Kisa Cha Aswhaabul-Kahf (Watu Wa Pangoni) Sehemu Ya 4
Imeandikwa na Alhidaaya.com
}}وَلاَ تَقُولَنَّ لِشَيْءٍ إِنِّي فَاعِلٌ ذَلِكَ غَدًا{{
{{Wala usiseme kamwe kwa jambo lolote lile: Hakika nitalifanya
}}إِلاَّ أَن يَشَاء اللَّهُ وَاذْكُر رَّبَّكَ إِذَا نَسِيتَ وَقُلْ عَسَى أَن يَهْدِيَنِ رَبِّي لأَقْرَبَ مِنْ هَذَا رَشَدًا {{
{{Isipokuwa Mwenyezi Mungu Akipenda. Na mkumbuke Mola wako Mlezi pale unaposahau, na sema: 'Asaa Mola wangu Mlezi Ataniongoa kwenye uongozi ulio karibu zaidi kuliko huu}}
}}وَلَبِثُوا فِي كَهْفِهِمْ ثَلَاثَ مِائَةٍ سِنِينَ وَازْدَادُوا تِسْعًا {{
{{Na walikaa katika pango lao miaka mia tatu, na wakazidisha tisa}}
}} قُلِ اللَّهُ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثُوا لَهُ غَيْبُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَبْصِرْ بِهِ وَأَسْمِعْ مَا لَهُم مِّن دُونِهِ مِن وَلِيٍّ وَلَا يُشْرِكُ فِي حُكْمِهِ أَحَدًا {{
{{Sema: Mwenyezi Mungu Anajua zaidi muda waliokaa. Ni Zake tu siri za mbingu na ardhi. Kuona kulioje na kusikia Kwake! Hawana mlinzi isipokuwa Yeye, wala Hamshirikishi yeyote katika hukumu Yake}} [Al-Kahf: 23-29]
UMUHIMU WA KUSEMA INSHA-ALLAAH
Anasema Allaah سبحانه وتعالى :
}}وَلاَ تَقُولَنَّ لِشَيْءٍ إِنِّي فَاعِلٌ ذَلِكَ غَدًا {{
{{Wala usisema kamwe kwa jambo lolote lile: Hakika nitalifanya
}}إِلاَّ أَن يَشَاء اللَّهُ{{
{{Ila AtakapopendaMwenyezi Mungu}}
Hapa Allaah سبحانه وتعالى Anamfundisha Mtume صلى الله عليه وآله وسلم adabu njema anapoazimia kufanya kitendo kwamba lazima asema 'InshaAllaah' (Allaah Akipenda) kwani Yeye Allaah سبحانه وتعالى Ndiye Mwenye kujua mambo ya 'ghayb' (yasiyoonekana). Nani atakayeweza kujua mambo gani yatakuwa au yatatokea na yapi hayatakuwa au hayatatokea wakati ujao?
Imesimuliwa katika Sahihayn (Sahihi mbili; Al Bukhaariy na Muslim) kwamba Abu Hurayrah رضي الله عنه amesema kwamba Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema:
((قال سليمان ابن داود عليهما السلام: لأطوفن الليلة على سبعين امرأة - وفي رواية: تسعين امرأة، وفي رواية مائة امرأة - تلد كل امرأة منهن غلاماً يقاتل في سبيل الله، فقيل له - وفي رواية: قال له الملك: قل إن شاء الله، فلم يقل، فطاف بهن فلم يلد منهن إلا امرأة واحدة نصف إنسان، قال رسول الله - والذي نفسي بيده لو قال إن شاء الله لم يحنث، وكان دركاً لحاجته وفي رواية: ولقاتلوا في سبيل الله فرساناً أجمعين))
((Nabii Sulaymaan bin Dawuud عليهما السلام alisema: "Usiku wa leo nitawatembelea (nitafanya kitendo cha ndoa) wanawake sabini (kwa riwaya nyingine ilikuwa ni tisini au mia) ili kila mmoja wao azae mtoto wa kiume ambao watapigana Fiy Sabiyli Allaah (Kwa ajili ya Allaah)". Akaaambiwa (kutokana na riwaya moja malaika alimwambia), sema InshaAllaah, lakini hakusema. Akawatembelea wanawake hao lakini hakuna aliyezaa isipokuwa mmoja tu ambaye alizaa mtoto aliyeumbika nusu tu. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akasema: Naapa kwa Yule Ambaye nafsi yangu iko mikononi Mwake, angelisema Insha Allaah, asingeliharibu kiapo chake na hivyo ingelimsaidia kupata alichotaka. (Na kutoka riwaya nyengine) Wangelipigana kama wapanda farasi kwa ajili ya Allaah))
[Fath Al-Bariy 6:41, Muslim 3:1275 ]
SABABU YA KUTEREMSHWA AYA HIZI
Ibn 'Abbaas amesema:
Quraysh walimtuma An-Nadr bin Al-Haarith na 'Uqbah bin Abi Mu'iytw kwa Mapadri Wayahudi walioko Madiynah na wakawaambia "Nendeni na waulizeni kuhusu Muhammad na wasimulieni kuhusu yeye Muhammad anayoyasema, kwani wao ni watu wa kwanza wa kupewa vitabu na wanayo elimu ya mitume kuliko sisi".
