Kumsomea Qur-aan Maiti Akishazikwa Kama Suwrah Ikhlaasw Na Yaasiyn Inajuzu?

 

Kumsomea Qur-aan Maiti Akishazikwa Kama Suwrah Ikhlaasw Na Yaasiyn Inajuzu?

 

Alhidaaya.com

 

 

 

SWALI:

 

Nauliza jee maiti akeshazikwa inafaa kumuombea dua hapo kaburini au kumsomea Qurani hasa ikhlas mara 11 au yaasiin? Asante.

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

 

Ili sisi tuweze kumfaidisha maiti aliyekufa inabidi tufuate muongozo wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na kwenda kinyume na maagizo yake ni kujibebesha mzigo wa madhambi ya bure. Ada ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipomaliza kuzika alikuwa anasimama kaburini na husema:

 

"Muombeeni msamaha ndugu yenu kwa Allaah na amfanye thabiti kwani hivi sasa anahojiwa" [Abu Daawuud].

 

Tunajifunza kutokana na Hadiyth ya hapo juu makosa mbali mbali yenye kufanywa na watu wengi wanaposimama makaburini mmoja wao anasimama na kuanza kuomba dua kwa sauti kubwa na wengine kuitikia Aamiyn. Au baada ya maiti kufukiwa anatokeza mtu na kijitabu chake cha Talaqini na kumsomea Talaqini!

 

Ilivyo ni kuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliwaamrisha Swahaba zake (Radhwiya Allaahu ‘anhum) wamtakie maghfira maiti wao kila mmoja katika nafsi yake na kila mmoja amuombe Allaah aliyetukuka Amthibitishe huyo maiti kwa kauli thabiti pindi atakapoulizwa na Malaika wawili.

 

Pia ni makosa kumlakinia maiti majibu atakayoulizwa na Malaika kaburini. Hili ni jambo ambalo halikufanywa na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wala Swahaba zake (Radhwiya Allaahu ‘anhum). Kwa hiyo, tusiwe ni wenye kufanya mambo ambayo ni kinyume na ilivyofundisha Dini yetu Tukufu.

 

Pia ni jambo ambalo limezoeleka kwetu sisi wengi kusema: Al-Faatihah kwa roho ya fulani au kusoma Suratu Yaasiyn (Suwrah ya 36) katika kaburi la maiti au kusoma Suwrah Al-Ikhlaasw (Qul Huwa Allaahu Ahad) mara 11, au baadhi ya ayah au Suwrah katika Qur-aan. Hapana shaka kuwa mambo haya ni kinyume kabisa na sheria ya Dini ya Allaah Aliyetukuka. Hakika hakuna Hadiyth hata moja inayoruhusu kusomwa kwa Suwrah Al-Faatihah kumi na moja au Suwrah Al-Ikhlaasw au Suwrah Al-Yaasin kaburini. Nasaha yetu kwa ndugu zetu waachane na hilo kabisa kwani ni kwenda kinyume na Sunnah ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).

 

 

Mambo ambayo yanamfaa maiti ni:

 

 

1.     Kwa watoto wake wema kumuombea duaa.

2.     Ikiwa ana deni kwa wanadamu alipiwe.

3.     Ikiwa adaiwa funga ya faradhi watu wake wamfungie.

4.     Watu wake wamtolee sadaka kwa niaba yake.

5.    Ikiwa aliweka nadhiri ya kufanya jambo la halali na hakuweza  kulifanya basi watu wake wamtekelezee.

6.     Kumfanyia Hajj au ‘Umrah ikiwa hakufanya.

7.     Waislamu kwa jumla wawe wanaombeana duaa.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

Share