13-Du’aa Toka Kwenye Qur-aan Tukufu Na Sharh Yake: Tusiwe Fitnah Kwa Watu Madhalimu

Du’aa Toka Kwenye Qur-aan Tukufu

 

Na Sharh Yake

 

Alhidaaya.com

 

 

 

13-Tusiwe Fitnah Kwa Watu Madhalimu

 

 

 

 

"رَبَّنَا لَا تَجْعَلْنَا فِتْنَةً لِّلْقَوْمِ الظَّالِمِينَ  وَنَجِّنَا بِرَحْمَتِكَ مِنَ الْقَوْمِ الْكَافِرِينَ"

 

Ee Rabb wetu! Usitujaalie kuwa ni mtihani kwa watu madhalimu  ●  Na Tuokoe kwa Rahmah Yako na watu makafiri”.  [Yuwnus: (85-86)].

 

Hii ni miongoni mwa du’aa nyingi za Nabiy Muwsaa (‘Alayhis Salaam) wakati akikabiliana na Fir-‘awn.  Inatuonyesha namna Muislamu anavyokabiliana na makafiri na madhalimu ambapo la kwanza kulifanya ni kutawakkal kwa Allaah kwa kufanya maandalizi yote yanayohitajika na kubeba nyenzo zote, halafu kuelekea kwa Allaah kwa du’aa.

 

Fir-‘awn kwa jeuri yake, aliikataa miujiza yote aliyokuja nayo Muwsaa kuthibitisha Utume wake, hoja zisizopingika na dalili bayana alizomtolea.  Lakini pamoja na hivyo, vijana wachache katika Baniy Israaiyl walimwamini Muwsaa kutokana na ukweli waliouona kama Anavyosema Allaah:

 

"فَمَا آمَنَ لِمُوسَىٰ إِلَّا ذُرِّيَّةٌ مِّن قَوْمِهِ عَلَىٰ خَوْفٍ مِّن فِرْعَوْنَ وَمَلَئِهِمْ أَن يَفْتِنَهُمْ ۚ وَإِنَّ فِرْعَوْنَ لَعَالٍ فِي الْأَرْضِ وَإِنَّهُ لَمِنَ الْمُسْرِفِينَ"

 

Basi hawakumwamini Muwsaa isipokuwa dhuriya (vijana) katika kaumu yake kwa sababu ya kumkhofu Fir’awn na wakuu wao wasiwatese. Na hakika Fir’awn ni jeuri katika ardhi, na hakika yeye bila shaka ni miongoni mwa wapindukao mipaka”.  [Yuwnus: (83)].

 

Wengi kwa kumwogopa Fir-‘awn, walishindwa kuamini au kutangaza iymaan yao hadharani.

 

Kisha Nabiy Muwsaa (‘Alayhis Salaam) aliwaamuru watawakkal kwa Allaah tu.

 

"وَقَالَ مُوسَىٰ يَا قَوْمِ إِن كُنتُمْ آمَنتُم بِاللَّـهِ فَعَلَيْهِ تَوَكَّلُوا إِن كُنتُم مُّسْلِمِينَ"

 

Na Muwsaa akasema: Enyi kaumu yangu! Ikiwa mmemwamini Allaah, basi Kwake mtawakali, mkiwa ni Waislamu”.  [Yuwnus: (84)]

 

Kwa kuwa Allaah Pekee Ndiye Mwenye Kumtosha Mja Wake kwa kila lile analoliogopa au kila linalomletea ghamu.

 

"وَمَن يَتَوَكَّلْ عَلَى اللَّـهِ فَهُوَ حَسْبُهُ"

 

“Na yeyote anayetawakali kwa Allaah, basi Yeye Humtosheleza”.

 

Na ili mja aweze kupata toshelezo kamili la Allaah, basi ni lazima asimamie vyema ‘ibaadah zake zote, kisha atawakkal. Allaah kwenye aayah nyingi Amekutanisha ‘ibaadah na tawakkul.  Anasema:

 

"فَاعْبُدْهُ وَتَوَكَّلْ عَلَيْهِ"

 

Basi mwabudu Yeye na tawakali Kwake”.   [Huwd: (123)].

 

Muwsaa akawaambia:  “Kama nyinyi mmemwamini kikweli Allaah ikiwa pamoja na Nusra Yake kwenu, basi tawakalini Kwake tu”.  Ameikariri sharti kwao kusisitizia na kubainisha kwamba ukamilifu wa iymaan unakuja kwa kutegemeza mambo yote kwa Allaah.  Hapo hapo nao wakajibu na kutii wakisema:  “Tumetawakali kwa Allaah”.

 

Kisha wakamwomba Allaah wakisema:  “Usitujaalie kuwa ni mtihani kwa watu madhalimu”.  Kwa maana:  Usiwape usaidizi dhidi yetu wakatushinda, likawa hilo ni mtihani kwetu kwa dini yetu, au makafiri wakafitinika kwa ushindi wao dhidi yetu wakasema: Kama (Waislamu) wangelikuwa juu ya haki, basi wasingelishindwa”.

 

Fitnah hii ndio sasa imetawala baada ya sisi Waislamu kuwa katika hali ya udhaifu wa mwisho kabisa.  Kila mmoja ametulenga sisi kutokana na udhaifu huo.

 

Na baada ya kumwomba Allaah Ailinde Dini kutokana na ufisadi, wakaandamizia kumwomba usalama kwa nafsi zao kutokana na watu makafiri wakisema:  “Na Tuokoe kwa Rahmah Yako na watu makafiri”.   Wameikhusisha tawassul yao kwa Rahma za Allaah, kwa kuwa kwa Rahmah hizo, ombi hujibiwa.  Na kwa ajili hii, Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa anajilinda kutokana na misiba ya dini, kwani hiyo ndio misiba na maangamio makubwa zaidi.  Alikuwa anasema:

 

"وَلَا تَجْعَلْ مُصِيبَتَنَا فِي دِينِنَا"

 

“Wala Usijaalie msiba wetu ndani ya dini yetu”.

 

Tunajifunza kutokana na du’aa hizi:

 

1-  Kwamba iymaan ya kweli inapelekea kutawakkal kwa Allaah Pekee.

 

"يَا قَوْمِ إِن كُنتُمْ آمَنتُم بِاللَّـهِ فَعَلَيْهِ تَوَكَّلُوا إِن كُنتُم مُّسْلِمِينَ"

 

Enyi kaumu yangu! Ikiwa mmemwamini Allaah; basi Kwake mtawakali, mkiwa ni Waislamu”.

 

2-  Du’aa haipingani na tawakkul, bali ni kipengele kisaidizi cha kufanikisha tawakkul.

 

3-  Muislamu anatakikana ajilinde na fitna kutokana na hatari yake kwa dini. Rasuli (Swalla Allaah ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:

 

"تعوَّذوا باللَّه من الفتن: ما ظهر منها، وما بطن"

 

“Jilindeni kwa Allaah na fitnah, zilizodhihiri kati yake, na zilizofichika”[Swahiyh. Imesimuliwa na Zayd bin Thaabit]

 

Na alikuwa pia anasema katika du’aa yake kabla ya kumaliza Swalah yake:

 

"اللَّهُمَّ إني أعوذ بك من عذاب جهنم، ومن عذاب القبر، ومن فتنة المحيا والممات"

 

“Ee Allaah! Hakika mimi najilinda Kwako na adhabu ya Jahannam, na adhabu ya kaburi, na fitnah ya uhai na umauti”. [Swahiyh. Muslim]

 

 

 

Share