10-Hakika Shirki Ni Dhulma Kubwa Mno! - Kumhusisha Rasuli wa Allaah Swalla Allaahu 'Alayhi Wa Aalihi Wa Sallam Katika Kumshirikisha Allaah.

 

إِنَّ الشِّرْكَ لَظُلْمٌ عَظِيمٌ

Hakika Shirki Ni Dhulma Kubwa Mno!

 

10-Kumhusisha Rasuli wa Allaah Swalla Allaahu 'Alayhi Wa Aalihi Wa Sallam

Katika Kumshirikisha Allaah. 

 

Alhidaaya.com

 

 

 

Baadhi ya Waislamu wanamhusisha Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika kumshirikisha Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) kwa namna mbali mbali. Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) na Rasuli wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wamekemea mno kwa dalili kadhaa miongoni mwazo ni: 

 

Hadiyth ya Abuu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba ilipoteremshwa kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa):

وَأَنذِرْ عَشِيرَتَكَ الْأَقْرَبِينَ ﴿٢١٤﴾

Na onya (ee Muhammad Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) jamaa zako wa karibu. [Ash-Shu’araa: 214]

 

 

Alisimama Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akasema:

 

 ((يَا مَعْشَرَ قُرَيْشٍ!)) أَوْ كَلِمَةً نَحْوَهَا ((اشْتَرُوا أَنْفُسَكُمْ، لاَ أُغْنِي عَنْكُمْ مِنَ اللَّهِ شَيْئًا، يَا بَنِي عَبْدِ مَنَافٍ لاَ أُغْنِي عَنْكُمْ مِنَ اللَّهِ شَيْئًا، يَا عَبَّاسُ بْنَ عَبْدِ الْمُطَّلِبِ لاَ أُغْنِي عَنْكَ مِنَ اللَّهِ شَيْئًا، وَيَا صَفِيَّةُ عَمَّةَ رَسُولِ اللَّهِ لاَ أُغْنِي عَنْكِ مِنَ اللَّهِ شَيْئًا ، وَيَا فَاطِمَةُ بِنْتَ مُحَمَّدٍ سَلِينِي مَا شِئْتِ مِنْ مَالِي لاَ أُغْنِي عَنْكِ مِنَ اللَّهِ شَيْئًا))

((Enyi maashara Quraysh!)) Au mfano wa maneno hayo ((Okoeni nafsi zenu, mimi sitowafaa kwa chochote mbele ya Allaah! Enyi Baniy ‘Abdi Manaaf! Mimi sitowafaa kwa chochote mbele ya Allaah!  Ee ‘Abbaas bin ‘Abdil-Mutwalib! Sitokufaa  kwa chochote mbele ya Allaah! Na ee Faatwimah bint Muhammad! Niombe utakacho katika mali, lakini sitokufaa kwa chochote mbele ya Allaah)) [Al-Bukhaariy (2753), Muslim (206)].

 

 

Amesema Imaam Ibn ‘Uthaymiyn (Rahimahu Allaah) katika Majmuw’ Fataawa wa Rasaail (9/285- 288):

 

“Ikiwa ujamaa wa karibu na Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hautowafaa chochote jamaa zake, ni dalili hiyo kukatazwa tawassul kwa jaha ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwa kuwa jaha ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hainufaishi kwayo isipokuwa Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Na ndivyo ikawa kauli sahihi kabisa ya Wanachuoni ni uharamu wa tawassul kwa jaha ya Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).”

 

 

Na Imaam Ibn Baaz (Rahimahu Allaah) amesema katika Majmuw’ Fataawaa (3/98):

 

“Mwongozo na kipimo cha hakika ni kufuata yaliyokuja katika Qur-aan Al-Kariym na Sunnah Al-Mutwaharrah kwa kauli na na vitendo na kuitakidi. Ama unasaba, hakika hautofaa (mtu) wala hauna umuhimu kama alivyosema Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam:  

 

وَمَنْ بَطَّأَ بِهِ عَمَلُهُ لَمْ يُسْرِعْ بِهِ نَسَبُهُ

((…na ambaye kazorotesha ‘amali zake, haitomharakisha nasaba yake)). [Muslim]

 

Akasema: ((Enyi maashara Quraysh! Okoeni nafsi zenu, mimi sitowafaa kwa chochote mbele ya Allaah!)). Hivyo ndivyo alivyomwambia ‘Ammi yake na ‘Ammat (shangazi) yake, na binti yake Faatwimah. Basi ingekuwa unasaba utamfaa mtu, ungewafaa hao.”

