186-Aayah Na Mafunzo: Ramadhwaan, Swiyaam Na Yanayohusu Duaa

 

Aayah Na Mafunzo:

 

Al-Baqarah

 

Alhidaaya.com

 

 

Anasema Allaah (سبحانه وتعالى):

 

وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ ۖ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ ۖ فَلْيَسْتَجِيبُوا لِي وَلْيُؤْمِنُوا بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ ﴿١٨٦﴾

Na watakapokuuliza Waja Wangu kuhusu Mimi, basi (waambie) hakika Mimi Niko Karibu (kwa ujuzi). Naitikia duaa ya muombaji anaponiomba. Hivyo basi waniitikie Mimi na waniamini Mimi, wapate kuongoka. [Al-Baqarah (2:186)]

 

 

 

Mafunzo:

 

Ramadhwaan, Swiyaam Na Yanayohusu Duaa

 

1-Ramadhwaan Ni Mwezi Wa Duaa Na Duaa Ya Mwenye Swawm Inaitikiwa:

 

 

Imaam Ibn ‘Uthaymiyn (رحمه الله) amesema: “Faida zinapatikana kutokana na Aayah hii. Kwanza: Kwamba kuna uwezekano mkubwa katika Swiyaam (funga) kuitikiwa duaa, kwa sababu Allaah (سبحانه وتعالى) Anataja Aayah hii baada ya kutaja Aayah za Swiyaam, khasa vile Anavotaja mwishoni mwa kutaja Aayaat za Swiyaam. Pili: Baadhi ya watu wa ilimu wamesema kwamba inaweza kupatikana katika humo faida nyengineyo, kwamba duaa iombwe mwisho wa Siku ya Swawm (kabla ya kufuturu). [Tafsiyr Imaan Ibn ‘Uthaymiyn]

 

Na Hadiyth kadhaa zimethibitisha kuitikiwa duaa ya mwenye Swawm, miongoni mwazo ni:

 

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ قَالَ قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: ((ثَلاثَةٌ لا تُرَدُّ دَعْوَتُهُمْ الإِمَامُ الْعَادِلُ وَالصَّائِمُ حِينَ يُفْطِرُ وَدَعْوَةُ الْمَظْلُومِ )) 

Amesimulia Abuu Hurayrah (رضي الله عنه):   Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Watatu duaa zao hazirejeshwi: Imaam (kiongozi)  mtenda haki, mwenye Swawm wakati anapofungua, na duaa ya aliyedhulumiwa.” [Imesimuliwa na At-Tirmidhiy Hadiyth nambari (2525), na Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh katika Swahihy At-Tirmidhiy Hadiyth nambari (2050)]

 

Na pia:

 

عَنْ أَبِي سَعِيدٍ الْخُدْرِيِّ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُ ، قَالَ : قَالَ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وسلم: ((إِنَّ لِلَّهِ تَبَارَكَ وَتَعَالَى عُتَقَاءَ فِي كُلِّ يَوْمٍ وَلَيْلَةٍ)) يَعْنِي: فِي َمَضَانَ وَإِنَّ لِكُلِّ مُسْلِمٍ فِي كُلِّ يَوْمٍ وَلَيْلَةٍ دَعْوَةً مُسْتَجَابَةً)) 

 

Amesimulia Abuu Sa’iyd Al-Khudriyy (رضي الله عنه): Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم)  amesema: “Allaah Ana watu wa kuwaacha huru na moto kila siku na usiku, na kila mja kati yao ana dua inayojibiwa.” [Imesimuliwa na Ahmad (7401). Na Al-Albaaniy kasema ni Swahiyh katika Swahihy Al-Jaami’i (2169), Swahiyh At-Targhiyb Wat-Tarhiyb (1002)]

 

 

2-Kuomba Duaa Kwa Allaah (عزّ وجلّ) Pekee Bila Ya Kumshirikisha:

 

Swahaba walikuwa wanamuuliza Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) maswali mbalimbali. Allaah (سبحانه وتعالى) Ameyataja katika Qur-aan na Akatoa majibu kwa kutanguliza kumwambia Rasuli Wake (صلى الله عليه وآله وسلم) aseme kuwajibu Swahaba “Sema!”. Mifano michache:

يَسْأَلُونَكَ عَنِ الْخَمْرِ وَالْمَيْسِرِ ۖ قُلْ ...  