Wakaenda maquraysh hao wawili na walipofika Madiynah waliwauliza mapadri ya Kiyahudi kuhusu Mtume صلى الله عليه وآله وسلم. Waliwaelezea sifa zake zote. Wakasema, "Nyinyi ni watu wa Tawraat na sisi tumekuja kwenu ili mtujulishe kuhusu sahibu yetu".
Mapadri wa kiyahudi wakawaambia, "Muulizeni mas-ala matatu ambayo tutakupeni mkamuulize, na pindi akijibu haya mas-ala matatu, basi yeye ni Mtume aliyetumwa na Allaah, na ikiwa hatojibu, basi atakuwa anajisemea mambo yasiyokuwa ya kweli, na hapo mfanye mnavyotaka.
Muulizeni:
1. Kuhusu vijana wa wakati wa kale ni kisa chao. Kwani kisa chao ni cha kustaajabisha. (Asw-haabul-Kahf – vijana Wa pangoni)
2. Nini kisa cha mtu aliyesafiri sana hadi akafika Mashariki na Magharibi ya dunia, yaani Dhul-Qarnayn.
3. Muulizeni kuhusu roho (nafsi) ni kitu gani hicho?
Akiweza kukupeni majibu ya mas-ala hayo matatu basi hakika yeye ni Mtume kwa hiyo mfuateni. Na asipokupeni majibu yake basi ni mtu aliyetunga uwongo kwa hiyo mfanyeni mnavyotaka".
An-Nadr na 'Uqbah wakarudi Makkah kwa Maquraysh na kuwaambia, "Enyi Quraysh, sisi tumekuja na uamuzi wa suluhisho ambalo litatatua na kumaliza mashaakil baina yetu na Muhammad. Mapadri Wayahudi wametuambia tumuulize Muhammad mas-ala matatu". Wakawaelezea mas-ala yenyewe, kisha wakamuendea Mtume صلى الله عليه وآله وسلم na kumuuliza hayo mas-ala. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akawaambia:
((أُخْبِرُكُم غَدَا عَمَّ سَأَلْتُم عَنْهُ))
((Nitakujulisheni kesho mambo mliyoyauliza))
Lakini hakusema Insha-Allaah. Wakaondoka zao kisha Mtume صلى الله عليه وآله وسلم akakaa siku kumi na tano bila ya Jibriyl عليه السلام kumjia kama ilivyo kawaida yake kumpa Wahyi (ufunuzi) kutoka kwa Allaah سبحانه وتعالى. Watu wa Makkah wakaanza kumtilia shaka na kupita kusema, "Muhammad katuahidi kutujibu mas-ala tuliyomuuliza siku ya pili na hadi leo siku ya kumi na tano zimepita hakutujibu lolote katika hayo".
Mtume صلى الله عليه وآله وسلم aliingiwa na huzuni sana kwa kuchelewa kupata 'Wahyi' na alisikitika kwa maneno ya watu wa Makkah waliyokuwa wakisema. Kisha Jibriyl عليه السلام akaja kumteremshia Surah hii ya 'Al-Kahf' ambayo kwanza imemliwaza Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kuhusu alivyokuwa akihisi huzuni na masikitiko ya watu wa Makkah,
}}فَلَعَلَّكَ بَاخِعٌ نَّفْسَكَ عَلَى آثَارِهِمْ إِن لَّمْ يُؤْمِنُوا بِهَذَا الْحَدِيثِ أَسَفًا{{
{{Huenda ukajihiliki nafsi yako kwa ajili yao, kuwasikitikia kwa kuwa hawayaamini mazungumzo haya!}} Al-Kahf: 6
Allaah سبحانه وتعالى Anasema: "Usijiangamize nafsi yako kwa majuto". Qataadah kasema, "Kujiua kwa hasira na huzuni kwa ajili yao" [At-Tabariy 17:597-598]
Mujaahid kasema, "kwa hamu" [At-Tabariy 17:598]
Maelezo hayo yana maana kwamba, "Usisikitike nao, wewe fikisha ujumbe tu wa Allaah سبحانه وتعالى kwao, na yeyote atakayekwenda njia ya haki basi ni kwa ajili ya manufaa yake, na atakayekwenda njia ya upotofu basi ni khasara yake mwenyewe, kwa hiyo wewe usijiangamize nafsi yako kwa huzuni juu yao".
