ‘Aaishah, na akaisahihisha Al-Haakim. (Wanazuoni wa Hadiyth) wametofautiana nae, wameafikiana kuwa ni dhaifu.

 

 

 

956.

وَعَنْ رُوَيْفِعِ بْنِ ثَابِتٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  عَنْ اَلنَّبِيِّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ: {لَا يَحِلُّ لِامْرِئٍ يُؤْمِنُ بِاَللَّهِ وَالْيَوْمِ اَلْآخِرِ أَنْ يَسْقِيَ مَاءَهُ زَرْعَ غَيْرِهِ} أَخْرَجَهُ أَبُو دَاوُدَ، وَاَلتِّرْمِذِيُّ، وَصَحَّحَهُ اِبْنُ حِبَّانَ، وَحَسَّنَهُ اَلْبَزَّارُ 

Kutoka kwa Ruwyfi’ bin Thaabit[19] (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Si halaal kwa mtu anayemuamini Allaah na siku ya mwisho kunyosheleza maji yake katika mmea wa mtu mwingine.” [Imetolewa na Abuu Daawuwd na At-Tirmidhiy, na akaisahihisha Ibn Hibbaan, na Al-Bazzaar akasema ni Hasan]

 

 

 

957.

وَعَنْ عُمَرَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ {فِي اِمْرَأَةِ اَلْمَفْقُودِ تَرَبَّصُ أَرْبَعَ سِنِينَ، ثُمَّ تَعْتَدُّ أَرْبَعَةَ أَشْهُرٍ وَعَشْرًا} أَخْرَجَهُ مَالِكٌ، وَالشَّافِعِيُّ 

Kutoka kwa ‘Umar (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: Kuhusu mwanamke ambaye mumewe ametoweka (hajulikani aliko): “Asubiri kwa miaka minne kisha ataketi eda miezi minne na siku kumi.”[20] [Imetolewa na Maalik na Ash-Shaafi’yy]

 

 

 

958.

وَعَنْ اَلْمُغِيرَةِ بْنِ شُعْبَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  {اِمْرَأَةُ اَلْمَفْقُودِ اِمْرَأَتُهُ حَتَّى يَأْتِيَهَا اَلْبَيَانُ} أَخْرَجَهُ اَلدَّارَقُطْنِيُّ بِإِسْنَادٍ ضَعِيفٍ 

Kutoka kwa Al-Mughiyrah bin Shu’bah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mke wa mume aliyetoweka (asiyejulikana aliko) anabaki kuwa ni mkewe mpaka ajiwe na ubainifu.” [Imetolewa na Ad-Daaraqutwniy kwa isnaad dhaifu]

 

 

 

959.

وَعَنْ جَابِرٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {لَا يَبِيتَنَّ رَجُلٌ عِنْدَ اِمْرَأَةٍ، إِلَّا أَنْ يَكُونَ نَاكِحًا، أَوْ ذَا مَحْرَمٍ} أَخْرَجَهُ مُسْلِمٌ

Kutoka kwa Jaabir (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mwanamume yeyote asilale kwa mwanamke[21] isipokuwa awe amemuoa au ni maharimu wake.”[22] [Imetolewa na Muslim]

 

 

 

960.

وَعَنِ اِبْنِ عَبَّاسٍ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهُمَا، عَنْ اَلنَّبِيِّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ: {لَا يَخْلُوَنَّ رَجُلٌ بِاِمْرَأَةٍ، إِلَّا مَعَ ذِي مَحْرَمٍ} أَخْرَجَهُ اَلْبُخَارِيُّ 

Kutoka kwa Ibn ‘Abbaas (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Asikae faragha mwanamume na mwanamke ila awe pamoja naye maharimu.” [Imetolewa na Al-Bukhaariy]

 

 

 

961.

وَعَنْ أَبِي سَعِيدٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ أَنَّ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ فِي سَبَايَا أَوْطَاسٍ: {لَا تُوطَأُ حَامِلٌ حَتَّى تَضَعَ، وَلَا غَيْرُ ذَاتِ حَمْلٍ حَتَّى تَحِيضَ حَيْضَةً} أَخْرَجَهُ أَبُو دَاوُدَ، وَصَحَّحَهُ اَلْحَاكِمُ  وَلَهُ شَاهِدٌ: عَنْ اِبْنِ عَبَّاسٍ فِي اَلدَّارَقُطْنِيِّ 

Kutoka kwa Abuu Sa’iyd (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema katika mateka wa kabila la Awtwaas: “Mjamzito asijamiiwe mpaka ajifunguwe, na asiyekuwa mjamzito asijamiiwe mpaka apate hedhi moja.” [Imetolewa na Abuu Daawuwd na akaisahihisha Al-Haakim nayo ina ushahidi katika Hadiyth ya ‘Abdullaah bin ‘Abbaas iliyopokewa na Ad-Daaraqutwniy]

 

 

 

962.

وَعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  عَنْ اَلنَّبِيِّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ: {اَلْوَلَدُ لِلْفِرَاشِ، وَلِلْعَاهِرِ اَلْحَجَرُ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ مِنْ حَدِيثِهِ 

وَمِنْ حَدِيثِ عَائِشَةَ فِي قِصَّةٍ  وَعَنْ اِبْنِ مَسْعُودٍ، عِنْدَ النَّسَائِيِّ  وَعَنْ عُثْمَانَ. عِنْدَ أَبِي دَاوُدَ

Kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mtoto ni wa kitanda,[23] mzinifu lake ni jiwe.” [Al-Bukhaariy, Muslim kutoka katika Hadiyth yake (Abuu Hurayrah)]

 

Na kutoka katika Hadiyth ya ‘Aaishah katika kisa kimoja kimepokewa kwa ‘Abdullaah bin Mas-‘uwd na An-Nasaaiy vile vile kimepokewa ‘Uthmaan kwa Abuu Daawuwd

 

[1] Eda ni muda wa kusubiri ambapo mwanamke haruhusiwi kuolewa, baada ya kifo cha mumewe au kuachika. Kuna aina tatu za Eda: 1. Eda ya kuzaliwa. 2. Eda ya hedhi, na 3. Eda ya mwezi. Kwa mwanamke mwenye mimba, katika hali yoyote iwe ni kifo cha mumewe au kuachika, eda yake ni baada ya kuzaliwa mtoto. Kwa mfano ameachika au mumewe amefariki leo, na siku inayofuata akajifungua mtoto, eda yake huisha kwa kuzaliwa mtoto. Hapo anaruhusiwa kuolewa wakati wowote, lakini kwa muda wote ambapo atakuwa yupo katika nifaas hatoruhusiwa kuingiliwa na mumewe.

 

[2] Al-Ihdaad ni ile hali ya kuangalilia msiba, kwa mwanamke aliyefiwa na mumewe.

[3] Huyu ni Subay’a ni binti wa Al-Haarith Al-Aslamiyyah wa Banu Aslam. Alikuwa ni Swahaabiyyah. Ibn Sa’d anamtaja kuwa alikuwa ni miongoni mwa waliohajiri. Aliolewa na Sa’d bin Khawlah ambaye alifariki katika Hajjatul Wadaai’ baada ya hapo akaolewa na kijana katika jamaa zake. Imetajwa katika mapokezi mengine kuwa aliolewa na Abuu Sanaabil.

 

[4] Huyu ni Muhammad bin Muslim bin ‘Ubaidillaah bin Abdillaah bin Shihaab Al-Quraysh Az-Zuhriy, mmoja katika Maimaamu wakubwa na Mwanazuoni mkubwa katika Hijaaz na Shaam. Alikua ni kiongozi wa kizazi cha nne cha Taabi’iyna uwezo wake ulifahamika na kukubaliwa. Al-Layth anasema hakuwahi kumuona Mwanazuoni aliyekusanya elimu nyingi kama Ibn Shihaab. Maalik anaeleza Ibn Shihaab alikuwa katika watu karimu na hakuwa na mfano wake. Alifariki mwaka 124H.

[5] Mume wake Bariyrah alikuwa ni mtumwa. Baada ya kuachwa huru kutoka utumwani kama mwanamke huru, alipewa khiyari ya kuchagua kuhusu ndoa yake. Bariyrah alichagua kuvunja ndoa yake. Kwa hivyo ilibidi kukaa eda ya hedhi tatu. Hadiyth hii inamaanisha kuwa muda wa eda unaotakiwa ni kwa kuangalia hali ya mke sio ya mume.

 

[6] Huyu ni Abuu ‘Amr ‘Aamir bin Sharahil bin ‘Abdillaah Ash-Sha’biyy Al-Hamdani Al-Kufi. Ni taabi’ na maarufu na Mwanazuoni mkubwa. Az-Zuhri anamueleza kuwa: “Ulamaa ni wanne: Ibn Al-Musayab wa Madiynah, ASh-Sha’b wa Kufa, Hasan Al-Baswri aliyepo Baswra na Mak-hul wa Shaam”. Ash-Sha’biyy alizaliwa wakati wa Ukhalifa wa ‘Umar na inasemekana kuwa alizaliwa miaka sita kabla ya kuanza kwa Ukhalifa wa ‘Uthmaan.

