Mume Hatimizi Haki Kwa Mke Mdogo Kwa Vile Hakuzaa Naye. Bali Anatimiza Kwa Mke Mkubwa Pekee. Je Shari’ah Inasemaje?

SWALI:

 

Asalaam alaikum warahmatulahi wabarakatu. Kuna hukumu gani ama kuna malipo gani ya Mwanamke ambaye ameishi na mumewe kwa miaka sita, kisha katika miaka hiyo sita huyo Mume ana Mke mwengine lakini anabagua anaangalia upande mmoja au sehemu mmoja kwa vile kazaa nae huyo Bi mkubwa? Hakumtizama huyo mke mdogo kwa lolote kama, chakula, mavazi na haki zote za Mke kwa jumla? Kuna hukumu gani hapo? Na kuna dua gani mwanamke aombe ili amshatakie Allah subhanau wataala. Shukra

 


 

 

 

JIBU:

 

Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu mume kutotimiza haki kwa mkewe mdogo

 

.

Inafaa ieleweke kuwa mume ana majukumu makubwa kwa mkewe aliyemuoa akiwa ni peke yake au ni zaidi ya mmoja. Allaah Aliyetukuka Anasema:

Wanaume ni wasimamizi wa wanawake, kwa kufadhiliwa na Allaah baadhi yao juu ya baadhi, na kwa mali yao wanayoyatoa” (an-Nisaa’ [4]: 34).

Ndio ikiwa mwanamme hana uwezo wa kuwaweka wake wawili au zaidi, Qur-aan ikamnasihi:

Na ikiwa mnaogopa kuwa hamtowafanyia mayatima uadilifu, basi oeni mnaowapenda katika wanawake, wawili au watatu au wanne. na mkiogopa kuwa hamwezi kufanya uadilifu, basi mmoja tu” (an-Nisaa’ [4]: 3).

 

Mas-ala wa uzazi yote yapo katika mikono ya Allaah Aliyetukuka. Na mara nyingine inakuwa ni ugonjwa unaompata mwanamme au mwanamke kumfanya asiweze kuzaa. Badala ya mume kumchukia mkewe anatakiwa ajaribu kumpeleka kwa matabibu na madaktari waliobobea katika magonjwa ya uzazi ili apate matibabu.

 

Ni makosa kwa mume kubagua baina ya wake zake, kwani kufanya hivyo ni dhuluma na dhuluma itakuwa ni giza Siku ya Qiyaamah. Na Siku hiyo kwa yule mume ambaye alikuwa akimpendelea mke juu ya mke mwengine atakuja mbele ya watu bega lake moja likiwa limeinama.

 

Ama kuhusu du’aa hakuna maalumu bali ni vile utakavyoomba na unavyotaka awe. Hata hivyo, ingekuwa ni bora zaidi mke kumuombea mumewe apate fahamu na arudi katika hisia zake na atekeleze majukumu yake. Kwani unapomuombea aliye kudhulumu hiyo inakuwa ni laana na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema kuwa du’aa ya mwenye kudhulumiwa haina pazia wala kizuizi na Allaah Aliyetukuka.

 

Nasaha yetu kwa mke ni kuwa ajaribu mwanzo kutafuta njia za kupata suluhu. Nayo anaweza kufanya yafuatayo:

 

1.     Kujaribu kuzungumza naye kwa njia nzuri ili atekeleze majukumu yake kwa njia iliyo nzuri.

 

 

2.     Ikiwa amekataa kukusikiliza au kuja kuzungumza nawe inabidi uitishe kikao baina ya mke, mume, wazazi au wawakilishi wa mke na mume. Na ikiwa kweli wanataka suluhu basi Allaah Aliyetukuka Atawatengenezea mambo yao.

 

 

3.     Ikiwa hakukupatikana ufumbuzi wowote itabidi uende kwa Qaadhi au Shaykh aliyewaozesha au Shaykh yeyote mwenye ucha Mngu, elimu na uadilifu ili aweze kuamua na kurekebisha tatizo hilo.

 

 

4.     Ikiwa imeshindikana kabisa basi akupatie talaka ili uweze kutizama maisha yako kwa kuolewa na mwengine.

 

 

 

Tunakutakia kila la kheri katika tatizo hilo na tunakuombea upate ufumbuzi wa haraka na wa kheri.

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

 

Share