042-Lu-ulu-un-Manthuwrun: Haingii Jannah Mtu Ila Kwa Iymaan, Kupendana na Kutoleana Salaam

Lu-ulu-un-Manthuwrun

(Mkusanyiko Wa Hadiyth Mbali Mbali Na Mafunzo Yake)

 

Hadiyth Ya  42

 

Haingii Jannah Mtu Ila Kwa Iymaan, Kupendana na Kutoleana Salaam

 

Alhidaaya.com

 

 

 

 

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ (رضي الله عنه) قَالَ: قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ: ((وَالَّذِي نَفْسِي بِيَدِهِ لاَ تَدْخُلُونَ الْجَنَّةَ حَتَّى تُؤْمِنُوا، وَلاَ تُؤْمِنُوا حَتَّى تَحَابُّوا، أَوَلاَ أَدُلُّكُمْ عَلَى شَيْءٍ إِذَا فَعَلْتُمُوهُ تَحَابَبْتُمْ؟  أَفْشُوا السَّلاَمَ بَيْنَكُمْ)) مسلم

Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah (رضي الله عنه) kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Naapa kwa Ambaye nafsi yangu imo Mikononi Mwake! Hamtoingia Jannh mpaka muamini, wala hamtoamini mpaka mpendane. Je, niwajulishe jambo mtakapolifanya mtapendana? Enezeni Salaam baina yenu)). [Muslim]

 

 

Mafunzo Na Mwongozo:

 

 

1. Kutekeleza amri ya kuamkiana kwa maamkizi ya Kiislamu. Anasema Allaah (سبحانه وتعالى):

 

 وَإِذَا حُيِّيتُم بِتَحِيَّةٍ فَحَيُّوا بِأَحْسَنَ مِنْهَا أَوْ رُدُّوهَا ۗ إِنَّ اللَّـهَ كَانَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ حَسِيبًا ﴿٨٦﴾

Na mtapoamkiwa kwa maamkizi yoyote, basi itikieni kwa yaliyo mazuri zaidi kuliko hayo au yarudisheni hayo hayo. Hakika Allaah daima ni Mwenye kuhesabu kila kitu. [An-Nisaa: 86]

 

2. Maamkizi ya Kiislamu yana kheri na baraka, ndio maana Allaah (سبحانه وتعالى) Akaamrisha mtu anapoingia nyumbani kwake ayatamke, hata kama hakuna mtu ndani ya nyumba. Anasema Allaah (سبحانه وتعالى):

 

  ۚ فَإِذَا دَخَلْتُم بُيُوتًا فَسَلِّمُوا عَلَىٰ أَنفُسِكُمْ تَحِيَّةً مِّنْ عِندِ اللَّـهِ مُبَارَكَةً طَيِّبَةً ۚ  

Mtakapoingia majumbani toleaneni salaam; maamkizi kutoka kwa Allaah, yenye Baraka, mazuri.  [An-Nuwr (24: 61)]

 

3. Jannah haipatikani ila kuweko na Iymaan, na Iymaan haikamiliki ila Muislamu ampendelee nduguye anayoyapenda nafsi yake. [Rejea Hadiyth namba 21].

 

 

4. Iymaan haikamiliki ila kwa matendo na amri zake.

 

 

5. Maamkizi ya Kiislamu katika shariy’ah na inavyopasa kuamkiana ni “Assalaamu ‘Alaykum” Au: “Assalaamu ‘alaykum wa RahmatuLLaah” Au: “Assalaamu ‘alaykum wa RahmatuLLaahi wa Barakaatuh”  na si vinginevyo kutokana na Hadiyth:

 

عَنْ عِمْرَانَ بْنِ حُصَيْنٍ  رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُمَا  قَالَ: جَاءَ رَجُلٌ إِلَى النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ فَقَالَ: "السَّلامُ عَلَيْكُمْ" فَرَدَّ عَلَيْهِ ثُمَّ جَلَسَ فَقَالَ النَّبِيُّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ: ((عَشْرٌ))  ثُمَّ جَاءَ آخَرُ فَقَالَ: "السَّلامُ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَةُ اللَّهِ"  فَرَدَّ عَلَيْهِ فَجَلَسَ فَقَالَ: ((عِشْرُونَ)) ثُمَّ جَاءَ آخَرُ فَقَالَ: "السَّلامُ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَةُ اللَّهِ وَبَرَكَاتُهُ" فَرَدَّ عَلَيْهِ فَجَلَسَ فَقَالَ : ((ثَلاثُونَ)) رواه ابو داود والترمذي و قال حديث حسن

'Imraan bin Al-Huswayn (رضي الله عنهما) amesimulia: "Mtu mmoja alikuja kwa Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) akasema: "Assalaamu 'Alaykum." Akamrudishia (Salaam) kisha yule mtu akaketi. Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) akasema: ((Kumi)) [Kwa maana amepata thawabu kumi]. Kisha akaja mtu mwengine, akasema: "Assalaamu 'Alaykum wa RahmatuLLaah." Naye akamrudishia, kisha yule mtu akaketi, Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) akasema: ((Ishirini)). Kisha akaja mtu mwingine akasema: "Assalaamu 'Alaykum wa RahmatuLLaahi wa Barakaatuh." Naye akamrudishia kisha akasema ((Thelathini)) [Imesimuliwa na Abu Daawuwd na At-Trimidhiy na akasema Hadiyth Hasan na ameisahihisha Al-Albaaniy katika Swahiyh Abiy Daawuwd (5195), Swahiyh At-Tirmidhiy (2869)]

 

 

Na haifai kuyafupisha katika maandishi kama ilivyozoeleka katika mitandao ya kijamii; baadhi ya watu kuandika: (AA) na vinginevyo. ‘Ulamaa wetu wamekemea jambo hili kwamba ni kinyume na maamrisho ya Qur-aan na Sunnah, na pia ni kujikosesha thawabu na fadhila zake.

 

 

5. Kutoleana Salaam ni sababu au chanzo cha kutambulisha na kujuana baina ya Waislamu, na kutoa Salaam kwa mtu mmoja kunaweza kuwafikia maelfu ya Waislamu na kupata fadhila, thawabu, na manufaa yake.

 

 

6. Maamkizi ya Kiislamu ni funguo za mapenzi baina ya Waislamu.

 

 

7. Maamkizi ya Kiislamu ndiyo yanayotofautisha baina ya Waislamu na makafiri.

 

 

8. Maamkizi ya Kiislamu yanalingana sawa na maana ya ‘Uislamu’ yaani amani.  

 

 

9. Fadhila ya Iymaan ni kumuingiza mtu Jannah.

 

 

 

 

Share