18-Uswuul Al-Fiqhi: Sura Ya Nne - Al-Imaam Ash-Shaafi'iy

 

SURA YA NNE

 

AL-IMAAM ASH-SHAAFI’IY

Al-Imaam ash-Shaafi’y alizaliwa mwaka 150 H, mwaka ambao Imaam Abuu Haniyfah alifariki. Alijifunza Fiqhi, kwanza Makkah pamoja na baadhi ya wanazuoni wa Ahl al-Hadiyth, kama vile Muslim bin Khaalid al-Zinji (amefariki mwaka 179) na Sufyaan bin ‘Uyaynah (amefariki mwaka 198). Baadaye alikwenda kwa Imaam wa Madiynah na kiongozi wa Ahl al-Hadiyth, Maalik bin Anas, na kujifunza pamoja naye, na alijifunza kuhifadhi (ili baadaye kulinganisha) mkusanyo wake pamoja na Hadiyth na mawazo ya kisheria, hiyo ni Muwattwaa. Hakika, al-Imaam ash-Shaafi’iy maisha yote alijiona yeye mwenyewe kuwa ana deni kwa Imaam Maalik.

 

Imesimuliwa kwamba Yuunus bin ‘Abd al-A’mla alimsikia Imaam ash-Shaafi’iy akisema: “Wakati wowote wanapotajwa ‘Ulamaa (kazi na elimu zao kulinganishwa). Maalik aliwamurika wote hao. Hakuna yeyote aliyenifanyia ihsani kubwa kuliko Maalik bin Anas”.[1] Hivi ndivyo alivyosema Imaam ash-Shaafi’iy baada ya kujifunza lugha, mashairi, fasihi, baadhi ya sayansi ya asili na sayansi ya hesabu na historia.

 

Al-Imaam ash-Shaafiy hakuvutika kwa kila kitu alichojifunza kutoka kwa katika kazi ya Ahl al-Hadiyth. Kwa mfano, aliwakosoa kwa kukubali Hadiyth ambayo ni Munqati’[2] akisema: “Hiyo Munqati’ si chochote.”

 

Al-Imaam ash-Shaafi’iy pia hakukubaliana na aina ya Hadiyth ya Mursal, [3](ingawa yeye mwenyewe alitumia kwa dharura Hadiyth Mursal kwa kesi ya iliyosimuliwa na Sai’iyd bin al-Musayyab), na kuamuru juu yake masharti makali kwa kukubaliana na wasimulizi kama wenye kutegemewa (na ikiwa Hadiyth walioisimulia kuwa ni sahihi).

 

Pale Imaam ash-Shaafi’iy alipokwenda Iraq, alitambua kutoka ngome kali ya Ahl ar-Ra-aykwamba; walikuwa tayari zaidi kutafuta kosa kwa taratibu za kisheria na mawazo ya watu wa Madiynah, hususan mwalimu wake al-Imaam Maalik. Hivyo, al-Imaam ash-Shaafi’iy alisimama kwa kumhami mwalimu wake, elimu yake ya fikra na utaratibu wake. Imesimuliwa kwamba aliwahi kusema:

 

Muhammad bin al-Hassan aliniambia: “Mwalimu wetu (yaani Abuu Haniyfah) alikuwa na ujuzi zaidi kuliko wako. Mwalimu wako alitakiwa kutozungumza, lakini mwalimu wetu angelikuwa ni mkosa kwa kubaki kimya.” Nilighadhibika na kumwambia: “Nakuuliza kwa jina la Allaah, ni nani alikuwa na ujuzi zaidi katika Sunnah ya Mtume; Maalik au Abuu Haniyfah?” Alisema: “Maalik. Lakini mwalimu wetu alikuwa mahiri zaidi kwenye Qiyaas. Nikamjibu, “Ndio, na Maalik alikuwa na ujuzi zaidi kuliko Abuu Haniyfah kuhusu Qur-aan, kuhusu utenguzi wake, na kuhusu Sunnah ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Yeyote aliye mjuzi zaidi katika Qur-aan na Sunnah, anayo haki zaidi ya kuzungumza!”[4]

 

Al-Imaam ash-Shaafi’iy alijifunza vitabu vya Muhammad bin al-Hassan na wanazuoni wengine wa Iraq.[5]Hakika, alikuja kuwa mwanafunzi wa Muhammad bin al-Hassan, na kujadiliana naye mawazo yake, wakati wote huo akikubali Sunnah na Ahl al-Hadiyth.

