Kusengenya (Ghiybah) Japo Kuwa Anayesengenywa Anayo Sifa Yenyewe Ni Dhambi

 

Kusengenya (Ghiybah) Japo Kuwa Anayesengenywa Anayo Sifa Yenyewe Ni Dhambi

 

Alhidaaya.com

 

Swali:

 

Tunasikia kuna Hadiythi inasema ukimsema mtu ni mfupi au mrefu ni vibaya! nami sikusema hivyo kwa kumdharau bali nimeuelezea wasifu wake jinsi alivyo, naomba ufafanuzi?

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho. 

 

Muislam haruhusiwi kuichafua heshima ya mwenzie kwa kumkashifu mbele ya watu wengine, sawa ikiwa unachokisema kina ukweli au kinyume chake.

 

Hata ikiwa mtu anayo sifa ile lakini madamu unamsema nyuma yake na ni jambo ambalo mwenyewe asingelipenda kulisikia basi pia huingia katika hukmu hii ya ghiybah: 

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رضي الله عنه ، أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ :  (( أَتَدْرُونَ مَا الْغِيبَةُ ؟ )) قَالُوا : اللَّهُ وَرَسُولُهُ أَعْلَمُ ، قَالَ :   ((ذِكْرُكَ أَخَاكَ بِمَا يَكْرَهُ )) ، قِيلَ : أَفَرَأَيْتَ إِنْ كَانَ فِي أَخِي مَا أَقُولُ ؟ قَالَ :  (( إِنْ كَانَ فِيهِ مَا تَقُولُ فَقَدِ اغْتَبْتَهُ ، وَإِنْ لَمْ يَكُنْ فِيهِ فَقَدْ بَهَتَّهُ)) [ أخرجه مسلم ]

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhwiya Allahu ‘anhu) kwamba aliuuliza Nabiy (Swalla Allahu ‘alayhi wa alihi wa sallam): ((Je mnajua maana ya Ghiybah? [Kusengenya])) Wakasema: Allaah na Rasuli Wake wanajua. Akasema: ((Ni kumtaja ndugu yako kwa jambo analochukia)). Akaulizwa: Hebu nieleze, iwapo ndugu yangu anayao yale niyasemayo? Akasema: ((Ikiwa analo hilo usemalo basi umeshamsengenya, na ikiwa hana hilo usemalo basi umeshamzushia uongo)) [Muslim]

 

Bibi ‘Aaishah alisema: “Nilimuambia Nabiy (Swalla Allahu ‘alayhi wa sallam):

 

سبك من صفية كذا وكذا"، قال بعض الرواة: تعني قصيرة، فقال: (( لقد قلت كلمة لو مزجت بماء البحر لمزجته))  

"Acha (kumsema) Swafiyah kadhaa na kadhaa” [katika riwaaya nyingine yaani ni mfupi] Akasema Nabiy(Swalla Allahu ‘alayhi wa alihi wa sallam) "Umesema neno ambalo lingelichanganywa na maji ya bahari lingeichafua." [Abu Daawuud na At-Tirmidhiy]

 

Kumsengenya mtu nyuma yake (Ghiybah) ni dhambi ambazo hazisamehewi na Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) hadi mwenyewe uliyemsengenya akusamehe kwani hiyo ni katika haki za baina ya binaadamu. Ama haki za baina ya Allah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na mja Wake, Yeye Humsamehe pindi anapoomba toba. Na jambo hili la haki za baina yetu limekuja makatazo yake katika Aayah zifuatazo:  

 

يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا لَا يَسْخَرْ قَوْمٌ مِّن قَوْمٍ عَسَىٰ أَن يَكُونُوا خَيْرًا مِّنْهُمْ وَلَا نِسَاءٌ مِّن نِّسَاءٍ عَسَىٰ أَن يَكُنَّ خَيْرًا مِّنْهُنَّ ۖ وَلَا تَلْمِزُوا أَنفُسَكُمْ وَلَا تَنَابَزُوا بِالْأَلْقَابِ ۖ بِئْسَ الِاسْمُ الْفُسُوقُ بَعْدَ الْإِيمَانِ ۚ وَمَن لَّمْ يَتُبْ فَأُولَـٰئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ﴿١١﴾يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا اجْتَنِبُوا كَثِيرًا مِّنَ الظَّنِّ إِنَّ بَعْضَ الظَّنِّ إِثْمٌ ۖ وَلَا تَجَسَّسُوا وَلَا يَغْتَب بَّعْضُكُم بَعْضًا ۚ أَيُحِبُّ أَحَدُكُمْ أَن يَأْكُلَ لَحْمَ أَخِيهِ مَيْتًا فَكَرِهْتُمُوهُ ۚ وَاتَّقُوا اللَّـهَ ۚ إِنَّ اللَّـهَ تَوَّابٌ رَّحِيمٌ﴿١٢﴾

Enyi walioamini! Wanaume wasiwafanyie dhihaka na kudharau wanaume wengineo asaa wakawa bora kuliko wao, wala wanawake kwa wanawake wengineo, asaa wakawa bora kuliko wao. Na wala msifedheheshane kwa kutukanana na wala msiitane majina (mabaya) ya utani. Ubaya ulioje kuita jina la ufasiki baada ya iymaan. Na yeyote asiyetubu, basi hao ndio madhalimu. Enyi walioamini!  Jieupusheni sana na dhana kwani hakika baadhi ya dhana ni dhambi. Na wala msifanyiane ujasusi, na wala wasisengenyane baadhi yenu wengineo. Je, anapenda mmoja wenu kwamba ale nyama ya nduguye aliyekufa? Basi mmelichukia hilo! Na mcheni Allaah! Hakika Allaah ni Mwingi wa kupokea tawbah, Mwenye kurehemu. [Al-Hujuraat: 11-12]

 

Hivyo haifai kabisa kumvunjia heshima ndugu mwenzio au kumsengenya. Makatazo haya pia yamekuja katika mafunzo ya Nabiy (Swalla Allah ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

عن أنس قال: قال رسول الله صلى الله عليه وسلم (( لما عرج بي مررت بقوم لهم أظفار من نحاس يخمشون وجوههم وصدورهم، فقلت: من هؤلاء يا جبريل؟)) قال: هؤلاء الذين يأكلون لحوم الناس ويقعون في أعراضهم"

Kutoka kwa Anas (Radhwiya Allahu ‘anhu) kwamba Nabiy (Swalla Allahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

"Nilipopandishwa mbinguni (Siku ya Israa na Mi’raaj) nilipita kwa watu ambao walikuwa wana kucha za shaba nyeupe wakijichana nyuso zao na vifua vyao. Nikauliza: Nani hawa ee Jibriyl? Akasema: Hawa ni watu ambao wamekula nyama za binaadamu na kuwavunjia heshima zao)) [Abu Daawud]

 

 

Allaah Anajua zaidi

 

Share