17-Uswuul Al-Fiqhi: Watu Wa Rai Na Watu Wa Hadiyth: Ahl Al-Hadiyth Na Ahl Ar-Ra-ay

 

WATU WA RAI NA WATU WA HADIYTH:

AHL AL-HADIYTH NA AHL AR-RA-AY

 

Huenda ukweli huu ukaja kuwa makini zaidi pale tutakapotaja chimbuko la fikra mbili za kisheria yasiyokuwa rasmi; watu wa Rai au Ahl ar-Ra-ay, na wale wa Hadiyth au Ahl al-Hadiyth, na kutokea kwa tofauti baina yao kuhusiana na vyanzo vyote vya utaratibu, na masuala ya kesi za sheria. Ijapokuwa ni kweli kwamba fikra zote hizi zilikuwa na mizizi yake katika kuvifuata vizazi viwili vilivyopita, ilikuwa ni katika wakati huu kwamba, tofauti zao kwenye masuala ya Fiqhi yalikuja kuwa wazi, na ilikuwa ni wakati huu kwamba watu walianza kujigawa makundi kwa msingi wa tofauti zao katika kupata dalili za kisheria kutokana na vyanzo.

 

Waandishi wa Historia ya Sheria ya Kiislamu, wanasisitiza kwamba watu wa fikra za Rai, wa Ahl ar-Ra-ay ilikuwa ni kupanuka kwa elimu iliyotolewa na ‘Umar na ‘Abdullaah bin Mas’uud ambao miongoni mwao Swahaabah, walikuwa na upana wa kupanga katika matumizi yao ya Ra-ay (yaani mawazo). Badala yake, ‘Alqamah an-Nakha’iy (amefariki mwaka 60 au 70 H), ami na mwalimu wa Ibraahiym an-Nakha’iy, Ibraahiym alishajiishwa nao, baadaye alimsomesha Hammaad bin Abi Sulaymaan (amefariki mwaka 120 H), ambaye, baadaye alikuwa ni mwalimu wa Abuu Haniyfah.

 

Wanahistoria hao hao wanafafanua kwamba, hao watu wa Hadiyth wa Ahl al-Hadiyth ilikuwa ni mfululizo wa elimu za hao Swahaabah ambao khofu zao za kuchanganya barua za vyanzo vya maandiko (Nuswuus) ziliwafanya kuwa na hadhari kwa kila upande, hadi kufikia ambapo walikuwa hawawezi kwenda mbali zaidi ya maandiko. Hili lilikuwa ni, na kwa urefu, kwa ‘Abdullaah bin ‘Umar bin al-Khattwaab, ‘Abdullaah bin ‘Amr bin al-‘Aas, az-Zubayr, na ‘Abdullaah bin ‘Abbaas.

 

Fikra za Ahl al-Hadiyth zilikuja kuenea zaidi sehemu za Hijaaz kwa sababu zilizo nyingi, na iliyo muhimu mno ilikuwa ni idadi kubwa ya Hadiyth na simulizi nyengine zilizojulikana na watu wa eneo hilo, na ukweli ni kwamba, Wilaya hiyo ilikuwa ni imara zaidi baada ya kiti cha Khilaafah kilipoondoshwa na shughuli nyingi za kisiasa zilipohamishwa, kwanza ni Damascus, baadaye Baghdaad. Imaam wa Madiynah, Sa’iyd bin al-Musayyab (amefariki mwaka 94 H), aliwahi kusimulia kwamba watu wa Makkah na Madiynah hawakupoteza Hadiyth na Fiqh nyingi, kwa sababu walikuwa wazoefu katika Fataawa na masimulizi ya Abuu Bakr, ‘Umar, ‘Uthmaan, ‘Aliy (kabla ya kuwa Khaliyfah), ‘Aaishah, Ibn ‘Abbaas, Ibn ‘Umar, Zayd bin Thaabit na Abuu Hurayrah, na hivyo hawakuona haja ya kutumia Ra-ay kwa lengo la kupata sheria.

 

Fikra za Ahl ar-Ra-ay, kwa upande mwengine, zilipata sifa nchini Iraq. Wanazuoni wa kundi hili walifikiria kwamba tafsiri za kisheria za Shari’ah ziwe na msingi wa hoja, waangalie vizuri mapenzi ya watu, na kurejeza pamoja na upambanuzi wenye hekima. Hakika, wanachuoni hawa waliamini kuwa ni jukumu lao kuweka bayana maana hizi na hekima zilizomo ndani ya sheria, na kuzitenganisha baina yao; ili kwamba, kama hoja za sheria yoyote zitakosa mnasaba kwa kupita wakati au kubadilika mazingira; sheria haitokuwa tena yenye nguvu. Kama wataona hoja ndani ya sheria, mara nyengine wataonelea bora kutoa hoja kwa kutumia msingi wa matumizi ya kufananisha kwa hoja hizo. Hivyo, kwa kesi nyingi, hoja zitaafikiana pamoja na sheria bora pale hoja hizo zitakapogongana na ushahidi wa makundi tofauti ya Hadiyth.

