11-Hakika Shirki Ni Dhulma Kubwa Mno! - Kutufu Makaburi Kuwaomba Waliomo Kaburini

 

إِنَّ الشِّرْكَ لَظُلْمٌ عَظِيمٌ

Hakika Shirki Ni Dhulma Kubwa Mno!

11- Kutufu Makaburi Kuwaomba Waliomo Kaburini

Alhidaaya.com

 

 

Miongoni mwa shirki kubwa ni kutufu makaburini, kuwaomba au kutawassal kwa walio makaburini. Maiti hawasikii du’aa wala hawaitikii, bali hawana uwezo wa kumnufaisha mtu wala kumdhuru! Dalili ni kauli za Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) zifuatazo:  

 

 إِنَّ الَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ عِبَادٌ أَمْثَالُكُمْ ۖ فَادْعُوهُمْ فَلْيَسْتَجِيبُوا لَكُمْ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ﴿١٩٤﴾

Hakika wale mnaowaomba badala ya Allaah ni waja kama nyinyi. Hebu waiteni wakuitikieni ikiwa nyinyi ni wakweli. [Al-A’raaf: 194] 

 

Na Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 وَلَا تَدْعُ مِن دُونِ اللَّـهِ مَا لَا يَنفَعُكَ وَلَا يَضُرُّكَ ۖ فَإِن فَعَلْتَ فَإِنَّكَ إِذًا مِّنَ الظَّالِمِينَ﴿١٠٦﴾

Na wala usiombe badala ya Allaah visivyokufaa wala visivyokudhuru. Na ukifanya, basi hakika utakuwa miongoni mwa madhalimu. [Yuwnus: 106] 

 

Na Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

وَالَّذِينَ يَدْعُونَ مِن دُونِهِ لَا يَسْتَجِيبُونَ لَهُم بِشَيْءٍ إِلَّا كَبَاسِطِ كَفَّيْهِ إِلَى الْمَاءِ لِيَبْلُغَ فَاهُ وَمَا هُوَ بِبَالِغِهِ ۚ وَمَا دُعَاءُ الْكَافِرِينَ إِلَّا فِي ضَلَالٍ ﴿١٤﴾

Na wale wanaowaomba badala Yake, hawawaitikii kwa chochote isipokuwa kama anayenyosha viganja vyake viwili vya mikono kwenye maji ili yafikie kinywani mwake, na wala hayafikii hata kidogo.  Na du’aa za makafiri hazipo ila katika upotofu.  [Ar-Ra’d: 14] 

 

Na Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 قُلْ مَن رَّبُّ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ قُلِ اللَّـهُ ۚ قُلْ أَفَاتَّخَذْتُم مِّن دُونِهِ أَوْلِيَاءَ لَا يَمْلِكُونَ لِأَنفُسِهِمْ نَفْعًا وَلَا ضَرًّا ۚ قُلْ هَلْ يَسْتَوِي الْأَعْمَىٰ وَالْبَصِيرُ أَمْ هَلْ تَسْتَوِي الظُّلُمَاتُ وَالنُّورُ ۗ أَمْ جَعَلُوا لِلَّـهِ شُرَكَاءَ خَلَقُوا كَخَلْقِهِ فَتَشَابَهَ الْخَلْقُ عَلَيْهِمْۚ قُلِ اللَّـهُ خَالِقُ كُلِّ شَيْءٍ وَهُوَ الْوَاحِدُ الْقَهَّارُ ﴿١٦﴾

Sema: “Ni nani Rabb wa mbingu na ardhi?” Sema: “Ni Allaah.” Sema: “Je, mnawafanya wengineo badala Yake kuwa walinzi na hali hawamiliki kwa ajili ya nafsi zao manufaa wala dhara?”  Sema: “Je, kipofu analingana sawa na mwenye kuona, au je, viza vinalingana sawa na nuru?” Au wamemfanyia Allaah washirika walioumba kama uumbaji Wake, kisha yakafanana maumbile kwao?  Sema: “Allaah ni Muumbaji wa kila kitu, Naye ni Mmoja Pekee, Mwenye kudhibiti na kudhalilisha, Mshindi, Asiyepingika.” [Ar-Ra’d: 16] 

