Skip navigation.
Home kabah

Kwenda Hajj Na Wazazi Ikiwa Mume Hataki Inafaa?

 

SWALI:

ASSALAM ALLAYKUM;

MIMI NI MWANAMKE MWENYE MUME NA NINA YA KWENDA

HIJA  LAKINI KILA NIKIMSHAURI MUME WANGU KUHUSU HILO  ANAONEKANA NI MZITO NA UWEZO ANAO. SASA ITAKUWA VIBAYA KAMA NITAKWENDA MIMI NA WAZAZI WANGU

 

 



JIBU:

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

Hakuna ubaya kabisa kwenda kutekeleza nguzo yako ukifuatana na wazazi wako. Bila shaka utakuwa umekusudia baba na mama yako, hivyo baba yako anakutosheleza kuwa ni mahram wako na ni jambo jema kabisa.

Kilichokuwa muhimu ni upate ruhusa ya mume vilevile jitahidi kumpa makala za Hajj zilizokuwemo humu AL HIDAAYA apate kusoma atambue umuhimu wa kutekeleza ibada hiyo na atambue kuwa kudharau amri za Mola wake na hali anao uwezo ni maasi makubwa ya kupelekea ukafiri, kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema:

 ((وَلِلّهِ عَلَى النَّاسِ حِجُّ الْبَيْتِ مَنِ اسْتَطَاعَ إِلَيْهِ سَبِيلاً وَمَن كَفَرَ فَإِنَّ الله غَنِيٌّ عَنِ الْعَالَمِينَ))

 

 

((Na kwa ajili ya Allah imewajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezae njia ya kwendea. Na atakayekanusha basi Allah si mhitaji kwa walimwengu)) [Al-'Imraan:96-97]

Ibn 'Abbaas (Radhiya Allahu 'anhu), Mujaahid na wengineo wamesema kuhusu Aayah hiyo kwamba: "Yeyote mwenye kukanusha umuhimu wa Hajj anakuwa ni kafiri na Allah yuko mbali naye kabisa (Hamuhitajii kwa chochote)" [Tafsiyr Ibn Kathiyr]  

Muislamu asitegemee kupewa umri zaidi, hakuna ajuaye lini ataondoka duniani na kama alivyosema  'Umar ibn Khatwtwwaab (Radhiya Allahu 'anhu) "Yeyote mwenye uwezo wa kutekeleza Hajj kisha asitekeleze, atakapofariki hatokuwa na tofauti baina yake na Yahudi au Naswara" [Hii ina isnaad sahihi inayofika kwa 'Umar – Al-Hilya 9:252 – imenukuliwa katika Tafsiyr ya Ibn Kathiry]

Kwa hiyo tunaona hatari ya kudharau kutekeleza nguzo hii kwa mwenye uwezo kuwa atakapofariki hatokuwa katika dini ya Uislamu, bila shaka hakuna mmoja wetu atakayependa kuwa na hatima mbaya kama hiyo.

Utakapojaaliwa kufika huko umuombee sana mumeo Allah Ampe imani ya kupenda kutekeleza tuliyoamrishwa katika dini yetu na tafadhali usitusahau na sisi kwa du'aa huko. 

Tunakuombea Hajj Mabruur wa Dhambim-maghfuur (Hijja ya kukubaliwa na dhambi za kughufuriwa)

Na Allah Anajua zaidi