 

Kuenea kwa utaratibu huu nchini Iraq, ulisaidiwa na idadi ya Swahaabah waliosukumwa na utaratibu wa ‘Umar. Miongoni mwao alikuwa ni Ibn Mas’uud, Abuu Muusa al-Ash’ariy, ‘Imraan bin Huswayn, Anas bin Maalik, Ibn ‘Abbaas na wengineo. Kuenea huku pia kulisababishwa sana na kupelekwa Khilaafah nchini Iraq, na kukaa kimakaazi kwa ‘Aliy na wafuasi wake.

 

Pale mapote, kama Shi’ah na Khawaarij, yalipotokea nchini Iraq, mgongano ukaibuka na utengenezaji wa Hadiyth za kubuni ukaenea sana[1]. Matokeo yake, wanazuoni wa kisheria wa Iraq walilazimishwa kuweka vigezo vya kukubali Hadiyth. Kutokana na ulazima huo, ni simulizi chache zilizotolewa na Swahaabah waishio Iraq zilikubalika. Juu ya hivyo, idadi kubwa ya matatizo ya kisheria na ongezeko la kuendelea kwenye masuala ya kisheria mapya ambayo hayakuwa na mfano wake nyuma kwenye eneo hilo, zilikuwa zaidi ya kujadiliwa kwa mnasaba wa Hadiyth zenye kutegemewa.

 

Kwa hivyo, ilikuwa kwa njia hii ambapo ‘Ummah uligawika, kwa wale wasiojihusisha na aidha Shi’ah au Khawaarij, kwenye makundi mawili, Ahl al-Hadiyth na Ahl ar-Ra-ay, na mgongano baina yao ukawa mkali.

 

Hivyo, Ahl ar-Ra-ay kawaida wakiwatoa makosa Ahl al-Hadiyth kwa kuwa na kiwango kidogo cha umakini na uchache wa ufahamu wa Fiqhi, ingawa Ahl al-Hadiyth walidai kwamba mawazo ya Ahl ar-Ra-ay hayakuegemezwa zaidi ila kwenye kubahatisha tu; na kwamba wamejitenga wenyewe kwa kutokuwa na hadhari inayohitajika katika masuala ya Dini yenye umuhimu, ambayo yanaweza tu kuhakikishwa kupitia msaada wa vyanzo vya maandiko.

 

Hakika, Ahl ar-Ra-ay walikubaliana na Waislamu wote kwamba pale mtu atakapofahamu Sunnah, hatoikataa. Kwa sababu si zaidi ila ni mawazo ya mtu fulani. Udhuru wao kwenye kesi zote hizo ambazo wamelaumiwa kwa kuchanganya Sunnah, si chochote ila kwamba hawakutambua Hadiyth yoyote kuhusiana na suala linalobishaniwa, au kwamba walitambua Hadiyth lakini hawakuikubali kuwa ni yenye maana kwa sifa ya udhaifu kwa wasimuliaji au kasoro nyengine waliyoiona (kasoro ambayo pengine wengine hawakuiona kuwa yenye kuharibu), au kwamba walitambua Hadiyth nyengine ambayo wao waliitambua kuwa yenye maana na ambayo ilipingana na kusudio la sheria ya Hadiyth inayokubalika na wengine.

 

Juu ya yote hayo, Ahl al-Hadiyth walikubaliana na Ahl ar-Ra-ay katika dharura ya kuwa na msaada wa hoja wakati wowote suala linapotokezea ambapo hakuna maamuzi maalum kwenye vyanzo vya maandiko. Lakini bado, juu ya sehemu hizi za makubaliano, mgogoro na mvutano baina ya makundi haya ulibaki kuwa mkali.



[1] Kwa vile kila dhehebu lilipigana kumzidi mwengine, na kupata wartadi kutoka katika Uislamu, waliamua kuziharibu maana za maneno ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kama ilivyowekwa kumbukumbu kwenye Hadiyth, na kuzizalisha na kuzinasibisha kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), maneno na maana zilizotengenezwa kunufaisha malengo yao wenyewe.

 

 

 

Share