Inafaa Kutokuvaa Hijaab Kwa Khofu Ya Wazazi Wake Kujua Kama Kasilimu?

 

Inafaa Kutokuvaa Hijaab Kwa Khofu Ya Wazazi Wake Kujua Kama Kasilimu? 

 

Alhidaaya.com

 

 

SWALI:

Shukrani zote zinamstahikia Allaah, kuna mwanafunzi mwenye asili ya kihindi anayeendlea na masomo yake nchini urusi amesilimu na hataki wazazi wake wajue ili kukamilisha azma hiyo ameamua kutojitofautisha kama alivyo kuwa mwanzo ikwa pamoja na kutovaa hijaab, je inajuzu kufanya hivyo?

 

 

JIBU:

 

AlhamduliLLaah Himidi Anastahiki Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa) Rabb wa walimwengu, Swalaah na salamu zimshukie Nabiy Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhwiya Allaahu 'anhum) na waliowafuata kwa wema mpaka Siku ya Mwisho.

 

Mas-alah ya Dini ya hasa ya kuvaa Hijaab kwa mwanamke wa Kiislamu si mas-alah ya khiyari bali ni wajibu kwake akiwa ni Muislamu au amesilimu kutekeleza wajibu huo. Allaah (Subhaanahu wa Ta'aalaa) Anasema:

 

وَمَا كَانَ لِمُؤْمِنٍ وَلَا مُؤْمِنَةٍ إِذَا قَضَى اللَّـهُ وَرَسُولُهُ أَمْرًا أَن يَكُونَ لَهُمُ الْخِيَرَةُ مِنْ أَمْرِهِمْ ۗ وَمَن يَعْصِ اللَّـهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا مُّبِينًا ﴿٣٦﴾

36. Na haiwi kwa Muumini mwanamme na wala kwa Muumini mwanamke, Anapohukumu Allaah na Rasuli Wake jambo lolote, iwe wana hiari katika jambo lao.  Na anayemuasi Allaah na Rasuli Wake, basi kwa yakini amepotoka upotofu bayana. [Al-Ahzaab: 36]

 

Naye ikiwa amejisalimisha katika kukubali dini ya haki basi inampasa asiogope mtu yeyote ila Muumba wake pekee. Hivyo ni lazima athibitishe Uislamu wake na atambue kuwa ni kawaida ya wengi wanaosilimu bila ya wazazi wao kupatwa na mitihani kama hiyo. Kuvumilia na kuwa imara katika dini yake ya haki ni jambo linalompasa. Wazazi wake hawana majukumu naye tena katika mas-alah ya dini, bali ni yeye mwenyewe ajiamulie yanayompasa kutekeleza amri za Mola. Wazazi wanabakia kuwapa heshima yao na kuwafanyia ihsaan (wema) kama kawaida.

 

Ingawa wazazi wanayo haki kwako ya kuwatii amri zao, lakini haipasi kuwatii katika maasi au amri zozote za Rabb Muumba. Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta’aalaa):

 

وَوَصَّيْنَا الْإِنسَانَ بِوَالِدَيْهِ حَمَلَتْهُ أُمُّهُ وَهْنًا عَلَىٰ وَهْنٍ وَفِصَالُهُ فِي عَامَيْنِ أَنِ اشْكُرْ لِي وَلِوَالِدَيْكَ إِلَيَّ الْمَصِيرُ ﴿١٤﴾وَإِن جَاهَدَاكَ عَلَىٰ أَن تُشْرِكَ بِي مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ فَلَا تُطِعْهُمَا ۖ وَصَاحِبْهُمَا فِي الدُّنْيَا مَعْرُوفًا ۖوَاتَّبِعْ سَبِيلَ مَنْ أَنَابَ إِلَيَّ ۚ ثُمَّ إِلَيَّ مَرْجِعُكُمْ فَأُنَبِّئُكُم بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ ﴿١٥﴾

14. Na Tumemuusia insani kwa wazazi wake wawili. Mama yake ameibeba mimba yake kwa udhaifu juu ya udhaifu, na kumwachisha ziwa katika miaka mwili; ya kwamba, unishukuru Mimi, na wazazi wako; Kwangu ndio mahali pa kuishia. Lakini wakikushikilia kuwa Unishirikishe na ambayo huna elimu nayo, basi usiwatii. Na suhubiana nao kwa wema duniani, na fuata njia ya anayerudi kutubia Kwangu. Kisha Kwangu ndio marejeo yenu, na Nitakujulisheni yale mliyokuwa mkiyatenda. [Luqmaan:14- 15]

 

Swahaba wa mwanzo kuingia katika Uislamu walipatwa na mitihani mikubwa zaidi ya mateso kutoka kwa Makafiri na wengine kutoka kwa wazazi wao lakini hawakurudi katika ukafiri bali walithibitika katika Uislamu na kupokea hiyo mitihani ambayo ni kama majaribio ya kuhakisha Uislamu wa mtu:

 

أَحَسِبَ النَّاسُ أَن يُتْرَكُوا أَن يَقُولُوا آمَنَّا وَهُمْ لَا يُفْتَنُونَ ﴿٢﴾وَلَقَدْ فَتَنَّا الَّذِينَ مِن قَبْلِهِمْ ۖ فَلَيَعْلَمَنَّ اللَّـهُ الَّذِينَ صَدَقُوا وَلَيَعْلَمَنَّ الْكَاذِبِينَ ﴿٣﴾

Je, wanadhani watu kwamba wataachwa kwa kuwa wanasema: Tumeamini. Nao ndio wasijaribiwe? Kwa yakini Tuliwajaribu wale wa kabla yao, ili Allaah Awatambulishe wale walio wakweli na ili Awatambulishe walio waongo. [Al-'Ankabuut: 2-3]  

 

Ama kuhusu Hijaab Allaah Anatubainishia wazi kabisa pale Aliposema:

 

يَا أَيُّهَا النَّبِيُّ قُل لِّأَزْوَاجِكَ وَبَنَاتِكَ وَنِسَاءِ الْمُؤْمِنِينَ يُدْنِينَ عَلَيْهِنَّ مِن جَلَابِيبِهِنَّ ۚ ذَٰلِكَ أَدْنَىٰ أَن يُعْرَفْنَ فَلَا يُؤْذَيْنَ ۗ وَكَانَ اللَّـهُ غَفُورًا رَّحِيمًا ﴿٥٩﴾

Ee Nabiy! Waambie wake zako, na mabinti zako, na wanawake wa Waumini wajiteremshie jilbaab zao. Hivyo kunapeleka karibu zaidi watambulikane (kwa heshima) wasiudhiwe. Na Allaah daima ni Mwingi wa kughufuria, Mwenye kurehemu. [Al-Ahzaab: 59].

 

Jambo muhimu la sisi kujiuliza je, Hijaab ya Kiislamu inafaa iwe vipi? Au masharti ya kivazi cha Kiislamu ni yepi? Masharti ni kama yafuatayo:

 

- Vazi kuwa pana.

- Kutoonyesha maumbile wala vilivyo ndani.

- Kusitiri uchi.

- Kutokuwa na mapambo aina yoyote.

- Kutofanana na vazi la kikafiri.

- Kutokuwa vazi la kujionyesha na kujifakharisha.

- Liwe halifanani na vazi la mwanamme.

 

Ushauri wetu utakuwa ni yeye awe ni mwenye kuvaa vazi lenye sifahizo.

 

Tunamuombea dada yetu kila la khayr aweze kuvuka mtihani huo kwa salama kabisa. 

 

 

Na Allaah Anajua zaidi.

 

Share