 

 

Baadhi ya vitendo vinavyomhusisha    Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) katika kumshirikisha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) ni kama ifuatavyo:  

 

 

1-Kumtukuza mno Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) mpaka kumfikisha daraja ya Allaah!

 

Amekemea Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):

لا تُطْرُونِي كَمَا أَطْرَتْ النَّصَارَى ابْنَ مَرْيَمَ فَإِنَّمَا أَنَا عَبْدُهُ فَقُولُوا عَبْدُ اللَّهِ وَرَسُولُهُ) رواه البخاري

Msinitukuze Kama Manaswara [Wakristo] walivyomtukuza Masiyh mwana wa Maryam, hakika mimi na mja kwa hiyo semeni, ‘mja wa Allaah na Mjumbe Wake’)). [Al-Bukhaariy na Muslim.]

 

Na pia Hadiyth:

 

 عَنْ أَنَسٍ (رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهُ) أَنَّ نَاسًا قَالُوا: يَا رَسُولَ اَللَّهِ! يَا خَيْرَنَا وَابْنَ خَيْرِنَا, وَسَيِّدَنَا وَابْنَ سَيِّدِنَا! فَقَالَ: ((يَا أَيُّهَا اَلنَّاسُ! قُولُوا بِقَوْلِكُمْ، وَلاَ يَسْتَهْوِيَنَّكُمْ اَلشَّيْطَانُ، أَنَا مُحَمَّدٌ عَبْدُ اَللَّهِ وَرَسُولُهُ، مَا أُحِبُّ أَنْ تَرْفَعُونِي فَوْقَ مَنْزِلَتِي اَلَّتِي أَنْزَلَنِي اَللَّهُ عَزَّ وَجَلَّ)) رَوَاهُ النَّسَائِيُّ بِسَنَدٍ جَيِّدٍ

Imepokelewa kutoka kwa Anas (Radhwiya Allaahu ‘anhu) amesema: kwamba watu walisema: “Ee Rasuli wa Allaah! Ee mbora wetu na mwana wa mbora wetu, na bwana wetu, na mwana wa bwana wetu!.” Akasema: ((Enyi watu! Semeni msemayo, asikupambieni shaytwaan hawaa zenu. Mimi ni Muhammad mja wa Allaah na Rasuli Wake. Sipendi mnipandishe cheo kuliko cheo changu ambacho Ameniteremshia Allaah Ázza wa Jalla)). [An-Nasaaiy kwa isnaad nzuri]

 

Na kutukuzwa kwengine ni vile kusifiwa mno kwa uzushi na pia kutajwa kwa sifa ambazo ni Sifa za Allaah Pekee. Mfano katika Mawlid mbalimbali kama Barzanjiy, Nuwn, Al-Hibshiy (Sumtud-Durar), Burdah n.k. Vilevile kwenye nyiradi mbalimbali miongoni mwa nyiradi za Kisufi kama, Swalaatun-Naariyah, Wasiylatush-Shaafi’, Dalaail Al-Khayraat, n.k.

 

i) Maneno ya shirki yaliyomo katika Swalaatun-Naariyah:

 

للهم صلي صلاةً كاملة وسلم سلاما تاما على سيدنا محمد الذي تنحل به العقد، وتتفرج به الكرب، وتقضى به الحوائج ، وتنال به الرغائب، وحسن الخواتيم ويستسقى الغمام بوجهه الكريم وعلى آله وصحبه في كل لمحة ونفس بعدد معلوم لك

 

 Ee Allaah, Mswalie  Swalaah iliyotimu bwana wetu Muhammad ambayo kwa fadhila zake, vizuizi vyote vinaondoka, mazonge (misukosuko) yanapoa, shida zote zinafarijika, na mahitaji yanakidhika, na inafikisha kwa yanayotamaniwa, na mwisho mwema wapatikana, na kwa fadhila zake yule mwenye uso mtukufu mawingu (mvua) huombwa kunyesha, na Swalah na Salaam ziwe juu ahli zake na Maswahaba wake kwa kila muda na kila pumzi kwa idadi ya kadiri ya Ujuzi Wako)

 

 

ii) Baadhi ya sifa za kumtukuza mno katika Mawlid ya Barzanjiy:

 

“Katika saa ya kuzaliwa Mtume alihudhuria Aasiyah na Maryam kutoka Mbinguni.”