 

 

Nukuu kutoka Fataawaa Al-Lajnah Ad-Daaimah (1/206) inasema:

 “…wala haijuzu kuomba du’aa kwa Mawalii au wengineo baada ya kufa kwao, bali inajuzu kuwaomba waja wema wakuombee. Wala haijuzu kutufu makaburi, kwani kutufu ni makhsusi kwa Ka’bah tukufu pekee. Atakayetufu makaburini kwa ajili ya kujikurubisha na watu wake humo ni shirki kubwa, japokuwa akiwa anakusudia kujikurubisha kwa Allaah tu! Hivyo ni bid’ah inayochukiza kabisa kwani haipasi kutufu makaburi wala kuswali kuyaelekea hata kama itakuwa ni kwa makusudio ya kutaka radhi za Allaah.” 

 

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa): 

وَالَّذِينَ تَدْعُونَ مِن دُونِهِ مَا يَمْلِكُونَ مِن قِطْمِيرٍ ﴿١٣﴾

Na wale mnaowaomba badala Yake hawamiliki hata kijiwavu cha kokwa ya tende.

 

 

إِن تَدْعُوهُمْ لَا يَسْمَعُوا دُعَاءَكُمْ وَلَوْ سَمِعُوا مَا اسْتَجَابُوا لَكُمْ ۖ وَيَوْمَ الْقِيَامَةِ يَكْفُرُونَ بِشِرْكِكُمْ ۚ وَلَا يُنَبِّئُكَ مِثْلُ خَبِيرٍ ﴿١٤﴾

 Mkiwaomba, hawasikii maombi yenu, na hata wakisikia, hawatakuitikieni.  Na Siku ya Qiyaamah watakanusha ushirikina wenu, na wala hakuna atakayekujulisha vilivyo kamaMwenye upeo wa khabari za dhahiri na za kufichika. [Faatwir: 13-14] 

 

 

Bali Siku ya Qiyaamah utadhihirika uadui baina yao na watawakanusha kabisa kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa)! 

 

وَمَنْ أَضَلُّ مِمَّن يَدْعُو مِن دُونِ اللَّـهِ مَن لَّا يَسْتَجِيبُ لَهُ إِلَىٰ يَوْمِ الْقِيَامَةِ وَهُمْ عَن دُعَائِهِمْ غَافِلُونَ﴿٥﴾

 

“Na nani aliyepotoka zaidi kuliko ambaye anayeomba asiyekuwa Allaah ambaye hamuitikii mpaka Siku ya Qiyaamah; nao wala hawatambui  maombi yao.”

 

 

وَإِذَا حُشِرَ النَّاسُ كَانُوا لَهُمْ أَعْدَاءً وَكَانُوا بِعِبَادَتِهِمْ كَافِرِينَ﴿٦﴾

Na pale watakapokusanywa watu, (miungu ya uongo) watakuwa ni maadui wao, na watakuwa wenye kuzikanusha ‘ibaadah zao. [Al-Ahqaaf: 5- 6] 

 

 

 

Washirikina kabla ya Uislamu walikuwa wakiomba masanamu ya Al-Laata, ‘Al-‘Uzza na wengineo, na hawakuwa wakiitakidi kuwa wana uwezo wa kuumba au kuteremsha mvua bali walidai kuwa yanawakurubisha kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) na kwamba masanamu hayo ni kama viombezi kwao. Kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa): 

 