Zikaendelea aya baada ya hiyo ya kumliwaza Mtume صلى الله عليه وآله وسلم
}}إِنَّا جَعَلْنَا مَا عَلَى الْأَرْضِ زِينَةً لَّهَا لِنَبْلُوَهُمْ أَيُّهُمْ أَحْسَنُ عَمَلًا{{
}} وَإِنَّا لَجَاعِلُونَ مَا عَلَيْهَا صَعِيدًا جُرُزًا{{
{{Kwa hakika Tumevifanya vilivyoko juu ya ardhi kuwa ni pambo lake ili Tuwafanyie mtihani, ni nani kati yao wenye vitendo vizuri zaidi}}
{{Na hakika Sisi Tutavifanya vyote vilio juu ya ardhi kuwa kama nchi iliyopigwa na ukame}} Al-Kahf: 7-8
Kisha Allaah سبحانه وتعالى Akampa fundisho Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kuwa asiseme atafanya jambo lolote ila baada ya kusema Insha Allaah kama ilivyo katika ayah ifuatavyo:
}}وَلاَ تَقُولَنَّ لِشَيْءٍ إِنِّي فَاعِلٌ ذَلِكَ غَدًا {{
{{Wala usiseme kamwe kwa jambo lolote lile: Hakika nitalifanya hilo kesho}}
}}إِلاَّ أَن يَشَاء اللَّهُ وَاذْكُر رَّبَّكَ إِذَا نَسِيتَ وَقُلْ عَسَى أَن يَهْدِيَنِ رَبِّي لأَقْرَبَ مِنْ هَذَا رَشَدًا {{
{{Isipokuwa Mwenyezi Mungu Akipenda. Na mkumbuke Mola wako Mlezi pale unaposahau, na sema: 'Asaa Mola wangu Mlezi Ataniongoa kwenye uongozi ulio karibu zaidi kuliko huu}}
}}وَاذْكُر رَّبَّكَ إِذَا نَسِيتَ{{
{{Na mkumbuke Mola wako Mlezi pale unaposahau}}
Hii ina maana kwamba, ukisahau kusema InshaAllaah basi sema pale unapokumbuka. Hii ni rai ya Abu 'Aliyah na Al-Hassan Al-Basriy [At-Twabariy 17:645]
Ibn 'Abbaas aliifasiri aya hii kuwa mtu anaweza kusema InshaAllaah hata kama baada ya mwaka ikiwa amesahau kusema baada ya kuweka kiapo au kusema atafanya jambo fulani. Hivi atakuwa amefanya Sunnah ya kusema InshaAllaah hata kama baada ya kuvunja kiapo. Hii vile vile ni rai ya Ibn Jariyr [At-Twabariy 17:646]. Lakini kasema hii haina maana kwamba inafidia kuvunja kiapo cha mtu, bali mtu anapovunja kiapo lazima afanye kafara yake (malipo ya kiapo). Na Allaah سبحانه وتعالى Anajua zaidi.
}}وَقُلْ عَسَى أَن يَهْدِيَنِ رَبِّي لأَقْرَبَ مِنْ هَذَا رَشَدًا{{
{{na sema: 'Asaa Mola wangu Mlezi Ataniongoa kwenye uongozi ulio karibu zaidi kuliko huu}}
Maana kwamba, "Ewe Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ikiwa umeulizwa jambo lolote ambalo hulijui, basi muombe Allaah سبحانه وتعالى kwa kurudi Kwake ili Akuongoze kujibu lililo haki". Na Allaah سبحانه وتعالى Anajua zaidi.
KUSEMA INSHA ALLAAH NI FUNDISHO KWETU SOTE
Inampasa kila Muislamu anapotaka kufanya jambo au anapotoa ahadi ya jambo fulani basi ni lazima aseme InshaAllaah, kwani hakuna anayejua kama hilo jambo ataweza kulitimiza ila kwa uwezo wa Allaah سبحانه وتعالى. Uwezekano wa kutendeka jambo au kutokutendeka kunategema na kupenda Kwake Allaah سبحانه وتعالى. Kuna mas-ala ambayo hatuyamiliki sisi, nayo ni kama mfano unapoagana na mtu kukutana siku fulani, wakati fulani na mahala fulani:
1) Uhai wa mmoja wa wawili walioagana kukutana, huenda mmoja wao akaiaga dunia kabla ya siku hiyo ya kukutana.
