Aliy (رضي الله عنه) Alikuwa Wapi Alipofariki ‘Uthmaan (رضي الله عنه) Na Kwa Nini Hakumzika?

SWALI:

 

Asssalam aleykum wallah ma tullah wabalakati, ndugu zangu ktk imani mimi nina tatizo juu ya kifo cha uthmaan bin affan radhia llahu anhu kama ifuatavyo: pindi uthmaan radhia lahu anhu alipozungukwa na wanafiki kwa muda wa siku arobaini na wakamnyima hata tone la maji SWALI ally radhia lahu anhu alikuwa wapi? maana uthumani radhia llahu anhu alikuwa madina swali la pili alipata taarifa kuwa Khaliyfah uthmaan kazungukwa na wanafiki mpaka kakosa maji na mpaka uthmani alikuwa akimuulizia kuwa yuko wapi ally na ally radhia lahu anhu alipata taarifa hizi za kuuliziwa na Khaliyfah wake ikafikia hatua ally alipopata hizi taarifa akamtumia uthmaan maji lakini maji yale aliyatumia yakaisha sasa kwa nini hakumtumia maji mengine na tayari alikuwa hanayo habar juu hili.

 

SWALI LAKE PILI:

 

asssalam aleykum wallah ma tullah wabalakati,ndugu zangu ktk imani.SWALI ally radhia llahu anhu aliwatoa watoto wake wawili wakamlinde uthmaan bin affan radhia llahu anhu hassan na hussein sasa swali linakuja wao walikuwa wakilinda vipi walikuwa wakila nini NA nani alikuwa akiwaletea pale chakula kwa maana wao wangekuwa wanakula basi hata uthmaan bin affan radhia llahu anhu asinge kosa hata maji kwa maana tayar alikuwa na watu ambao wanamlinda kwa hivyo walikuwa wanajua kila kitu kuhusu Khaliyfah wao kama ana maji au laa?  YAANI kazi ya walinzi ni kujua yule wanae mlinda anaendelea vipi sasa iwapo walikuwa wanalinda halafu hawajui khakifa wao anakula nini na wanaona kabisa hatoki hata nje kwa ajiri ya wale wanafiki.KWA NINI ALLY RADHIA RAHU ANHU HAKUSHIRIKI KUMZIKA UTHMAAN BIN AFFAN RADHIA RAHU ANHU JE ALIWAOGOPA WALE WANAFIKI? KIPINDI CHA UKHALIYFAH WA UTHMAAN  BIN AFFAN RADHIA RAHU ANHU JE ALLY RADHIA RAHU ANHU ALIKUWA NA CHEO CHOCHOTE KTK UKHAALIFA WA UTHMAAN BIN AFFAN RADHIA RAHU ANHU.


 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu kuuliwa kwa ‘Uthmaan bin ‘Affaan (Radhiya Allaahu ‘anhu).

 

Wakati Khaliyfah “Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu) amezungukwa ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alikuwa yupo Madiynah. Bila shaka ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alipata taarifa za kuzungukwa Khaliyfah na ndio akawapeleka watoto wake, al-Hasan na al-Husayn (Radhiya Allaahu ‘anhuma) wamlinde asivamiwe na watu hao wabaya. Na si hao wawili pekee waliokuwa wakifanya shughuli hiyo bali pia Maswahaba wengine wakubwa walisaidia katika ulinzi huo. Hakika ni kuwa ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu) hakumuulizia ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) kwa kuwa yeye mwenyewe alikwenda kwake na kumtaka Khaliyfah aruhusu kupigwa kwa hao mujrimina (wahalifu) lakini ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu) akakataa hilo.

 

Kwa kuwa kulikuwa na walinzi nje ya nyumba ya Khaliyfah, Khaliyfah alikuwa anapelekewa maji na chakula chake na watu wake. Na ni ajabu watu kuzua mambo ambayo hayapo ili kuwatia makosani Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) wasiokuwa nayo. 

 

Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) walikuwa wanalinda nyumba kama vile mlinzi anavyolinda nyumba au sehemu ya duka aliyopatiwa kazi. Na kwa kuwa walikuwa nje ya nyumba walikuwa wanaletewa chakula na maji na hivyo kuweza kula na kunywa kama wanavyokula na kunywa watu wa kawaida.

 

Na ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu) kabla ya kuuliwa na wahalifu aliwaita Maswahaba na watu wa Madiynah na kuwahutubia na miongoni mwa waliokuwepo ni ‘Aliy bin Abi Twaalib (Radhiya Allaahu ‘anhu). Na siku ile aliyouliwa ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu) walisimama kikundi cha Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) kwa kumuosha, kumkafini, kumswali na kumzika, na miongoni mwao aliyekuwa mstari wa mbele katika yote hayo ni ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) {Tazama al-Bidaayah wan Nihaayah cha Ibn Kathiyr, Mjalada wa 7, ukurasa wa 199 na pia ‘Uthmaan bin ‘Affaan (Radhiya Allaahu ‘anhu), Dkt. ‘Aliy Muhammad Muhammad asw-Swallaabiy, ukurasa wa 400}.

 

‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) si muoga wala hakumuogopa yeyote katika maisha yake yote katika jambo la haki. Ushujaa wake ulijulikana sana kuanzia wakati wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mpaka kufa kwake, hakurudi nyuma hata mara moja. Ukweli ni kuwa ni ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) aliyemwambia Khaliyfah kuwa ana watu mia tano (500) wako tayari kupigana na wahalifu hao waovu. ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu) alimjibu: “Allaah Akujaze kheri, sipendi damu imwagike kwa ajili yangu” (Ibn ‘Asaakir, Taarikh Dimishq, uk. 403). Na hilo ndilo jibu alilokuwa akimjibu kila aliyetaka kumtetea ili asipatikanwe na balaa ya aina yoyote ile.

 

Katika uKhaliyfah wa ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu), ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) alikuwa na dauru muhimu sana katika shuura ya Khaliyfah.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share