Kuomboleza Katika Misiba Kwa Kujipiga Na Kuchana Nguo

 

Kuomboleza Katika Misiba Kwa Kujipiga Na Kuchana Nguo

 

Alhidaaya.com

 

 

 

Swali:

 

Asalam aleykum warahamtullah wabarakatu.

 

Ndugu katika Imani mimi ni mmoja wa wale wenye kufuatilia na kupata vipeperushi vyenu mnavyotoa kila mwezi, ninaishi Muhoro Rufiji, swali langu je Uislamu unasema nini kuhusu mtu anapofiwa akalia kupita kiyasi na wengine wanafikia kuchana nguo zao, kijimwagia machanga,unga na kuna watu wananyoa nywele zao kwa ajili ya kuomboleza hili jambo linajuzu? Na je kuomboleza imethibiti ni siku ngapi?

 

 

Jibu:

 

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Uislamu unakataza kabisa mtu kulia kupita kiasi, kujichania nguo, kunyoa nywele na kuomboleza maombolezo ya kijahiliya, na dalili  ni kama zifuatazo:

 

Amesema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): “Si katika sisi (Waislamu), mwenye kulia kwa kujipigapiga, kujichania nguo na kuomboleza kwa maombolezo ya kijahiliya” [al-Bukhaariy na Muslim]

 

Na pia,

 

Amesema Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) “Jambo hili la kulia kwa kelele si katika mwenendo wangu, bali moyo unahuzunika na macho yanatoa machozi na wala asikasirikiwe na Allaah.” [al-Haakim na Ibn Hibbaan]

 

Na pia,

 

Amesema Nabiy Swalla (Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), “Si katika sisi mwenye kulia kwa kelele, kupasua nguo na anayejipiga uso na akatamka maneno ya kijahiliya.” [Tuhfatul-Ahwadhiy, Mj. 4, Uk. 40-41]

 

Na pia,

 

Abuu Muwsaa alipokuwa mgonjwa taabaan ghafla alizimia, mkewe akapiga kelele kulia kwa sauti, alipozinduka akasema kumwambia mkewe: “Mimi nimeepukana na matendo aliyokataza Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kwani Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  ameepukana na yule mwenye kulia na kupayuka sababu ya msiba, mwenye kunyoa nywele zake na mwenye kupasua nguo zake sababu ya msiba.” [al-Bukhaariy na Muslim]

 

Pia,

 

Anas Bin Maalik (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema kuwa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Subira inatakikana pale mwanzo wa mshtuko (wa msiba).” [al-Bukhaariy, Muslim na Abu Daawuwd]

 

Na kuhusu idadi ya siku za kuomboleza kunatakikana kusizidi siku tatu tu kwa kutokana na  Swahaba Abdullaah bin Ja‘afar (Radhwiya Allaahu ‘anhumaa) kwamba hakika Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliwapa muda wa siku tatu watu wa Ja‘far bin Abiy Twaalib kwenda kufarijiwa kisha Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akawaendea (siku ya tatu) akasema msilie juu ya ndugu yangu baada ya leo.” [Abu Daawuwd na an-Nasaaiy]

 

Na kumfariji mfiwa kuna fadhila kubwa kutokana na  Hadiyth ya Anas Bin Malik (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba: Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: Mwenye kumfariji ndugu yake Muumini katika msiba wake, Allaah Atamvisha vazi zuri tukufu Siku ya Qiyaamah” [Al-Khatwiyb Mj. 7, Uk. 397]

 

Kwa shahidi hizo, ni bora na ndio salama kwa Dini yako Muislamu kujiepusha na mambo hayo yasiyo ya Kiislam ambayo yameigizwa kutoka katika Jaahiliya ya mwanzo na Jaahiliya hii ambayo bado wamo ndani yake wasio Waislam.

 

Na yasiwaghuri yale yanayofanywa na baadhi ya watu wanaojiita Waislamu kama Mashia ambao hufanya mambo haya ya kujipiga na kujikatakata pale wanapoadhimisha vifo vya wanaodai ni 'Imamu wao katika mwezi wa Al-Muharram. Hayo ni mambo potofu yanayopingana na khulqa njema na upole, huruma, na usamahevu wa Dini yetu hii safi ya Kiislam.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share