2) Sehemu walioagana inaweza kuwa imefikwa na maafa ikawa haiko tena.
3) Wakati wa kuagana inaweza kutokea dharura
Kwa hiyo ni muhimu
Mas-ala matatu hayo aliyoulizwa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم Ameyataja Allaah سبحانه وتعالى
Aya kuhusu Mas-ala ya kwanza (Vijana wa Pangoni) Asw-haabul-Kahf )
Kisa hiki cha Asw-haabul-Kahf kimeelezewa katika Surah hii tukufu na kikaanza kwa ayah hii,
}}أَمْ حَسِبْتَ أَنَّ أَصْحَابَ الْكَهْفِ وَالرَّقِيمِ كَانُوا مِنْ آيَاتِنَا عَجَبًا{{
{{Bali unadhani ya kwamba wale Watu wa Pangoni na Maandishi walikuwa ni ajabu miongoni mwa ishara Zetu?}} Al-Kahf:9
Na zikaendelea aya kuelezea kisa chao kama tulivyokielezea mwanzo wa visa hivi (Tazama kisa sehemu ya kwanza hadi sehemu ya tatu).
Kuhusu Mas-ala ya pili (Mtu aliyesafiri sana hadi akafika Mashariki na Magharibi ya dunia – Dhul-Qarnayn)
Aya kuhusu mas-ala ya pili vile vile zimelezewa katika Surah hii tukufu:
}}وَيَسْأَلُونَكَ عَن ذِي الْقَرْنَيْنِ قُلْ سَأَتْلُو عَلَيْكُم مِّنْهُ ذِكْرًا {{
{{Na wanakuuliza khabari za Dhul- Qarnayn. Waambie: Nitakusimulieni baadhi ya hadithi yake}} Al-Kahf: 83
Na kisa chake kinaendelea baada ya aya hii. (Tukijaaliwa Insha Allaah tutakielezea itakapofika wakati wake)
Kuhusu Mas-ala ya tatu (Roho [Nafsi])
Ametaja Allaah سبحانه وتعالى kuhusu Mas-ala haya katika Surah ya Bani Israiyl,
}}وَيَسْأَلُونَكَ عَنِ الرُّوحِ قُلِ الرُّوحُ مِنْ أَمْرِ رَبِّي وَمَا أُوتِيتُم مِّن الْعِلْمِ إِلاَّ قَلِيلاً {{
{{Na wanakuuliza khabari za Roho. Sema: Roho ni katika mambo ya Mola wangu Mlezi. Nanyi hamkupewa katika ilimu ila kidogo tu}} Bani Israiyl: 85
MUDA WALIOKAA PANGONI
Mwisho wa kisa hiki Allaah سبحانه وتعالى Anaelezea muda ambao vijana hao walikaa pangoni,
}}وَلَبِثُوا فِي كَهْفِهِمْ ثَلَاثَ مِائَةٍ سِنِينَ وَازْدَادُوا تِسْعًا{{
{{Na walikaa katika pango lao miaka mia tatu, na wakazidisha tisa}}
}}قُلِ اللَّهُ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثُوا لَهُ غَيْبُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ أَبْصِرْ بِهِ وَأَسْمِعْ مَا لَهُم مِّن دُونِهِ مِن وَلِيٍّ وَلَا يُشْرِكُ فِي حُكْمِهِ أَحَدًا{{
{{Sema: Mwenyezi Mungu Anajua zaidi muda waliokaa. Ni Zake tu siri za mbingu na ardhi. Kuona kulioje na kusikia Kwake! Hawana mlinzi isipokuwa Yeye, wala Hamshirikishi yeyote katika hukumu Yake}}
Allaah سبحانه وتعالى Anamuelezea Mtume صلى الله عليه وآله وسلم muda waliokaa pangoni kuanzia wakati Alipowapa usingizi wa kufa hadi wakati Alipowafufua na walipojulikana na watu wakati ule. Muda wenyewe ulikuwa ni miaka mia tatu na tisa kwa miaka mwezi. Tofauti baina ya miaka mwezi mia moja na miaka jua mia moja ni miaka mitatu. Ndio maana baada ya Allaah سبحانه وتعالى kutaja miaka mia tatu Ameongeza miaka tisa. Yaani miaka 3 x 3 = 9.