 

Al-Imaam ash-Shaafi’iy aliondoka Baghdaad kwa kipindi fulani, na aliporejea; mwaka 195 H, kulikuwa na darsa za duara arobaini au hamsini ambazo zilikutana kwa kawaida msikiti mtukufu. Al-Imaam ash-Shaafi’iy alianza kuhama kuanzia darsa moja ya duara kwenda nyengine, akielezea nini “Allaah na Mtume wakisema”, wakati walimu wengine walizungumza yale tu ambayo walimu wao walisema. Hatimaye, kukawa hakuna darsa ya kujifunza ndani ya msikiti isipokuwa kwa darsa ya kujifunza kwa Imaam ash-Shaafi’iy.

 

Baadhi ya wanazuoni wakubwa wa Ahl ar-Ra-ay kama Abuu Thawr, az-Za’farani’, al-Karaabiisi na wengine (ni miongoni mwa) waliohudhuria darsa za duara ya al-Imaam ash-Shaafi’iy. Wengi walitupilia mbali utaratibu wa Ahl ar-Ra-ayna kuanza kumfuata al-Imaam ash-Shaafi’iy. Al-Imaam Ahmad bin Hanbal pia alihudhuria darsa hii, na inasimuliwa kwamba alisema: “Msimuliaji yeyote ambaye amebeba kijidau cha wino, amefaidika kwa njia yoyote kutoka kwa al-Imaam ash-Shaafi’iy.” Pale al-Imaam Ahmad alipoulizwa kuelezea, alisema: “Hao Ahl ar-Ra-ay walikuwa wakiwacheka Ahl al-Hadiyth hadi pale al-Imaam ash-Shaafi’iy alipowafundisha vyenginevyo, na akathibitisha nafasi ya watu wa Hadiyth kwa hoja zilizo wazi.[6]

 

Juu ya hivyo, ilikuwa ni kujibu maombi ya Ahl al-Hadiyth, kwamba al-Imaam ash-Shaafi’iy aliandika kitabu chake, al-Hujjah (Mjadala) nchini Baghdaad. Kwa lengo la kufuta hoja ambazo Ahl ar-Ra-ay walizozileta dhidi yake.[7]

 

Baada ya hayo, al-Imaam ash-Shaafi’iy alitembelea Misri ambapo alikuta kwamba, watu walio wengi walijifunza somo na bila ya kuulizia kwa maoni ya Maalik. Kutokana na hayo, al-Imaam ash-Shaafi’iy alianza uchunguzi wa kina wa maoni ya kisheria ya Maalik, na kuona kwamba kwenye baadhi ya kesi “…yeye (Maalik) anatengeneza mawazo kwa kuegemea kanuni ya jumla (‘Aam), wakati akiacha masuala mahsusi (Khaasw); ilhali katika nyakati nyengine anatoa maamuzi kwenye suala mahsusi na akiacha kanuni ya jumla.”

 

Al-Imaam ash-Shaafi’iy pia aliona kwamba mara nyengine Maalik alikataa Hadiyth ya maana kwa kuegemeza tamko lililofanywa na mmoja wa Swahaabah au Taabi’uun, au kwa hoja yake mwenyewe iliyo bora. Mara nyengine, al-Imaam ash-Shaafi’iy aligundua kwamba; Maalik alikataa tamko la mmoja wa Swahaabah kwa kupendelea maoni ya Taabi’i, au mawazo yake binafsi; na kwamba angelifanya hivi kwenye kesi moja moja, na akirudia maelezo ya sheria yasiyojulikana ukweli wake. Bila ya kuangalia kanuni za jumla. Juu ya hivyo, Maalik alidai kwenye kesi nyingi kwamba kulikuwepo na Ijma’a kuhusiana na jambo hilo, pale panapotokezea, hasa, kutokubaliana kuhusiana nayo.