 

“Wanyama walitamka kwa Kiarabu kuwa leo imechukuliwa mimba ya Mtume.”

 

“Wanyama wakapeana khabari ya kuchukuliwa mimba ya Mtume.”

 

“Majini wakatoa khabari kwa watu kuwa imechukuliwa mimba ya Mtume.”

 

“Katika saa ya kuzaliwa Mtume alihudhuria Aasiyah na Maryam kutoka Mbinguni.”

 

“Wanavyuoni wameona ni jambo zuri watu kusimama wakati inapotajwa kuzaliwa Mtume.”

 

“Akamwona Allaah kwa macho yake.”

 

 

iii) Baadhi ya maneno ya shirki kwenye Mawlid Ya Nuwn

 

“Lau kuwa si Mtume asingepatikana Aadam wala Ibraahiym….. na ufalme wa Nabii Sulaymaan…”

 

“Manabii wote ni manaibu wa Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wakimwendeshea kazi yake.”

 

 

iv) Baadhi ya maneno ya shirki katika uradi wa Nabhaaniy: 

 

“Lau kuwa si Nabii Muhammad tusingekuja ulimwenguni wala tusingeishi!”

 

 

 

2-Kumuomba du’aa Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) badala ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa):

 

 

Du’aa huelekezwa kwake kama kusema: “Ee Rasuli nisaidie”, “Ee Rasuli niondoshee dhiki, shida zangu”. Hakuna kiumbe yeyote mwenye uwezo wa hayo isipokuwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa). Angekuwa na uwezo huo basi yasingemfika madhara, mateso, maudhi mbali mbali yaliyomsibu kutoka kwa makafiri. Allaah Alimuamrisha awaambie washirikina:

 

قُل لَّا أَمْلِكُ لِنَفْسِي نَفْعًا وَلَا ضَرًّا إِلَّا مَا شَاءَ اللَّـهُ ۚ وَلَوْ كُنتُ أَعْلَمُ الْغَيْبَ لَاسْتَكْثَرْتُ مِنَ الْخَيْرِ وَمَا مَسَّنِيَ السُّوءُ ۚ إِنْ أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ وَبَشِيرٌ لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ﴿١٨٨﴾

Sema: “Siimilikii nafsi yangu manufaa yoyote wala dhara yoyote isipokuwa Apendavyo Allaah. Na lau ningekuwa najua ya ghayb, bila shaka ningelijikithirishia ya kheri, na wala lisingelinigusa ovu. Mimi si chochote isipokuwa ni mwonyaji na mbashiriaji kwa watu wanaoamini.” [Al-A’raaf: 188]

 

 

Na Akamwambia tena aseme:

قُلْ إِنَّمَا أَدْعُو رَبِّي وَلَا أُشْرِكُ بِهِ أَحَدًا﴿٢٠﴾

Sema: (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم): “Hakika mimi namuomba Rabb wangu na wala simshirikishi na yeyote.”

 

قُلْ إِنِّي لَا أَمْلِكُ لَكُمْ ضَرًّا وَلَا رَشَدًا﴿٢١﴾

Sema: “Hakika mimi sikumilikieni dhara na wala uongofu.”