}} قُلِ اللَّهُ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثُوا{{
{{Sema: Mwenyezi Mungu Anajua zaidi muda waliokaa}}
Maana, "utakapoulizwa kuhusu muda waliokaa na wewe huna elimu kwayo kutoka kwa wahyi wa Allaah سبحانه وتعالى, basi usijibu kitu bali jibu kuwa:
}}اللَّهُ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثُوا لَهُ غَيْبُ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ{{
{{Mwenyezi Mungu Anajua zaidi muda waliokaa. Ni Zake tu siri za mbingu na ardhi}}
Maana, hakuna yeyote anayejua jambo hilo isipokuwa Mwenyewe Subhana Wa Ta'aala na viumbe Alivyovichagua kuwajulisha. [Hii ni rai ya ma'ulamaa zaidi ya mmoja kama Mujaahid na wengineo waliokuja katika kizazi cha mbele].
}}وَلَبِثُوا فِي كَهْفِهِمْ ثَلَاثَ مِائَةٍ سِنِينَ وَازْدَادُوا تِسْعًا {{
{{Na walikaa katika pango lao miaka mia tatu, na wakazidisha tisa}}
Qataadah amesema, hii ni rai ya Ahlul-Kitaab (Watu Waliopewa kitabu) na Allaah سبحانه وتعالى Ameikanusha kwa Kusema:
}} قُلِ اللَّهُ أَعْلَمُ بِمَا لَبِثُوا{{
{{Sema: Mwenyezi Mungu Anajua zaidi muda waliokaa}}
Maana, Allaah سبحانه وتعالى Anajua zaidi kuliko wanayosema watu [At-Twabari 17:647]. Hii pia ilikuwa ni rai ya Mutwarraf bin 'Abdullah [At-Twabari 17:648]. Lakini rai hii iko wazi kujadiliwa kwa sababu Ahlul-Kitaab walivyosema wameishi katika pango kwa muda wa miaka mia tatu bila ya kutaja miaka tisa, walikuwa wakikusudia miaka jua na si miaka mwezi (kama ambavyo Waislam tunavyotumia kwa kalenda zetu) na Allaah سبحانه وتعالى Amesimulia yale waliyotaja kwani Asingelisema:
}}وَازْدَادُوا تِسْعًا{{
{{na wakazidisha tisa}}
Maana iliyo dhahiri ya ayah ni kwamba Allaah سبحانه وتعالى Kutaja uhakika wenyewe na Hakusimulia yale waliyosema Ahlul-Kitaab. [Hii ni rai ya Ibn Jariyr رحمه الله]. Na Allaah سبحانه وتعالى Anajua zaidi.
}}أَبْصِرْ بِهِ وَأَسْمِعْ{{
{{Kuona kulioje na kusikia Kwake!}}
Yeye Allaah سبحانه وتعالى Anawaona na Kuwasikia. Ibn Jariyr amesema, "Lugha imetumika hapa ya ufasaha kudhihirisha himdi (sifa) ya Allaah سبحانه وتعالى " [At-Twabariy 17:650]
Kifungu cha maneno haya kinaweza kufahamika kwa kumaanisha jinsi gani Allaah سبحانه وتعالى Alivyokuwa na uwezo wa Kuona kila kilichokuweko na jinsi gani Alivyokuwa na uwezo wa Kusikia kila kinachosikilizwa kwani hakuna kinachofichika Kwake.
Inasemekana kuwa Qataadah amesimulia katika aya hii,
}}أَبْصِرْ بِهِ وَأَسْمِعْ{{
{{Kuona kulioje na kusikia Kwake!}}
"Hakuna anayesikia au kuona zaidi ya Allaah سبحانه وتعالى" [At-Tabariy 17:650]
Maana, Yeye Allaah سبحانه وتعالى Ndiye Mwenye uwezo wa Kuumba na Kuamrisha, Ambaye Ufalme Wake hakuna wa kuupindua. Hana mshauri, msaidizi wala mshirika, Mola Mtukufu Subhanah wa Ta'ala.
Mafunzo na uongofu tunayopata: [Shaykh Abubakar Al-Jazaairy]
1. Mja kuwa na Adabu na Allaah سبحانه وتعال kutokusema 'nitafanya jambo fulani' ila baada ya kusema InshaAllaah.
2. Adabu ya mja anaposahau kumtukuza Allaah سبحانه وتعالى amtaje japo kuwa baada ya muda kupita anapokumbuka. Na akiapa basi hakimfai kiapo mpaka amtukuze isipokuwa ikiwa imeambatana na maneno yake pale pale.
3. Utajo sahihi wa muda waliokaa vijana katika pango kwa muda wa miaka mia tatu na tisa kwa hesabu ya miaka mwezi (hesabu tunayofuata waislam katika kalenda yetu)
Mwisho wa kisa
- Login or register to post comments
- Email this page
- Chapisha


