Siku Za Kiislamu Zinaanzia Saa Ngapi?

 

 Siku Za Kiislamu Zinaanzia Saa Ngapi?

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Siku kwa waislam inaanza na kwisha saa ngapi?

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Siku za Kiislamu zinaanza kuhesabika jua linapozama yaani wakati wa Magharibi hivyo kama mfano leo ni siku ya Alkhamiys na Magharibi inapoingia, basi usiku huo huitwa tena Laylatul-Jumu'ah (Usiku wa Ijumaa) na hali kadhalika kwa masiku mengine.

 

Na si saa sita ya usiku kama ilivyo hali ya siku au tarehe za ki-Gregorian ambayo ni marekebisho ya tarehe zilizokuwa zikijulikana zamani kama tarehe za ki-Julian ambazo ndizo zinazotumika katika ulimwengu leo hii. Nazo hujulikana zaidi kwa wengi kama tarehe za kikristo au tarehe za kizungu!

 

Kubadilika huko kwa siku za Kiislam wakati wa Magharibi, ni kwa sababu tarehe za Kiislam hufuata mwezi na hazifuati jua kama ilivyo hali ya tarehe nyinginezo. Na ndio maana Waislamu huanza kuswali Swalaah ya taaarawiyh usiku huo huo wa  kuandama mwezi kabla ya kuanza Swawm kwa vile usiku huo umeshaingia kuwa ni wa mwezi wa Ramadhwaan.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share