“Wanakuuliza kuhusu pombe na kamari. Sema…” [Al-Baqarah (2:219)]

 

يَسْأَلُكَ النَّاسُ عَنِ السَّاعَةِ ۖ قُلْ ...

“Watu wanakuuliza kuhusu Saa (Qiyaamah). Sema…” [Al-Ahzaab (33:63)]

 

وَيَسْأَلُونَكَ عَنِ الْمَحِيضِ ۖ قُلْ ...  

“Na wanakuuliza kuhusu hedhi. Sema…” [Al-Baqarah (2:222)]

 

Na maswali yote mengineyo katika Qur-aan, jibu la Allaah (سبحانه وتعالى) limeanzia hivyo hivyo: “Sema….” isipokuwa swali hili ambalo Allaah (عزّ وجلّ) Analijibu Mwenyewe moja kwa moja Anaposema: 

فَإِنِّي قَرِيبٌ

“Basi hakika Mimi ni Niko karibu.”

 

 

Hivyo ni kwa sababu Allaah (سبحانه وتعالى) Anadhihirisha kwamba Yuko karibu kabisa na hakuhitaji mtu kuomba duaa kupitia kwa mtu yeyote ili isije kuwa ni kumshirikisha Allaah (سبحانه وتعالى) katika kuabudiwa Kwake, kwa sababu duaa ni ibaada kama alivyosema Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم) katika Hadiyth aliyosimulia Nu’umaan bin Bashiyr  (رضي الله عنه)  kwamba Nabiy (صلى الله عليه وآله وسلم)  katika kauli yake  Allaah (سبحانه وتعالى)

وَقَالَ رَبُّكُمُ ادْعُونِي أَسْتَجِبْ لَكُمْ ۚ

“Na Rabb wenu Amesema: “Niombeni, Nitakuitikieni.”  Amesema: “Duaa ni ibaada.” Kisha akasoma Aayah hiyo tukufu.   [Ghaafir (40:60)] [Abu Daawuwd, At-Tirmidhiy, Ibn Maajah, na Ahmad – Hadiyth Hasan Swahiyh]

 

Basi watanabahi na wazingatie na wamche Allaah wanaomshirikisha Allaah (سبحانه وتعالى) katika duaa zao kupitia viumbe kama wafanyavyo wenye kutufu makaburi kuwaomba wafu, jambo ambalo linaingia katika shirki kubwa ambayo Allaah (سبحانه وتعالى) Haisamehi pindi mtu akifariki bila ya kutubia.

 

 

 

3-Madamu Utamuomba Allaah Pekee Atakauitikia

 

Du’aa hupokelewa tu madamu Muislamu atamkabili Allaah (تعالى) bila ya kumshirikisha: Salmaan (رضي الله عنه) amehadithia kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Hakika Rabb wenu (تبارك وتعالى) (Aliyebarikika na Aliyetukuka), Yuhai, Mkarimu, Anastahi kutoka kwa mja Wake anaponyanyua mikono yake kisha Airudishe sifuri.” [Abuu Daawuwd, At-Tirmidhiy na Ibn Maajah]

 

Pia; Abuu Sa’iyd (رضي الله عنه) amehadithia kwamba Rasuli wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: “Hakuna Muislamu atakayeomba du’aa ambayo haina dhambi wala kukata undugu wa uhusiano wa damu isipokuwa Allaah Atampa mojawapo ya matatu; ima Amharakishie du’aa yake, au Amuwekee akiba Aakhirah au ima Amuepushe nayo ovu kama hilo.” Wakasema: Basi tutazidisha (kuomba du’aa). Akasema: “Allaah Mwingi zaidi (wa kuongeza).” [Ahmad]

 

 

 

 

 

Share