 

Al-Imaam ahs-Shaafi’iy pia alitambua mawazo ya Maalik; kuhusu Ijma’a ya watu wa Madiynah kwamba inaweza kutumika kama ni chanzo cha ushahidi, ilikuwa, ukweli hasa, sio yenye nguvu. Aliandika kitabu kwa jina la Al-Ikhtilaaf Ma’a Maalik ‘Kutokubaliana pamoja na Maalik’, ambamo alijadili mambo yote yaliyotajwa hapo juu.[8]

 

Kwa mujibu wa al-Imaam ash-Shaafi’iy, al-Imaam Maalik alipindukia mipaka iliyowekwa kwenye kutumia kanuni zake za al-Maswaalih al-Mursalah (uchaguzi wa iliyo bora zaidi), bila ya kuhitaji msaada wa kukuwepo taabu ya kutafuta chanzo cha ushahidi. Mawazo yake kwa mnasaba wa Abuu Haniyfah yalikuwa kwamba; kwenye kadhia nyingi alitilia mkazo jambo moja moja, katika masuala madogo na maelezo, bila ya kuangalia kanuni za msingi na masharti.[9]

 

Kwa kuyaweka akilini masuala haya, baadaye al-Imaam ash-Shaafi’iy alifikia hitimisho kwamba linalostahiki kuangaliwa zaidi ni mkusanyo wa masharti ya utungaji sheria, usimamizi wa kanuni za msingi kuhusu matumizi yake, na maendeleo ya utaratibu wa vyanzo kwa njia ambayo masuala ya Fiqh yanaweza kuamuliwa kupitia msaada wa usahihi na aina mnasaba za ushahidi. Hivyo, Fiqh inaweza kuwa ni matumizi ya vitendo kwa utaratibu huu, ili kwamba Fiqh iliyo mpya kuwezekana kuibuka kama ni mbadala wa fikra mbili zilizoanzishwa za mawazo ya kisheria.

 

Ilikuwa ni kwa sababu hii kwamba al-Imaam ash-Shaafi’iy alitunga ar-Risaalah, na kujenga Fiqh yake na mafunzo ya kisheria kwenye msingi wa masharti na utaratibu aliouelezea kwa kina ndani ya kitabu chake.

 

Al-Imaam Ahmad bin Hanbal alisema: “Hadi pale al-Imaam ash-Shaafi’iy alipokuja, hatukupata kuwaza vitu kama vya jumla na mahsusi al-‘Umuum wa al-Khuswuus[10]

 

Al-Imaam ash-Shaafi’iy alikuwa akisema kwa Imaam Ahmad: “Wewe una ujuzi zaidi kuhusu Hadiyth na wasimulizi kuliko mimi. Hivyo, kama Hadiyth ni sahihi, basi niambie. Kama ni sahihi, mimi nitaikubali hata kama (imesimuliwa na wasimulizi) kutoka Kuufah, Baswrah au Damascus.”[11] Tamko hili linaonesha wazi kwamba al-Imaam ash-Shaafi’iy alitilia mkazo zaidi kwa kuanzisha masharti kuliko kujihusisha na masuala madogo na maelezo.

 

Wanazuoni wanaoandika kwenye somo la historia ya Uswuulul al-Fiqh wote kwa pamoja wamekubaliana kwamba mwandishi wa kwanza kwenye somo hilo alikuwa ni al-Imaam ash-Shaafi’iy, na kwamba kitabu cha mwanzo kilichowahi kuandikwa kwenye somo hilo kilikuwa ni ar-Risaalah.[12]

 

Ndani ya kitabu chake, al-Bahr al-Muhiytw, az-Zarkashi (alifariki mwaka 794 H) ametenga sura kwa hili, ambamo amesema:

 

“Al-Imaam ash-Shaafi’iy alikuwa ni wa mwanzo kuandika kitabu kuhusu Uswuulul al-Fiqh. Ameandika ar-Risaalah, Ahkaam al-Qur-aan (Tafsiri ya Kisheria za Qur-aan), Ikhtilaaf al-Hadiyth (Mgongano wa Hadiyth), Ibtilaal al-Istihsaan (Kutofaa kwa Msaada wa Wanazuoni), Jima’a al-’Ilm (Ulinganifu wa ujuzi), na al-Qiyaas (Hoja kwa Kufananisha) – Kitabu ambacho amejadili makosa ya kundi la Mu’tazillah, na alibadili fikra zake kuhusu kukubali tamko lao. Baadaye, wanazuoni wengine walimuiga katika kuandika vitabu vya al-Uswuul.”