 

قُلْ إِنِّي لَن يُجِيرَنِي مِنَ اللَّـهِ أَحَدٌ وَلَنْ أَجِدَ مِن دُونِهِ مُلْتَحَدًا﴿٢٢﴾

Sema: “Hakika hakuna yeyote awezaye kunilinda na Allaah na wala sitoweza kupata mahali pa kukimbilia. [Al-Jinn: 20-22]

 

 

Na pia Akamuamrisha Rasuli Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) :

 

قُلْ إِنَّمَا أَنَا بَشَرٌ مِّثْلُكُمْ يُوحَىٰ إِلَيَّ أَنَّمَا إِلَـٰهُكُمْ إِلَـٰهٌ وَاحِدٌ ۖ فَمَن كَانَ يَرْجُو لِقَاءَ رَبِّهِ فَلْيَعْمَلْ عَمَلًا صَالِحًا وَلَا يُشْرِكْ بِعِبَادَةِ رَبِّهِ أَحَدًا ﴿١١٠﴾

 Sema (ee Muhammad صلى الله عليه وآله وسلم): “Hakika mimi ni mtu kama nyinyi, nafunuliwa Wahy kwamba: Hakika Muabudiwa wa haki wenu ni Ilaah Mmoja Pekee. Hivyo anayetaraji kukutana na Rabb wake, basi na atende ‘amali njema na wala asimshirikishe yeyote katika ‘ibaadah za Rabb wake.” [Al-Kahf: 110]

 

 

3-Kumuomba Nabiy (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) mbele ya kaburi lake:

 

Kuna wanaoelekea kaburi lake wanapofika Masjid Nabawiy Madiynah na kumuomba. Inavyopasa ni kuelekea Qiblah. Allaah Anakataza wazi kumshirikisha Yeye ndani ya Misikiti na hata penginepo, pale Anaposema:

 

وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّـهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّـهِ أَحَدًا﴿١٨﴾

Na kwamba Misikiti ni kwa ajili ya Allaah, basi msiombe yeyote pamoja na Allaah. [Al-Jinn: 18]

 

Naye Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam amekataza:

((لا تجعلوا قبري عيدًا))

((Msifanye kaburi langu ni sehemu ya kurudiwa rudiwa [kuendewa kila mara])). [Musnad Ahmad, Muswannaf 'Abdur-Razzaaq]

 

Na akasema:

 

   لعنة الله على اليهود والنصارى اتخذوا قبور أنبيائهم مساجد

((Allaah Amewalaani Mayahudi na Manaswara, wamefanya makaburi ya Manabii wao kuwa misikiti)). [Al-Bukhaariy  (425) Muslim (531)]

 

 

4-Kutawassul (kujikurubisha) kwa du’aa kupitia kwake:

 

Mfano kusema: “Ee Allaah, hakika mimi nakuomba kwa jaha ya Rasuli Wako Unikidhie haja zangu kadhaa, au Uniokoe na janga au balaa fulani, Unighufurie dhambi zangu n.k.”

 

Baada yakufariki Nabiy (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) haipasi kutawassal kwake. Maswahaba waliacha kutawassal kwake bali walitawassal kwa ami yake ‘Abbaas kwa kuwa alikuwa hai wakati huo kama ilivyothibiti katika Hadiyth ifuatayo:

 

 عَنْ أَنَسِ بْنِ مَالِكٍ  (رضي الله عنه)  أَنَّ عُمَرَ بْنَ الْخَطَّابِ (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُ) كَانَ إِذَا قَحَطُوا اسْتَسْقَى بِالْعَبَّاسِ بْنِ عَبْدِ الْمُطَّلِبِ فَقَالَ:  "اللَّهُمَّ إِنَّا كُنَّا نَتَوَسَّلُ إِلَيْكَ بِنَبِيِّنَا فَتَسْقِينَا وَإِنَّا نَتَوَسَّلُ إِلَيْكَ بِعَمِّ نَبِيِّنَا فَاسْقِنَا"  قَالَ" فَيُسْقَوْنَ

Kutoka kwa Anas bin Maalik (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba ‘Umar bin Al-Khatwaab (Radhwiya Allaahu ‘anhu) aliomba mvua kulipokuwa na ukame kwa kutawassal kwa ‘Abbaas bin ‘Abdil-Muttwalib akisema: “Ee Allaah, tulikuwa tunatawassal Kwako kupitia Nabiy wako, Ukatunyeshea mvua, na sasa tunatawassal Kwako kupitia ‘ami wa Nabiy Wako basi tunyweshee mvua”. Akasema: Wakanyweshewa mvua. [Al-Bukhaariy]

 

 

 

 

Share