وَالَّذِينَ اتَّخَذُوا مِن دُونِهِ أَوْلِيَاءَ مَا نَعْبُدُهُمْ إِلَّا لِيُقَرِّبُونَا إِلَى اللَّـهِ زُلْفَىٰ إِنَّ اللَّـهَ يَحْكُمُ بَيْنَهُمْ فِي مَا هُمْ فِيهِ يَخْتَلِفُونَ ۗ إِنَّ اللَّـهَ لَا يَهْدِي مَنْ هُوَ كَاذِبٌ كَفَّارٌ ﴿٣﴾

na wale waliojichukulia badala Yake walinzi (wakisema): “Hatuwaabudu isipokuwa ili wapate kutukurubisha kwa Allaah tumkaribie” Hakika Allaah Atahukumu baina yao katika yale waliyokhitilafiana nayo. Hakika Allaah Hamwongoi aliye muongo, kafiri. [Az-Zumar: 3] 

 

Basi hakuna tofauti na wanaoomba wakaazi wa makaburi kwani sanamu, makaburi, matwaghuti… yote yana maana moja ya kuabudu au kuomba asiyekuwa Allaah; ikiwa ni maiti au hai, na sababu za kuomba ni kama hizo. Anakanusha Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) hayo Anaposema:

 

قُلِ ادْعُوا الَّذِينَ زَعَمْتُم مِّن دُونِهِ فَلَا يَمْلِكُونَ كَشْفَ الضُّرِّ عَنكُمْ وَلَا تَحْوِيلًا ﴿٥٦﴾

Sema: “Iteni wale ambao mnadai (ni waabudiwa) pasi Naye, basi hawamiliki kukuondesheeni dhara na wala kuihamisha (kwa mwengine).” [Al-Israa: 56] 

 

 

Na Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anamwambia Rasuli Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) awajibu washirikina: 

 

 قُلْ أَفَرَأَيْتُم مَّا تَدْعُونَ مِن دُونِ اللَّـهِ إِنْ أَرَادَنِيَ اللَّـهُ بِضُرٍّ هَلْ هُنَّ كَاشِفَاتُ ضُرِّهِ أَوْ أَرَادَنِي بِرَحْمَةٍ هَلْ هُنَّ مُمْسِكَاتُ رَحْمَتِهِ ۚ قُلْ حَسْبِيَ اللَّـهُ ۖ عَلَيْهِ يَتَوَكَّلُ الْمُتَوَكِّلُونَ﴿٣٨﴾

Sema: “Je, mnaonaje wale mnaowaomba badala ya Allaah; ikiwa Allaah Atanikusudia dhara; je, wao wataweza kuondosha dhara Yake? Au Akinikusudia rahmah; je wao wataweza kuizuia rahmah Yake?” Sema: “Ananitosheleza Allaah”, Kwake watawakali wenye kutawakali. [Az-Zumar: 38] 

 

Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

قُل لَّا أَمْلِكُ لِنَفْسِي نَفْعًا وَلَا ضَرًّا إِلَّا مَا شَاءَ اللَّـهُ ۚ وَلَوْ كُنتُ أَعْلَمُ الْغَيْبَ لَاسْتَكْثَرْتُ مِنَ الْخَيْرِ وَمَا مَسَّنِيَ السُّوءُ ۚ إِنْ أَنَا إِلَّا نَذِيرٌ وَبَشِيرٌ لِّقَوْمٍ يُؤْمِنُونَ﴿١٨٨﴾

Sema: “Siimilikii nafsi yangu manufaa yoyote wala dhara yoyote isipokuwa Apendavyo Allaah. Na lau ningekuwa najua ya ghayb, bila shaka ningelijikithirishia ya kheri, na wala lisingelinigusa ovu. Mimi si chochote isipokuwa ni mwonyaji na mbashiriaji kwa watu wanaoamini.” [Al-A’raaf: 188] 

 

Na pia Anasema (Subhaanahu wa Ta'aalaa):

 

 قُلِ ادْعُوا الَّذِينَ زَعَمْتُم مِّن دُونِ اللَّـهِ ۖ لَا يَمْلِكُونَ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ فِي السَّمَاوَاتِ وَلَا فِي الْأَرْضِ وَمَا لَهُمْ فِيهِمَا مِن شِرْكٍ وَمَا لَهُ مِنْهُم مِّن ظَهِيرٍ ﴿٢٢﴾

