Mume Kumlazimisha Mke Kuvaa Niqaab Je, Inajuzu?

 

Mume Kumlazimisha Mke Kuvaa Niqaab Je, Inajuzu?

 

Alhidaaya.com

 

 

Swali:

 

Asalam Aleykum Warahmatullah Wabarakat

 

Ninavyojua ni kwamba mwanamke anafaa kujistiri kila pahali isipokuwa uso na vitanga vya mikono. Sasa nataka kuuliza ni nini hukumu ya kuvaa hijab na niqab, na jee inafaa mume wako kukulazimisha kuvaa niqab?

Shukran.

 

 

Jibu:

 

AlhamduliLLaah - Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salaam zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Kuna ikhtilaaf za ‘Ulamaa kuhusu mas-ala haya.  Kuna waliosema kwamba kujifunika kwa mwanamke ni kujifunika kila sehemu ya mwili isipokuwa uso na viganja vya mikono. Lakini wengine wameona kwamba ni wajib mwanamke kujifunika kila kitu mpaka uso kutokana na dalili katika Qur-aan na Sunnah. Dalili kutoka katika Qur-aan ni kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاءِ الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ۚ ذَٰلِكَ أَدْنَىٰ أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٥٩﴾

Ee Nabiy! Waambie wake zako, na mabinti zako, na wanawake wa Waumini wajiteremshie jilbaab zao. Hivyo kunapeleka karibu zaidi watambulikane (kwa heshima) wasiudhiwe. Na Allaah daima ni Mwingi wa kughufuria, Mwenye kurehemu. [Al-Ahzaab: 59]

 

Jilbaab ni guo analopaswa  mwanamke kulivaa juu ya khimaar, kwa maana kutoka kichwani na inashuka kumfunika uso wake.

 

Na 'Aliy bin Abiy Twalhah amerepoti kwamba Ibn 'Abbaas amesema kwamba Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Amewaamrisha wanawake waumini wajifunike nyuso zao kutoka vichwani mwao wakiacha jicho moja tu, wanapotoka nje ya nyumba zao kwa ajili ya kutafuta mahitajio yao. [Tafsiyr Ibn Kathiyr: 8: 45].

 

Na pia Hadiyth kadhaa ni dalili kwamba wanawake wanapaswa kujifunika kila kitu mpaka uso. Baadhi ya Hadiyth hizo ni:

 

Kutoka kwa ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) kwamba  ilipoteremeshwa kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَىٰ جُيُوبِهِنَّ ۖ  

Na waangushe khimaar (shungi) zao mpaka vifuani mwao… [An-Nuwr: 31]

         

Wanawake wa Ki-Muhaajirina walichana na kukata gauni zao pembeni ili kufunikia nyuso zao )) [Al-Bukhaariy]

 

Vile vile kuhusu wanawake wanaokwenda kutelekeza ‘Umrah au Hajj wakaingia katika Ihraam ni kauli ya Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

 

((لَا تَنْتَقِبُ الْمَرْأَةُ الْمُحْرِمَةُ وَلَا تَلْبَسُ الْقُفَّازَيْنِ))

((Mwanamke katika Ihraam asivae niqaab wala glavu)) [Al-Bukhaariy]

 

Na pia katika safari ya Hajj, 'Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) amesema: "Wapandaji (wanaume) walipita mbele yetu tukiwa na Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Walipokuwa sambamba mbele yetu tuliteremsha utaji (shungi) zetu usoni na vichwani mwetu, kisha walipotoweka tulijifunua)) [Abu Daawuwd na Ibn Maajah]

 

Hii inaonyesha kwamba wanawake walipokuwa nje ya Ihraam walikuwa wakijifunika nyuso zao.

 

Nasaha zetu ni kwamba kwanza mshukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) kwa kukujaalia mume ambaye anakutakia jambo la kheri na stara. Tambua kuwa wako wapi siku hizi wanaume kama hao waliokuwa na hima ya kutaka wake zao wabakie katika stara na heshima? Ni wachache sana, kwa sababu utasikia katika jamii mwanamke anataka  kujifunika uso lakini   mume wake hataki. Hivyo inakuwa ni mtihani kwa mwanamke. Na baya zaidi ni kwamba waume wengine hata vazi la hijaab  hawataki wake zao wavae. Basi ni neema kwako kujaaliwa mume anayekupendelea sitara.   

 

Kwa hiyo mche Allaah ('Azza wa Jalla) kwa kuitikia amri mbili; amri ya Allaah ('Azza wa Jalla) na amri ya mume wako. Bila shaka hii ni kheri kwako, kwani mumeo hakuamrishi jambo ovu bali ni jambo jema lenye faida tele nawe. Mojawapo ya faida ni  itakupunguzia usumbufu na maudhi njiani kwa wale wahuni na wenye uchu wa zinaa. Na wewe ndiye utakayekuwa ni sababu ya kuwazuia kutazama yaliyo haramu kwao hivyo utajiepusha na dhambi hizo.

 

Pia kumtii mume wako bila shaka itamridhisha na kumfurahisha mumeo na azidi kuwa na mapenzi na wewe na uzidi kuijenga nyumba yako katika furaha na amani.  

 

Na Allaah Anajua zaidi

 

 

Share