Wanaojiita Waalimu Huchukua Vitu Kwa Wanaowatibu Na Kuwalisha Yamini Kuwa Wasiseme Na Wala Wasiviulize Tena.

 

Wanaojiita Waalimu Huchukua Vitu Kwa Wanaowatibu Na Kuwalisha Yamini Kuwa Wasiseme Na Wala Wasiviulize Tena.  

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

Assalamu alaykum,

Kuna Wanaojiita waalimu wanumuambia mgonjwa una majini wahitaji kutolewa, baada ya kukusomea anamwambia mgonjwa kama amevaa pete azitowe azitie kwenye kijitunga na nguo mbili hivi anazozipenda sana kisha anamlisha yamini kuwa amezitoa na hataziuliza tena kisha asimueleze mtu. Hizo ni kafara za majini. 

Vipi mambo haya??

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aala) Rabb wa walimwengu, Swalaah na Salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho

 

 

Hakika ni kuwa waalimu hawafai kupatiwa vitu kama pete baada ya kumsomea mgonjwa wala kutaka kupatiwa vitu katika vijitunga. Huo ni udanganyifu na Muislamu hafai kuwa mdanganyifu.

 

Ni nasaha kwetu kwa Waislamu wanapokuwa wagonjwa na ikashukiwa kuwa amekumbwa na jini basi aende kwa Mwalimu au Shaykh Muislamu mwaminifu na mcha wa Allaah ambaye atamsaidia na wala sio yule mwenye kumuingiza katika shirki ya aina moja au nyengine.

 

Hao ‘Maalim’ na ‘Maustaadh’ au ‘Mashekhe’ wa aina hiyo uliowataja, ni wale watu wadanganyifu na wasio na Iymaan ambao labda wanajua Aayah chache na kuzitumia kudanganyia watu ili kupata chakula chao na kushibisha njaa zao. Yote inasababishwa na watu kutotaka kujituma na kufanya kazi na kubuni hila na njia za mkato za kuwapatia chumo rahisi la haraka.

 

Wapo wengine pia wenye kuwatengenezea Waislamu makombe na kuwafungia baadhi ya Aayah na maneno ya Kiarabu yasiyojulikana ili ziwakinge. Na kuna wengine waliojenga majumba na kutajirika kwa kazi kama hizo za kuwadanganya Waislamu dhaifu wajinga wasiojua Dini yao na wasiojua njia za kufuata wanapougua.

 

Ni muhimu Waislamu wajihadhari na mashekhe na maalim na maustaadh waongo kama hao. Na pia watu wawabainishe na kuwapiga vita kwa kila njia ili ufisadi kama huo utokomee katika jamii za Kiislamu.

 

 

Na Allaah Anajua zaidi.

 

Share