Atekeleze Fardhi Ya Hajj Kwanza Au Aoe?

 

Atekeleze Fardhi Ya Hajj Kwanza Au Aoe?

 

 Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Kwanza sina budi kumshukuru Allaah ambae ameumba mbingu na arthi, na yeye ni mjuzi wa kila kiu. Vile vile natuma salamu zangu kwako kwa kusema Assalam alaykum.

 

Mwalimu naomba kuuliza swali langu kama ifuatavyo;

 

Kwa mujibu wa dini ya Kiislamu neno Ndowa ni sunna, na vile vile ukitizama neno  hijja ni nguzo ya tano ya Uislam na pia ni Fardhi. Sasa je mwalimu mimi nnapesa taslimu za kunitoshelezea kwenda kuhiji, lakini mimi ni kijana ambaye sina mke, sasa je nnaweza kuhijji kwa kuwa Hijja ni fardhi au kwanza nifunge ndowa? Natumai swali langu litajibiwa vizuri na kwa ufasaha zaidi.

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

 

Mara nyingi huchanganyikiwa kuhusu mas-ala ya ndoa kwani wengi wetu huchukua kuwa ni Sunnah tu, hivyo mtu aweza kuoa au kuacha kufanya hivyo. Uhakika wa mambo sivyo kabisa kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ametoa amri kwetu tuoe na Akaileta kwa njia ya lazima. Hiyo ni:

 

وَأَنكِحُوا الْأَيَامَىٰ مِنكُمْ وَالصَّالِحِينَ مِنْ عِبَادِكُمْ وَإِمَائِكُمْ ۚ إِن يَكُونُوا فُقَرَاءَ يُغْنِهِمُ اللَّـهُ مِن فَضْلِهِ ۗ وَاللَّـهُ وَاسِعٌ عَلِيمٌ ﴿٣٢﴾

Na waozesheni wajane miongoni mwenu na walio Swalihina kati ya watumwa wenu wanaume na wajakazi wenu. Wakiwa mafakiri Allaah Atawatajirisha katika fadhila Zake. Na Allaah Mwenye Wasaa, Mjuzi wa yote. [An-Nuwr: 32]

 

Na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

"Yeyote mwenye kukengeuka na Sunnah yangu si katika mimi [Al-Bukhaariy na Muslim] Ndoa ikiwa ndani yake.

 

 

Kwa minajili hiyo, ‘Ulamaa wamegawanya ndoa katika sehemu tatu:

 

  1. Faradhi kwa yule asiyeweza kujizuia.

 

  1. Sunnah iliyohimizwa kwa Muislamu anayejiweza.

 

  1. Haraam kwa asiyeweza kumuweka mke ima kwa kutoweza kumtimizia tendo la ndoa na kadhalika.

 

Kuhusu kadhiya yako inategemea uko katika kundi gani. Ikiwa uko katika kundi la mwanzo itakuwa ni aula mwanzo uoe ili usiingie katika zinaa baadaye utakwenda Hijjah. Ama ukiwa katika aina ya pili au ya tatu, utahitajika mwanzo kwenda Hijjah, kisha uoe.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share