07-Swahiyh Fiqh As-Sunnah: Kitabu Cha Mavazi Na Mapambo: Pambo Kwa Mwanamke Wa Kiislamu: Kutumia Mafuta Mazuri

 

Swahiyh Fiqh As-Sunnah

 

كِتَابُ اللِّبَاسِ وَالزِّيْنَةِ 

Kitabu Cha Mavazi Na Mapambo

 

 

الزِّيْنَةُ للمَرْأَةِ المُسْلِمَةِ

Pambo Kwa Mwanamke Wa Kiislamu

 

Alhidaaya.com

 

 

07-Kutumia Mafuta Mazuri:

  

Kutumia mafuta mazuri ni katika madh-hari ya pambo lililoruhusiwa kwa mwanamke kwa ajili ya mumewe.  Anaweza kutumia mafuta yoyote ayapendayo.

 

Zaynab bint Salamah amesema: 

 

"دَخَلْتُ عَلَى أُمِّ حَبِيبَةَ زَوْجِ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ  حِينَ تُوُفِّيَ أَبُوهَا أَبُو سُفْيَانَ بْنُ حَرْبٍ، فَدَعَتْ أُمُّ حَبِيبَةَ بِطِيبٍ فِيهِ صُفْرَةٌ خَلُوقٌ أَوْ غَيْرُهُ فَدَهَنَتْ مِنْهُ جَارِيَةً، ثُمَّ مَسَّتْ بِعَارِضَيْهَا، ثُمَّ قَالَتْ وَاللَّهِ مَا لِي بِالطِّيبِ مِنْ حَاجَةٍ، غَيْرَ أَنِّي سَمِعْتُ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ  يَقُولُ:‏ "‏لاَ يَحِلُّ لاِمْرَأَةٍ تُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الآخِرِ أَنْ تُحِدَّ عَلَى مَيِّتٍ فَوْقَ ثَلاَثِ لَيَالٍ، إِلاَّ عَلَى زَوْجٍ أَرْبَعَةَ أَشْهُرٍ وَعَشْرًا"

 

“Niliingia kwa Ummu Habiybah mke wa Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wakati alipofariki baba yake Abu Sufyaan bin Harb.  Ummu Habiybah akaagiza aletewe manukato yenye unjano wa khalouwq na akampaka kijakazi aliyekuwepo, naye akajipaka kidogo mashavuni, halafu akasema:  Wallaah, mimi sina haja na mafuta mazuri isipokuwa tu kwa vile nimemsikia Rasuli wa Allaah (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akisema:  “Si halali kwa mwanamke anayemwamini Allaah na Siku ya mwisho kumuomboleza maiti kwa zaidi ya siku tatu, isipokuwa kwa mumewe, ni miezi minne na siku kumi ”.  [Al-Bukhaariy (5334) na Muslim (1486)]    

 

Mwanamke Anaweza Kutumia Mafuta Mazuri Ya Kiume Na Mwanamume Anaweza Kutumia Ya Kike:

 

Hii ni kwa Hadiyth ya ‘Aaishah:

 

"أَنَّ امْرَأَةً، سَأَلَتِ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ  عَنْ غُسْلِهَا مِنَ الْمَحِيضِ، فَأَمَرَهَا كَيْفَ تَغْتَسِلُ قَالَ ‏"‏ خُذِي فِرْصَةً مِنْ مِسْكٍ فَتَطَهَّرِي بِهَا ‏"‏‏.‏ قَالَتْ كَيْفَ أَتَطَهَّرُ قَالَ ‏"‏ تَطَهَّرِي بِهَا ‏"‏‏.‏ قَالَتْ كَيْفَ قَالَ ‏"‏ سُبْحَانَ اللَّهِ تَطَهَّرِي ‏"‏‏.‏ فَاجْتَبَذْتُهَا إِلَىَّ فَقُلْتُ تَتَبَّعِي بِهَا أَثَرَ الدَّمِ"

 

“Kwamba mwanamke mmoja alimuuliza Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihi wa sallam) namna ya kuoga josho la hedhi.  Rasuli akamwelekeza namna ya kuoga akimwambia:  Chukua kipande cha kitambaa kilichotiwa miski ujipanguse nacho (kwenye utupu).  Akauliza:  Nijipanguse nacho vipi?  Akamwambia:  Jisafishe nacho.  Akauliza: Vipi?  Akasema:  Subhaanal Laah!  Jisafishe.  Nikamvutia kwangu nikamwambia:  Kipitishe sehemu ilipo athari ya damu”.  [Swahiyh Al-Bukhaariy (314)]

 

Hapa Rasuli amemwelekeza mwanamke yule atumie kitambaa kilichotiwa mafuta ya miski, na mafuta haya ni mahsusi kwa wanaume.

 

Katika Hadiyth ya Abu Sa’iyd, amezungumzia kupendeza mwanaume ajitie mafuta mazuri Siku ya Ijumaa “hata kama ni ya wanawake”.  Hadiyth inasema:

 

"غُسْلُ يَوْمِ الْجُمُعَةِ عَلَى كُلِّ مُحْتَلِمٍ وَسِوَاكٌ وَيَمَسُّ مِنَ الطِّيبِ مَا قَدَرَ عَلَيْهِ ‏"‏ [وَلَوْ مِنْ طِيبِ الْمَرْأَةِ" ]

 

“Ni juu ya kila aliyebaleghe kuoga Siku ya Ijumaa na kupiga mswaki, na ajitie mafuta mazuri anayoweza kuyapata [hata kama ni ya wanawake].  [Swahiyh Muslim (846), An-Nasaaiy (1375) na Abu Daawuwd (344)]

 

 

 

Share