 

[7] Hukumu ya kishariy’ah kuhusu talaka ni kuwa ni jukumu la mwanamme kugharamia maskani na chakula hadi muda wa eda wa mwanamke unapomalizika. Lakini mwanamme huyo huyo hana haki ya kumgharamia maskani na chakula pindi anapotoa talaka tatu. (ambayo si talaka rejea)

[8] Muda wa eda kwa mjane (asiyekuwa mjamzito) ni miezi mine na siku kumi. Eda ya mwanamke aliyeachika ni hedhi tatu kamili, maadamu ni bado kijana. Ama ikiwa ni ajuza hedhi yake imeshakatika au ni msichana mdogo eda yake ni miezi mitatu.

 

[9] ‘Aswbi ni aina ya nguo kutoka Yemen

 

[10] Qustwi ni aina ya udi au manukato.

[11] Maelekezo yaliyopo wakati wa eda ni kuwa hairuhusiwi kwa mwanamke kutumia manukato, kuvaa nguo za rangi rangi, kupaka wanja na kuingia katika mkataba au mazungumzo yoyote ya posa na mwanamme. Hali hii inahusu wanawake wote walioolewa kwa ujumla.

[12] Furay’ah bint Maalik ni dada yake Abuu Sa’d AL-Khudriyy alishuhudia Bay’ah Ar-Ridhwaan. Amepokea baadhi ya Hadiyth

[13] Wanawake walioachika wanatakiwa wakae eda zao katika nyumba za waume zao, iwe wameachika au ni wajane. Hata hivyo mwanamke aliyeachika talaka tatu haiwi hivyo. Mwanamke aliyeachika talaka tatu hakai katika nyumba ya mume wake.

 

[14] Jina lake ni Furay’ah bint wa Maalik bin Sinaan Al-Khudriyah, dada wa Swahaba maarufu Sa’d Al-Khudriyy. Alihudhuria Bay’ah Ar-Ridhwaan.

 

[15] Mjane anatakiwa amalize muda wake wa eda katika nyumba ya mumewe. Hii ndio hukumu iliyotolewa na ‘Ulamaa  wengi.

[16] Muda wa Eda wa Ummul Walad (kijakazi aliyejifungua mtoto wa bwana wake), kama ni mjane, baadhi ya ‘Ulamaa wanaona kuwa ni miezi mine na siku kumi, wengine wanaona kuwa ni hedhi moja, ambayo ndiyo hukumu iliyo sahihi.

 

[17] Kuna maneno kadha ya kiarabu ambayo ina maana ya neno na kinyume chake. Maneno kama hayo yanaitwa Dhawaatul-‘Addad (ni maneno na kinyume chake). Moja katika maneno hayo ni Al-Qar-u ambayo maana yake ni kipindi cha hedi, na wakati huo huo ina maana ya Twuhr na kadhalika.

[18] Hii ina maana kijana wa kiume (mtumwa) anaacha kwa talaka mbili na mwanamke muda wake wa eda ni hedhi mbili.

[19] Ruwyfi’ bin Thaabit Al-Answaar ni wa kabila la Baniy Maalik bin An-Najjar, anahisabiwa ni katika wakazi wa Misri. Alifariki mwaka wa 46 Hijriyyah.

 

[20] Mwanamke aliyepotewa na mume wake asubiri miaka mine (kabla ya kuolewa tena. Muda huu uliwekwa na ‘Umar bin Al-Khatwaab. Baadaye Maswahaba walikubaliana na hukumu hii na ndio hukumu ambayo inafuatwa na ‘Ulamaa wote.

[21] Hadiyth hii inakataza mwanamme kuwa na mwanamke ajnabi peke yake. Hukumu ya Hadiyth hii kadhalika imetajwa katika Hadiyth nyingine, ushawishi wa shaytwaan unaweza kuingia katikati yao na kufanya jambo lisilotakiwa la uzinifu. Hata kama hawawezi au wasifanye jambo hili lakini kuna uwezekano mkubwa wa kutuhumiwa katika hilo, ni vizuri watu wakawa mbali na tuhuma kama hizi.

 

[22] Maharimu ni jamaa wa karibu wa mwanamke ambao ndoa baina yao ni haraam, uharaam wa milele.

[23] Hii ina maana mtoto wa mwanamke atanasibishwa kwa mume wake na atakuwa chini ya ulezi wake, ikiwa mtu atadai kuwa alikuwa na uhusiano na mwanamke fulani  na ya kuwa mtoto ni wake, katika hali hii bado mtoto atakuwa chini ya ulezi wa mumewe na yule mwanamme aliyethibitisha kuzini, shariy’ah itamhukumu kwa hilo. Hakuna hukumu yoyote itakayochukuliwa dhidi ya mwanamke kwa maneno ya mtu bila ushahidi wa wazi wa watu wane. Vinginevyo hukumu itamuendea aliyemtuhumu na kuadhibiwa yeye.

Share