034-Saba-a: Utangulizi Wa Suwrah

 

034-Saba-a: Utangulizi Wa Suwrah

 

Alhidaaya.com

 

 

 

Imeteremka: Makkah kwa itifaki ya ‘Ulamaa.

 

Idadi Za Aayah: 54

 

Jina La Suwrah: Saba-a

 

Imeitwa Saba-a (Mji wa Yemen), na inayodalilisha ni kutajwa kisa cha watu wake katika Aayah namba (15).

 

Miongoni Mwa Makusudio Ya Suwrah:

 

1-Kubainisha hali za watu wanapopata neema (wakaikufuru), na Desturi za Allaah katika kuibadilisha hali hiyo (ya neema). [Al-Mukhtaswar Fiy Tafsiyr Al-Qur-aan Al-Kariym]

 

2-Kubatilisha ushirikina na kuwapinga washirikina.

 

3-Kubainisha Tawhiyd ya Allaah (سبحانه وتعالى) kwa dalili na ukweli wa Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم).

 

Miongoni Mwa Maudhui Ya Suwrah:

 

1-Suwrah imefunguliwa kwa Kumhimidi Allaah (سبحانه وتعالى) Aliyetakasika na kila mapungufu, Mmiliki wa vilivyomo mbinguni na ardhini, na kubainisha upana (kuenea) wa Ilimu Yake.

 

2-Imebainisha kwamba washirikina wanapinga Siku ya Qiyaamah na kufufuliwa, na baadhi ya maneno yao ya yaliyokuwa ni baatwil.

 

3-Imetajwa sehemu fulani ya kisa cha Nabiy Daawuwd (عليه السّلام) na mwanawe Sulaymaan (عليه السّلام) na neema na fadhila zake za kutiishiwa majini. 

 

4-Imetajwa kisa cha kabila la Saba-a waliokufuru Neema za Allaah (سبحانه وتعالى) na hatima yao.

 

5-Imebainishwa Tawhiyd ya Allaah (سبحانه وتعالى) na kwamba Yeye Ndiye Mwenye kuruzuku waja.

 

6-Imebainishwa kwamba Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) ametumwa kwa watu wote ulimwenguni na sio Waarabu pekee.

 

7-Imetajwa baadhi ya matukio ya Siku ya Qiyaamah, na mijadala itayokuwepo kati ya wafuasi na wanaofuatwa.

 

8-Radd kwa matajiri ambao walidai kuwa mali zao na watoto wao vitawanufaisha Siku ya Qiyaamah.

 

9-Imetajwa baadhi ya ada za washirikina kutokuamini Qur-aan na kutokumuamini Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم).

 

10-Daawah kwa makafiri ya kuwataka waifikirie sana Daawah ya Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم).

 

11-Suwrah imekhitimishwa kwa kuwatisha makafiri ya kwamba watakuwa na mwisho mbaya, kama wataendelea na misimamo yao ya ukafiri na ukaidi.

 

Faida:

 

Suwrah Saba-a (34), ni miongoni mwa Suwrah tano zinazoanzia kwa AlhamduliLlaah. Nyenginezo ni Al-Faatihah (1), Al-An’aam (6), Al-Kahf (18), na Faatwir (35).

 

 

Share