Sema: “Ombeni wale mnaodai kwa dhana (ni waabudiwa) badala ya Allaah, hawamiliki hata uzito wa sisimizi mbinguni wala ardhini, na wala hawana humo ushirika Naye, na wala Yeye (Allaah) Hana msaidizi miongoni mwao.” [Sabaa: 22] 

  

Tahadhari Muislamu kuingia katika shirki kubwa juu ya kuwa hao wanaoombwa hawawezi kukuitikia du’aa zako bali elekea kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Ambaye Ndiye Mwenye uwezo wa kukunufaisha au kukuondoshea madhara kama Anavyosema: 

 

أَمَّن يُجِيبُ الْمُضْطَرَّ إِذَا دَعَاهُ وَيَكْشِفُ السُّوءَ وَيَجْعَلُكُمْ خُلَفَاءَ الْأَرْضِ ۗ أَإِلَـٰهٌ مَّعَ اللَّـهِ ۚ قَلِيلًا مَّا تَذَكَّرُونَ ﴿٦٢﴾

Au nani Anayemuitika mwenye dhiki mno anapomwomba, na Akamuondoshea ouvu na Akakufanyeni makhalifa wa ardhi? Je, yuko mwabudiwa pamoja na Allaah? Ni machache mno mnayokumbuka. [An-Naml: 62] 

 

 

Aayah hiyo aliisoma mtu alipofikwa na balaa la kukaribia kuuliwa, alipoisoma Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Alimuokoa. [Tafsiyr Ibn Kathiyr] 

 

Tena Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Yuko karibu mno nawe na Mwenye kuitikia du’aa za kila anayemuomba, Anasema: 

 

وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ ۖ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ ۖ فَلْيَسْتَجِيبُوا لِي وَلْيُؤْمِنُوا بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ﴿١٨٦﴾

Na watakapokuuliza waja Wangu kuhusu Mimi, basi Mimi ni Niko karibu (kwa ujuzi); Naitikia du’aa ya muombaji anaponiomba. Basi waniitikie Mimi na waniamini Mimi, wapate kuongoka. [Al-Baqarah: 186] 

 

 

Na fuata mafunzo Swahiyh kama alivyofundisha Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwamba unapozuru au kupitia makaburi usome du’aa: 

 

السَّلامُ عَلَـيْكُمْ أَهْلَ الدِّيارِ مِنَ المؤْمِنيـنَ وَالْمُسْلِمينَ، وَإِنّا إِنْ شاءَ اللهُ بِكُـمْ لاحِقُـونَ، (وَيَرْحَمُاللَّهُالْمُسْتَقْدِمِينَ مِنَّاوَالْمُسْتَأْخِرِينَ) أَسْـاَلُ اللهَ لَنَـا وَلَكُـمْ العَـافِيَةَ. 

Assalaamu ’Alaykum ahlad-diyaar minal Mu-uminiyna wal Muslimiyn, wainnaa In Shaa Allaahu bikum laahiquwn. (Wa yarhamu-Allaahu al-mustaqdimiyna minnaa wal musta-akhiriyna). As-alu-Allaaha lanaa walakumul-’aafiyah.

 

Amani ishuke juu yenu watu wa nyumba za Waumini na Waislamu, nasi apendapo Allaahtutakutana nanyi (Na Allaah Awarehemu wa mwanzo na wa mwisho). Namuomba Allaah Atupe sisi nanyi afya njema. [Hadiyth ya Buraydah bin Al-Huswayb (Radhwiya Allaahu ‘anhu) - Muslim (2/671) [975], Ibn Maajah na tamshi lake (1/494) [1547] kutoka kwa Buraydah  (Radhwiya Allaahu ‘anhu). Yaliyo katika mabano ni Hadiyth ya ‘Aaishah (Radhwiya Allaahu ‘anhaa) iliyopokelewa na Muslim (2/671) [974].] 

 

 

 

Share