Swahaba Yupi Aliyeoshwa Na Malaika?

SWALI:

 

Assalaam Alaykum,

 

Tafadhali niambie kama kuna swahaba yeyote aliyezikwa na malaika. Shukran.


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu Swahaba aliyezikwa na Malaika.

 

Hakika ni kuwa hakuna Swahaba aliyezikwa na Malaika bali yupo Swahaba aliyeoshwa na Malaika, naye anaitwa Handhwallah bin ‘Abdillaah ar-Raahib (Radhiya Allaahu 'anhu) kutoka katika kabila la ‘Aws. Yeye alioshwa na Malaika kwa sababu ilipotangazwa vita vya Uhud ilikuwa ni siku ya pili yake ya ndoa yake. Aliposikia mwito tu wa kupigana jihaad alitoka kukimbilia vitani bila ya kuoga (ghuslu) janaba. Hivyo imesemekana kwamba alipouliwa vitani, Maswahaba walimuona uso wake na mwili wake umejaa matone ya maji na alipoulizwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  alisema kuwa Malaika wamemuosha.

 

Swahaba mwengine ni yule ambaye jeneza lake lilibebwa na Malaika, naye ni Sa‘ad bin Mu‘aadh (Radhiya Allaahu 'anhu). 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share