 

Katika kuisifu ar-Risaalah, al-Juwayni ameandika:-

 

“Hakuna yeyote kabla ya al-Imaam ash-Shaafi’iy aliyeandika vitabu kwenye somo la al-Uswuul, au aliyekuwa na ujuzi zaidi kama wake kuhusiana nayo. Imesimuliwa kwamba Ibn ‘Abbaas alitamka kitu kuhusu kuweka vitu vilivyo jumla kwa kuchambua kimoja kimoja, na kwamba baadhi ya wengine miongoni mwa wanazuoni wa mwanzo walitamka maneno yaliyoonesha kwamba walifahamu masharti haya. Lakini bado, wale waliokuja baada yao hawakusema chochote kuhusu al-Uswuul, na hawakuchangia chochote katika hilo. Tumeona vitabu vya Taabi’un na vya kizazi cha tatu, na tumeona kwamba hamna yeyote kati yao aliyeandika vitabu kuhusu al-Uswuul.”[13]

 



[1] Ibn ‘Abdul-Barr, Al-Intiqa’, uk. 23.

[2] Inaitwa Munqati’ kwa sababu ni Hadiyth iliyokatika sehemu yoyote ndani ya mnyororo wa wasimulizi. Kwani hata hivyo, haitohitaji kuthibitishwa kwa kudhani kwamba Hadiyth hiyo imepitishwa kutokea kizazi cha kale, na wala sio kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), Hadiyth kama hiyo ilikataliwa na Fuqahaa wote waliofuatia.

[3] Ufafanuzi kuhusiana na Hadiyth Mursal, na mzozo unaoizunguka, umetolewa ndani ya Surah ya tatu. Angalia ‘rejeo chini ya ukurasa’ nambari 36.

[4] Ibn ‘Abdul-Barr, Al-Intiqa’, uk. 24.

[5] Ni vyema itajwe hapa kwamba Muhammad bin Hassan pia alijifunza chini ya al-Imaam Maalik, na kwamba toleo lake la Muwattwaa ya Maalik inatambulika na wengi kuwa iliyo sahihi zaidi. Al-Imaam Muhammad ndani ya kitabu chake cha Kitaab ar-Radd ‘Alaa Ahl al-Madiynah ni yenye uwezo wa kushawishi matamshi juu ya tofauti zinazopatikana kwa kuziendea taratibu zilizotumiwa na fikra mbili za mawazo ya kisheria; Maalik na Hanafiy, na hasa kwa Ahl ar-Ra-ay na Ahl al-Hadiyth, kwa ujumla.

[6] Ibn ‘Abdul-Barr, Al-Intiqa’, uk. 86.

[7] Ibn ‘Abdul-Barr, Al-Intiqa’, uk. 86.

[8] Angalia Fakhr ar-Raazi, Manaaqib ash-Shaafi’iy, uk. 26

[9] Imaam al-Haramayn, ‘Abd al-Maalik Juwayni, Mughiyth al-Khalq.

[10] Az-Zarkashi, Al-Bahr al-Muhiytw, MS.

[11] Ibn ‘Abdul-Barr, Al-Intiqa’, uk. 25.

[12] Kumekuwa na uchache wa kutopatana kutokana na makubaliano kwenye suala hili. Achilia mbali, kutoka kwa wafuasi kadhaa wa fikra za mwanzo za mawazo ya sheria ambao wametoa ushahidi. Hata hivyo, lakini sio mwepesi kukubali madai yao juu ya wanazuoni kabla ya al-Imaam ash-Shaafi’iy, kama ilivyo kwa al-Imaam Abuu Yuusuf wa fikra za Hanafiy, kwamba waliandika kuhusu matawi haya muhimu ya sayansi ya Sharia’h.

[13] Angalia ‘Abd ar-Razzaaq, Tamhiyd li Taariykh al-Falsafah, Cairo, uk. 152.

Share